MALYA KWENDA HUNGUMALWA

 


Adeladius Makwega-MWANZA

Mwanakwetu hivi karibuni alisafiri kupitia katika vijiji kadhaa vilivyo katika tumbo la mikoa mitatu; Mwanza, Simiyu na Shinyanga huku akifaidi mno pale alipotumia bodaboda kwani katika ardhi hiyo ndiyo anafika kwa mara ya kwanza tangu azaliwe.

Safari hii kwa hakika ilizidi kumpa picha ya hali ya hewa na mwenendo wa matokeo ya mvua za mwaka huu wa 2023 katika mashamba ya wakulima wetu. Safari ya bodaboda ndiye ilimpa picha ya wazi mno huku macho yake yakikaribishwa na majani makavu ya mahindi yenye kimo kifupi yaliyokauka kana kwanza wakati wa kuvuna umekaribia lakini hayakuonesha kubeba chochote .

Hali hiyo ilianzia Malya huku mwanakwetu akienda eneo la Hungumalwa, hayo yakiwa majira ya jioni. Barabara ilikuwa ya vumbi lakini inayopitika vizuri sana ilimpa picha labda ilikuwa ikingoja mkandarasi aje kuweka lami.

Sasa walifika Kijiji Cha Lyoma, njiani walikutana na makundi matatu ya mifugo yenye ng’ombe wengi, mbuzi na punda wachache. Walitoka kijiji hicho walikwenda mwendo kidogo na kufika Kijiji Cha Busule na hapo pia walikutana na makundi mawili ya mifugo mingi wachungaji wakiwa nyuma yao.

Wakafika Kijiji cha Mwakulilinga alafu wakafika Kijiji cha Mwakulyambiti hapa walikutana shule moja nzuri ya msingi yenye majengo imara na mazuri yaliyojengwa zamani .

“Mna shule nzuri za msingi, zenye majengo mazuri, uzoefu wangu wa kuzunguka katika katika maeneo mbalimbali huwa naikosa mandhari hii ninayoiona leo hii.”

Mwanakwetu alimwambia kijana huyu wa bodaboda.

Safari iliendelea na walifika Kijiji cha Mwamakoye hapo hawakuona kundi la mifugo barabarani lakini makundi mengi yalikuwa yanaoneka mashambani. Kijana wa bodaboda akasema kuwa unayaona yale makundi ya mifugo hayapo barabarani bali yanalishwa mashamba ya mahindi maana mahindi mwaka huu yamegoma kabisa. Malisho haya si hapo tu bali tangu kule Malya.

Kijana huyu akasema kwa miaka mingi ambayo kilimo kinakuwa vizuri ni vigumu mfugaji kuweza kupitisha mifugo mashambani msimu huu maana hilo litakuwa hatari kubwa kwake na mifugo yake.

Kumbuka msomaji wangu inaendelea wakafika sehemu wakakutana na watu wakianua juani choroko zao na kuziweka katika magunia, tayari kusafirishwa, hapo zilionekana gunia kama nne hivi. “Hawa jamaa wamebahatisha mno kupata hizo choroko zao, wanatakiwa kuzitunza sana zitawafaa mno hapo baadaye.” Kijana wa Bodaboda alisema.

Sasa iliendelea wakawa wanakaribia Hungumalwa, kabla ya kufika hapo walipita sehemu walikutana watu wanakunywa pombe katika baa moja, kijana huyu wa bodaboda akasema kwa hali ilivyo mwakani inawezekana hata vilabu vya pombe vikapungua maana hayo mazao ya kupika pombe yatatoka wapi?

Wakafika mbele kidogo wakakutana na kundi la ng’ombe kubwa barabarani, hapo mchungaji wala hakuangaika kuwasogeza ng’ombe zake pembeni.“Kaka unajua matajiri wa ng’ombe wanaogopa magari tu si kinginecho na ndiyo maana hawahaingaiki kuziswaga kando.”

Bodaboda haiwezi kumpa madhara ng’ombe labda wewe ukimgonga ndiyo utaumia mwanakwetu alimwambia.

Safari iliendelea na baada ya muda midogo mwanakweru alifika Hungumalwa ambapo alibani safari hiyo ilikuwa ya saa nzima. huku akiambiwa kuwa kwa basi ni safari ya saa moja na nusu na kwa baiskeli saa tano na kwa miguu ni safari ya siku nzima.

Kumbe ujio wa bodaboda umeokoa saa 11 za kutembea kwa mguu kutoka Malya kwenda Hungumalya.Kwa kuwa mida huo ulikuwa Jioni kuelekea usiku mwanakwetu alifika Hungumalwa na kulala.

Mwanakwetu anasema nini siku ya leo?

Kwa hakika mandhari aliyoiona katika vijiji alivyovitaja na vingine vingi ambavyo majina yake hakuweza kuyanukuu vizuri hali ya hewa inachangamoto. Kwa yule mwenye ndugu zake maeneo hayo kama atapigiwa simu kuelezwa juu ya hali ya hewa ilivyo atambue kuwa hilo ni la kweli. Kwa mazingira aliyoyaona watu kunywa pombe ni kwa muda tu na pengine mazao ya mwaka jana ndiyo yanayotumika kufanya hivyo.

Mwanakwetu anatambua kuwa kuyasoma, kuyasikiliza na hata kuyaona haya ni hatua ya kwanza na kuyatatua ni hatua nyingine.

makwadeladius@gmail.com

0717649257

0/Post a Comment/Comments