ANAOMBA RADHI

 


Adeladius Makwega-MWANZA

Tangu mwaka 2019 hadi Machi 12, 2023 mwanakwetu alikuwa akisali Kanisa la Bikira Maria Imakulata, Parokia ya Chamwino Ikulu, Jimbo Kuu Katoliki la Dodoma, huku Jumuiya yake ikifahamika kama Mtakatifu Sesilia inayoongozwa na Mwenyekiti Bernard Lubogo jumuiya iliyo mkono kulia wa Ikulu ya Chamwino. Katika kipindi chote hicho mwanakwetu amejifunza mambo mengi ya maisha binadamu yawe ya kimwili na ya kiroho, huku wingi huo kama yakiandikwa basi yanaweza kujaa kitabu chenye kurasa nyingi.

Siku ya leo msomaji wake anatamani akusimulie tukio moja ambalo ninaamini jamii ya Wakristo na hata ya wale Imani zingine wanaweza wakalitazama kama jambo hilo lina umuhimu basi wakalifanya maana ni funzo kutoka katika Parokia hii ya Chamwino Ikulu.

Je jambo hilo ni lipi?

Ambatana na simulizi hii ya siku ya leo hatua kwa hatua.

Mwaka 2022 Parokia hii Jumapili mojawapo ilikuwa ni siku Wanaume Wakatoliki (UWAKA), siku hiyo iliamuliwa kuwa UWAKA wote ndiyo wawe wahudumu wa kanisani, kabla ya misa na hata wakati wa siku ya misa hiyo ya dominika. Jumamosi kabla ya misa hii wanaume hao walifika na kufanya usafi wa kanisa lao na mazingira yote ndani na nje akiwamo mwenyekiti wa Parokia hiyo Ndugu Komba na Katibu wake Dkt.David Msimbe.

Siku hiyo hakuwepo mwanamke hata mmoja hivyo kila idara ya kukamilisha usafi na maandalizi ya misa ya Jumapili wanaume walikuwa kazini, kila mmoja akiwajibika, wapo kanisani, wengine nje kanisa na wengine walikuwapo vyooni. Kanisa lilifanyiwa usafi vizuri huku frateri ambaye alikuwa anatokea Kongo(Zaire) akishirikiana na wanaume hao Wakatoliki tangu mwanzo hadi mwisho.

Wakati zoezi hilo likiendelea sabuni za kufanyia usafi ikawa imekwishwa, Baba anapokuwa nyumbani kitu kikiisha anamuuliza nani? Jukumu lake kutoa pesa na kununua.Ndugu hawa waliokuwa wakifanya usafi chooni wakaamua wakanunue sabuni hiyo dukani ili kukamilisha usafi wa vyoo vyao vya Kanisa lao. Mmojawapo akaenda kununua sabuni duka jirani. Hapo kulikuwa na duka nyuma ya kanisa hilo kuvuka Jiko la Nyerere (ambalo ni jengo lililo jirani na kanisa hilo ikiaminika kuwa zamani wakati wa utawala wa mwalimu Nyerere eneo hili lilitumika kumpikia chakula chake akiwa Ikulu ya Chamwino na wakati huo eneo hili likiwa sehemu ya Ikulu). Alikwenda kununua alijiongeza mno alinunua pakiti kadhaa za sabuni za unga na vipande na pia alinunua dazeni ya pakiti za sodo za dharura.

Kama unavyofahamu mazingira ya dukani wateja wanakuwa wanawake kwa wanaume  wakawa wanashanga mbona ndugu huyu ananunua dazeni nyingi za sodo ? Kushangaa ilikuwa haki yao lakini kuuliza walishindwa.Akabeba mzigo wake hadi Kanisani.

Akafika na kuendelea na kazi na kuchukua sabuni wakafanya usafi wa vyoo vya wanaume na wanawake ambayo vilikuwa na vyumba kadhaa.Wakafanyia usafi vyombo vyote vya chooni pande zote mbili. Upande wa wanawake ulikuwa na jaba mojawapo kubwa likajazwa maji vizuri alafu mfuko wenye dazeni ya sodo ukaingizwa na kupachikwa eneo mojawapo vizuri. Kabla ya kuwekwa sodo hizo hapo Katibu wa UWAKA wa parokia alijulishwa kufanyika kwa jambo hilo.Aliyeshuhudia tukio hilo hakuweza kulikumbuka jina la kiongozi huyu lakini aiba yake tu ilikumbukwa alikuwa mtu mmoja mrefu, mweusi mwenye mwili wa uliojengeka. Kazi ikawa imekamilika milango ya vyoo ikarudishwa vizuri tayari kwa matumizi ya wahitaji siku iliyofuta. Vyoo hivyo vya kisasa vilikuwa na maji muda wote maana Kanisa hilo lina matenki makubwa ya kuhifadhi.

Jumapili ilifika na misa kusaliwa vizuri, mama mmoja ambaye anasali hapo alisema sodo hizo zilipata wahitaji, hoja ya kuandaa kupatikana kwake Zaidi ilianza lakini lilikuwa wazo la mtu mmoja. Mtu huyo baadaye alijitahidi wakati jumuiya yake inapokuwa zamu aliweza kushirikiana na akina mama kuweka sodo hizo katika vyoo vya wanawake, kila jumuiya yake ikiwa zamu.

“Hizi sodo zinakaa muda mchache maana mtu anaweza kuvutiwa kuchukua awezavyo, lakini hilo linaonesha kuwa wahitaji wapo.” Mama mmoja wa Jumuiya ya Mtakatifu Sesilia alinukuliwa. Utafiti ulibani kuwa baadhi ya wanafunzi walikuwa wanapita na kujihudumia siku ambazo sodo hizo zilipokuwapo, inawezekana wanafunzi hao waliokuwa wanasali hapo waliwauma sikio wenzao kupatika kwa bidhaa hiyo.

Mwandishi wa makala haya anaamini kuwa kama Parokia yoyote ile ikijiwekea utaratibu kila Jumuiya Katoliki ikiwa zamu lazima kununua dazeni kadhaa za sodo na kuziweka na ikawa huduma ya kudumu katika maliwato ya wanawake wa kila Kanisa litakuwa jambo jema, tendo hilo litakuwa tendo la utu mkubwa kwa kila mwanamke na kila mwanamme maana wanaume wote wamezaliwa na wanawake.

Wahitaji watakuwa wengi na tendo hili linaweza kuwavutia hata wapita njia na kuona wema kwa walioifikisha bidhaa hiyo na hata kuvutiwa na imani hiyo pia. Je tendo hilo kufanywa ni baya au zuri? Huu ukiwa ni utaratibu wa jamii uliojiwekea wenyewe linakuwa jambo zuri na la heshima kwa mwanamke.

Mwanakwetu mimi na wewe tumeweza kuzaliwa baada mama zetu kuwa na afya njema ya uzazi, basi wewe na mimi tufanikishe hilo kwa wahitaji ni kulinda afya njema ya uzazi kwa mwanamke popote alipo. Tukio hili pengine haliweza kuwa linafahamika na wengi hata wanaosali katika kanisa hilo la Bikira Maria Imakulata ndiyo maana mwandishi aliyelifuatilia kisa hiki ameamua leo hii kukisimulia.

Naweka kalamu yangu chini kwa kusema kuwa kama tendo hili ni la kiutu basi bila kujali imani zetu tuliige na kama mwandishi amekosea kwa hisani yako msomaji wake anaomba radhi.

makwadeladius@gmail.com

0717649257

0/Post a Comment/Comments