MAFIGA YANAYOBEBA CHUNGU YANAFANANA

 


Adeladius Makwega-MWANZA

Hivi karibuni mwanakwetu alizungumza na rafiki yake mmoja ambaye alitaka kujua kwanini hasemi chochote juu ya kiongozi mmoja mkubwa wa taifa moja kutembelea taifa letu? Mwanakwetu alijibu ni kweli hataki kuzungumzia kabisa jambo hilo kwa kuwa kwa miaka zaidi ya kumi nyuma anafahamu msimamo wa chama kinachotawala katika taifa hilo katika kuunga mkono mahusiano ya jinsia moja. Anachoamini yeye hata kumtaja jina lake, kumuandika au kupachika picha yake kiongozi huyo kwa namna yoyote ile ni kuunga mkono msimamo wao katika hilo.

Je inakuwaje kujisogeza jirani naye?

Hilo mwanakwetu hana jawabu lakini anavyoamini yeye ndiyo hivyo.

“Mafiga yanayopachikwa chungu lazima yalingane, kinyume chake chungu hakiwezi kukaa mekoni na chakula vigumu kupikwa na kuiva.”

Mwanakwetu alimuongezea nduguye huyo.

Ili kumfahamu huyu ndugu huyu yeye ni msomi mwenye Shahada ya Uzamivu ya Sheria, akisema mwanakwetu umezungumzia suala la maadili, hilo ni jambo la msingi mno kwa watoto, vijana wetu na taifa letu pia.

Mazungumzo hayo yalipamba moto na baadaye mwanakwetu kusimuliwa kisa hiki cha kweli cha mtoto wa msomi huyu.

“Nina kijana wangu anasoma Chuo Kikuu sasa, yu mwaka wa tatu, mwaka jana nilishangaa anaingia nyumbani kwangu yupo yeye na binti amebeba mtoto. Kama baba nilishangaa, ebo sasa nimepata mjukuu? Mbona sijashiriki kulipa mahari na harusi? Nikawauliza hapo hapo huku wamesimama, haya kulikoni? Chuoni kwema? ‘Baba ni kwema huyu ninasoma naye chuoni na nilikuwa nakaa nae, tukapata mtoto, ndiyo hivyo tena na leo nimekuja naye hapa nyumbani’ Hiyo ndiyo digrii niliyokutuma ukasome? ‘Baba hapana, nimekosa, naomba msamaha.’ Haya na wewe mama hiyo ndiyo kazi waliyokutuma wazazi wako ukafanya huko chuoni? ‘Hapana baba ilikuwa ni bahati mbaya tu.’ Ndugu yangu mwanakwetu nilikaa kimya kwa dakika tano huku wao wamesimama, mke wangu ananitazama na wanangu wadogo wako pembeni, nikawauliza jina la huyu mtoto, walivyokuwa washenzi wamempa jina langu, nikawaambia nani kawaruhusu kumpa jina langu mtoto wenu? Hakuna jibu lililotolewa. Nikasema kumbe sasa mwanangu umekuwa mkubwa na umeyaanza majukumu, nakupa hongera sana (hongera ya dhihaka alisema moyoni baba huyo), sasa wewe, mkeo na huyo na mtoto wenu sitaki kuwaona katika nyumba hii ninayolala mimi, mke wangu na wanangu wadogo. Nakuomba sasa hivi beba kilicho chako ukakae kule nje katika banda la uani na kuanzia leo uanze kujitegemea maana maisha unayaweza na ndiyo maana umemchukua binti wa watu unakaa naye unyumba, sintakupa chochote, sasa anza kujitegemea.”

Msomi huyu alisema kuwa Kweli kijana huyu alichukua vitu vyake na kuhamia katika kibanda hicho na kuanza maisha huku wakifanya vibarua vidogo vidogo akimtunza binti huyu aliyezaa naye. Walikaa hapo hadi likizo ilipoisha walirudi chuoni.

“Kaka wakirudi tena likizo ya pasaka nafungisha ndoa waendelee na maisha yao.”

Ndugu huyu alimwambia mduguye mwanakwetu, hizi tabia siyo nzuri na lazima wazazi tuwe wakali katika haya mambo ya haki za watoto yana shida sana leo na hata kesho yao badala ya kusoma vizuri sasa wana majukumu ya kutunza mtoto

Mwanakwetu akamwambia hilo ni sahihi maana hata wanao wadogo watakuwa wamejifunza kuwa wakijaribu kuingia huko balaa kama hilo linaweza kuwambuka kama la kaka yao. Ungefanya kosa kubwa kama ungekaa kimya na pale unapomuambatanisha mtu mwema na mtu mwovu, hoja itakuwa kama ile ya mafiga jikoni chakula hakiweza kupikika.

Mwanakwetu akasema mara zote jamii inachukizwa na tabia mbaya na inavutiwa mno na mtoto/kijana mwenye tabia nzuri. Kama anavyofahamika mtu mwovu na hata mwema huwa anajulikana na kupendwa na wengi kwa mwenyewe kufahamu au kwa kutokufahamu. Mwanakwetu akaamua kumsimulia ndugu huyu simulizi hii,

“Kaka Kati ya mwaka 2005-2008 nilikuwa mwanachuo cha Tumaini Iringa nikisoma na wanachuo wengi, kuna nyumba moja alikuwa akiishi rafiki yangu anayefahamika kama Hendry Msaki, ndani ya nyumba hiyo walikuwapo wapangaji kati 25-30 wanachuo tupu wakike kwa wakiume wenye tabia tofauti. Nyumba hii nilikuwa nikienda kuwatembelea rafiki zangu kadhaa. Miongoni mwa wanachuo waliokuwa wakiishi katika nyumba hiyo alikuwepo dada mmoja anayefahamika kama Deborah ambaye alikuwa anasoma Shahada ya Kwanza katika Uongozi wa Biashara (BBA). Binti huyu alikuwa na sifa kubwa nne ya kwanza ni mtulivu mno, pili ni mshika dini, tatu alikuwa anajiheshimu sana na nne alikuwa na umri mdogo kuliko wote katika nyumba hiyo. Msaki na mwanakwetu hawakupenda Deborah aonewe na mtu yoyote yule awe chuoni, awe anarudi anapokaa au katika makazi hayo maana upole wake, utulivu wake uliwavutia mno kaka zake hao. Deborah akiwa mwanachuo gafla ilisikika amefunga ndoa, wengi walitamani kujua Deborah ameolewa na nani? Mbona hatukumuona huyo mchumba wake kaja kumtembelea? Mbona hatukuona pete ya uchumba? Lakini Deborah alikuwa sasa ameolewa. Kumbe kaka yao akina mwanakwetu, waliokuwa wanafanya naye siasa ndugu Addo Novemba Mwasongwe ndiye aliyefunga ndoa na Deborah Binti Mtulivu.”

Mwanakwetu alipomaliza kumsimulia nduguye huyu msomi wa sheria yeye alisema kuwa watoto/vijana wengi wanapotea sana kwa kutokuwa makini na maisha yao huku wakivutiwa na maisha ya kimaigizo ya wazungu. Kweli mazungumzo haya yalimalizika na kila mmoja kuendelea na ratiba yake ya siku hiyo.

Mwanakwetu siku ya leo anasema nini?

Swali ambalo lilibaki wakati huo lilikuwa huyo aliyemuoa Deborah alimfahamia wapi? Mbona hakuwa mwanachuo? Mwanakwetu akamwabia rafiki yake Hendry Msaki ambaye sasa ni marehemu kuwa kama kinavyofahamika kibaya na wabaya na hata kizuri kinafahamika zaidi na wazuri. Hilo walifahamiana wapi litabaki kwao wenyewe Deborah na mumewe Mchungaji Addo Novemba Mwasongwe. Deborah huyu anayezungumziwa leo hii ndiye Mke wa Mchungaji huyo. Mwanakwetu kwa heshima zote ametumia kisa cha Deborah Mama Mchungaji kujenga matini yake juu ya maadili kwa vijana wetu popote walipo baada ya kukiacha tu kisa cha wanachuo waliopeana uja uzito kusimama pekee. Kwa hoja moja kubwa mazuri lazima yasemwe zaidi. Mwanakwetu kwa matini haya anatawakia maisha mema ya ndoa ya familia hiyo ya Mchungaji Addo Novemba Mwasongwe popote walipo siku ya leo.

Kwako wewe msomaji wangu kumbuka kuwa, “Mafiga yanayobeba chungu yanafanana.”

Nakutakia siku njema.

makwadeladius@gmail.com

0717649257

 

 

 

 

0/Post a Comment/Comments