MAJI YALE MENGINE

Adeladius Makwega-MWANZA

Miaka ya 2000 mwanakwetu alikuwa mkaazi wa Iringa Mjini na baadae akawa akienda huko na kuondoka hadi mwaka 2011, mji huu ambao ulikuwa Ngome ya Mkwawa LILINGA. Katika maisha yake katika eneo hilo alifahamu mengi ya watu wengi wa eneo hilo lenye historia moja kubwa ya Tanzania na kidunia. Akikutana na watu wengi wasomi wa mkoa, wanasiasa na hata wanahabari wa kitaifa na kimataifa waliotapaka ulimwengu mzima.

Mwanasiasa ambaye alikutana naye kwa karibu na hata kufika nyumbani kwake ni marehemu Josephy Mungai ambaye alikuwa na urafiki wa karibu sana ni mwanahabari mkongwe Majidi Mjengwa.

Kumbukumbu za mwanakwetu zinamrejesha wakati huo kuna siku moja alialikwa nyumbani kwa mheshimiwa Mungai ambaye alikuwa waziri katika serikali kadhaa za awamu hizo. Makazi ya mheshimiwa Mungai yalikuwa katikati ya Ofisi za CCM Wilaya Iringa Mjini na Chuo cha Ruaha, jirani na makazi ya akina Abri hawa wafanyabiashara wa Iringa. Waziri Mungai alikuwa na nyumba yake moja ya kawaida tu haikuwa nyumba ya kibepari akiishi yeye na familia yake, huku watoto wake wengine wakubwa waliashanza maisha yao maeneo mengine, hapo akiishi yeye, mkewe na watoto wake wadogo.

Mwanakwetu alipofika hapo alibaini kuwa palikuwa na sherehe ya siku ya kuzaliwa ya mtoto wa mheshimiwa huyu mdogo na waalikwa wengi walikuwa ni watoto labda walikuwa wakisoma na mtoto huyu. Hapo mwanakwetu alikutana na mwanahabari mkongwe Majidi Mjengwa, mwanakwetu akasema kumbe hayupo peke yake, akapata mtu wa kuongea naye. Kwa heshima waliyopewa mwanakwetu na Mjengwa walingizwa sebuleni kwa mheshimiwa Waziri Mungai. Sebule hii ilikuwa ya kawaida tu yenye makochi machache, mapazia ya kawaida, meza ya kulia chakula na picha ya mheshimiwa Mungai ukutani.

Kumbuka katika ua wa nyumba ya waziri ndipo sherehe inafanyika watoto na vijana wakicheza muziki. Mama mwenye mji huu akaagiza wageni wa Waziri Mungai wapewe vinywaji. Binti mhudumu akapiga goti mbele ya Mjengwa na mwanakwetu, Mwanakwetu akiwa bado hajaoa lakini Mjengwa akiwa ana mke na watoto kadhaa. Mwanakwetu alikuwa na ruhusa ya kutia neno la mapenzi kwa binti mhudumu nyumbani kwa waziri, lakini Mjengwa alikuwa hana kibali hicho maana kufuri ya ndoa ilimbana.Hata kama Mjengwa angetia neno kwa binti huyo mwanakwetu akamchoma kwa mkewe mara moja, lakini hili halikutokea.

“Haya tuwaletee nini?” binti huku kapiga goti alisema, waungwana hawa wakaagiza soda kwa pamoja. Hapo sasa mwanakwetu akatambua kuwa Majidi Mjengwa siyo mnywaji wa maji yalee.

Waagizwaji wanacheka, inakuwaje ndugu hawa vijana wenzetu wanakunywa soda? Muonekano wa Majidi Mjengwa mtu mwembamba alionekana kijana mdogo kumbe alikuwa kaka mkubwa kwa mwanakwetu.

Kwa mazingira ya Iringa watu wengi wanakunywa pombe ya ulanzi na pombe zingine, mazoezi ya kunywa Ulanzi tangu utoto yanampa mtu uzoefu wa pombe na kumbuka Ulanzi una hatua kadhaa zenye utamu mwingi unavutia mtu kunywa hadi kuwa pombe kamili.

Mama mheshimiwa akasema sasa wageni wenyewe wa soda waleteeni boksi za juisi kila mmoja.

Msomaji wangu tambua kuwa mheshimiwa Mungai alikuwa waziri aliyefanya kazi tangu Nyerere, Mwinyi na Mkapa. Waungwana hao wapo hapo wanakunywa juisi huku wanaongea habari zao, kiongozi wa mazungumo hayo alikuwa Mjengwa akasimulia simulizi nyingi na ya kwanza ilikuwa ya Mfalme Umekaa Vibaya simulizi hiyo ikaisha baadaye ikaja simulizi ya Siyo Kila Anayekupa Kitu Anakupenda.

Dhana ya Mjengwa siku hiyo ilijengeka katika kisa cha mama mpishi aliyepo jikoni anapika, mandhari ya jikoni sakafuni yupo paka aliyevutiwa na mapishi ya mama, paka anampapasa miguuni mama mpishi na huku paka huyu ambaye siye pakashume akivutiwa na harufu ya mapishi ya mama mwenye nyumba. Mama anampikia mumewe akirudi kazini ale. Paka anamgasi mama na kumtambaa miguuni. Mama mpishi anakerwa na tabia hiyo huku akimfukuza paka awe mbali naye lakini paka anaendeleza na vurugu zake, mara kamramba miguu mara kampalamia, mara kamkwaruza, mama mpishi anarusha miguu na kumsukuma kando paka huyu.

Ghasia hizo zikamkera mama mpishi hivyo akachukua upawa akachota kipande cha nyama chanye fupa lililokaa kama kisu na akamtupia paka huyu mwenye uchu na mapishi yanayopikwa mekoni.

Paka alipotupiwa akalifakamia fupa hilo, likamuunguza na kumkaba kooni. Mama sasa anaendelea na mapishi na alitoa finyango hilo si kwa kupenda bali kuondoa kero ya kupapaswa, kukwaruzwa na kusumbuliwa na paka ili aweze kupika vizuri na kumgoja mumewe aje kula chakula hicho. Fupa lile likamsumbua paka likamnasa koo na kumbana pumzi likasababisha paka akafa.

Kumbuka hapo juisi zipo mezani kazi ni simulizi, boksi za juisi zikisafiri kutoka mezani kwenda koonimandhari ni nyumbani kwa mheshimiwa Waziri Mungai.

Gafla zikasikika hatua za viatu vya kiume zikishuka ngazi akatokea mheshimiwa Mungai kutokea ngazi za juu ya nyumba yake hii, akawasalimu huku Mjengwa na mwanakwetu wakisimama kwa heshimu zote, ukafanyika utambulisho kidogo alafu soga zikapamba moto. Mheshimiwa Mungai akaagiza waungwana hao waletewe vinywaji Zaidi, hapo sasa boksi za juisi zilijaa mezani, huku wahudumu wakiwacheka zaidi wageni wa mheshimiwa waziri wanakunywa juisi ?


Kiongozi wa mazungumzo haya sasa alikuwa mheshimiwa Mungai huku wanahabari hao wakayanukuu maelezo yake kwa kutumia kinasa sauti cha mwanakwetu. Sherehe iliendelea hadi saa moja usiku na ilipoisha Mjengwa aliwakusanya watoto wake na kurudi zake kwake naye mwanakwetu alirudi nyumbani kwake huko Mwangingo.

Msomaji wangu tambua kuwa tangu Majidi Mjengwa wakati huo alikuwa akiandika makala, chambuzi na habari mbalimbali katika magazeti maarufu yote na maelezo haya yalipamba katika vyombo vya habari mbalimbali baada ya kikao hicho na mheshimiwa Mungai.

Mwanakwetu anasema nini siku ya leo?

Msomaji wangu tambua kuwa mwanakwetu amemkumbuka kaka yake Majidi Mjengwa, huku akijenga tafakari ya ule mwaliko nyumbani kwa mheshimiwa Mungai na pia anakumbuka hiki kisa cha cha mama mpishi mekoni, kubwa siyo kila anayekupa kitu anakupenda.

Swali ni je Mungu anaweza kuufilisi ulimwengu na kukosa watu rahimu? Hilo haliwezekani maana wapo watu ambao wanaweza kumpa mtu kitu huku wakimpenda

Mwanakwetu mpaka leo bado anakunywa juisi na soda, lakini anajiuliza je kaka yake Majidi Mjengwa katika kipindi chote cha miaka 20 aliyemwaacha Iringa je Ulanzi ulimshawishi kuunywa?

Kaka Mjengwa je umefuzu kuanza kunywa maji yale mengine ?

Mwanakwetu upo?

Nakutakia Siku Njema.

0717649257

 

 

 

 






0/Post a Comment/Comments