NITAKUSIMULIA SIKU NYINGINE

 

Lucas Masunzu- MAKOLE

Mwaka 2017 nduguyetu alikuwa anaishi wilaya mojawapo inayopatikana Mkoa wa Tabora. Wilayani huko alibahatika kukutana na watumishi wa umma kadhaa ambao walikuwa wakifanya kazi katika ofisi mbalimbali za umma katika wilaya hiyo. Kwa muda alioishi na hao watumishi aliweza kubaini kuwa watumishi hao walitofauti katika umri, vyeo, dini, elimu na hata vimo vyao katika upembuzi wa mambo walitofautiana. Wenye umri mkubwa ndio watawahi kustaafu, kuruhusu wengine kuingia kwenye huo utumishi halafu wenye umri mdogo wataendelea kubaki kwenye foleni nao wakisubiri muda wao wa kustaafu! Hii ni kwa sababu utumishi wa umma ni wa muda mfupi mno, kipenga cha kuanza kazi kikipigwa kumbuka pia kuna muda kipenga hichohicho kitapigwa kukuengua kwenye utumishi huo maana tayari muda wako wa utumishi utakuwa umetamatika.

Miongoni mwa watumishi hao wa umma, nduguyetu alibahatika kukutana na mtumishi wa umma ambaye ni Shaaban Mgasi ambaye alikuwa ni mtu mwenye mwili uliojengeka kiasi, mpole, mvumilivu mno na mwenye kupenda haki. Mbali na utumishi wa umma alikuwa ni mkulima hodari wa mahindi na miwa. Kiumri mtumishi huyo alikuwa amebakiza miaka michache ili astaafu katika utumishi, apokezane kijiti na wale wanaoingia katika utumishi huo. Kubakiza miaka michache na kustaafu ni uneemevu pia ni ngekewa kubwa mno kwenye utumishi wa umma kuna nongwa na kadhia lukuki, ukikutana na mstaafu asikuache bure ongea nae anaweza kutengeneza darasa lenye tija kwako, ana mengi mno ya kukusimulia kwa maana umri wa miaka 60 amekutana na mambo mengi, amefanya kazi na watu mbalimbali wakiwamo wema na wale wenye nia ovu.

Jumapili moja Nduguyetu alikuwa amepumzika na nduguze chini ya mti wa mhama ambao ulikuwa karibu na duka. Kwa mbali alionekana mtu akitembea kwa mguu, akivalia kibalagashia kichwani kwake. Alipokaribia alikuwa ni mtumishi wa umma aitwaye Shaaban Mgasi ambapo tulifanya jaliko, tukampisha kwenye benchi ili aketi maana wote alituzidi umri. Kwa hisani yake mtumishi huyo wa umma   aliwanunulia soda kwenye duka lililokuwa karibu na mti huo wa mhama nao wakanywa. Nduguyetu na marafiki zake walifurahi sana wakaendelea na mazungumzo yaliyodumu kwa muda wa saa moja na dakika 49. Kwa kuwa aliwazidi umri na uzoefu, mtumishi huyo alitawala mazungumzo hayo, huku akituambia;

 “Utumishi wa umma una mambo mengi unapofurahia haki yako katika utumishi huo hakikisha haukanyagi haki za wengine, wawe wakubwa hata wale unaowaona ni wadogo wapatie haki yao, katu usiwe kizuizi wa kuikanyaga, wapo wanaokanyaga haki za wenzao kwa hila zao mbaya, kama mtabahatika kuwa viongozi katu nyie msiicheze hiyo ngoma! Pia, unapokuwa na cheo kiwe kikubwa au kidogo katika utumishi wa umma ishi na watu unawaongoza kwa usawa, usifanye upendeleo wa aina yoyote, kamwe usitumie nia yako ovu kunyanyasa wengine, dunia ni duara. Hata kama utakutana na mabaya yapokee tu ili maisha yaendelee mengine kashitaki kwa Mungu wako aliyekuumba. Mimi katika utumishi wangu mpaka sasa sijawahi kutenda hata kufikiria kuyatenda haya mabaya”.

Mazungumzo yalipamba moto, mtumishi huyo akasema “ngoja niwape nongwa mbili alizokutana nazo rafiki yangu katika utumishi wake wa umma”. Tulikaa kimya kusikiliza huku tukiendelea kunywa soda alizotununulia. Alianza kusimulia kisa kilichompata rafiki yake hapo kale.

“Mwaka 1989 rafiki yangu mmoja (kwa sasa sijui aliko) alikuwa Mkuu wa Shule katika moja ya shule kubwa ya Wavulana nchini. Siku moja mpishi mmoja wa zamu alibainika kuiba kilo za unga zilipowekwa kwenya mzani zilikuwa ni zaidi ya kilo arobaini za unga wa mahindi. Kilifanyika kikao kikakubaliana kuwa hilo ni kosa. Mwalimu aliyekuwa zamu siku hiyo alisema ndiyo maana watoto wamekuwa wakilalamika kuwa wanapata mchinjo (chakula kidogo) kwenye mlo. Mpishi alikiri kufanya hilo, kikao kikaamua mpishi huyo aandike barua ya kukiri kufanya kosa kwa rejea za baadaye huku wajumbe wa kikao hicho wakiomba busara itumike kumsamehe mpishi huyo ukizingatia kuwa mpishi huyo amekubali kufanya kosa hilo. Baadaye kitendo cha kuandika maelezo kilimuuma mno mpishi huyo aliona kuwa ameonewa na hajatendewa haki, akaamua kwenda kutafuta msaada anakojua yeye”.

“Mkuu wa shule ananitaka kimapenzi nimemkataa ameamua kunibambikizia kesi ya wizi wa unga” mpishi huyo aliamua kupika uongo huo na kila alipopiga hodi mpishi huyo alisema maneno hayo ili ahalalishe kitendo kiovu alichokifanya.

Mtumishi huyo wa umma aliendelea kusimulia “utata wa nongwa hiyo ulizidi kukua, masikini alichokiambulia rafiki yangu ni kuvuliwa cheo chake na kupelekwa kituo kingine cha kazi kama adhabu”. Ndugu yetu alidakia akasema inawezekana alitafuna pesa za umma ndiyo maana akaondolewa”. Mtumishi huyo alisema “rafiki yake anamfahamu vizuri ni mwaminifu mno, dini yake pia kaishika vizuri mno hawezi hakufanya hivyo abadani! Kuna mengi katika utumishi wa uuma”. Mtumishi huyo wa umma alisisitiza hivyo.

 

Jambo la msingi ni lipi kwa siku ya leo?

Mosi, unapofurahia haki yako katika utumishi wa umma hakikisha haukanyagi haki za wengine. Pili, katika utumishi wa umma ishi na watu unaowaongoza kwa usawa, usifanye upendeleo wa aina yoyote vilevile usitumie nia yako ovu kunyanyasa wengine. Tatu, cheo ulichonacho unaweza kuvuliwa kwa nia ovu za watu katu usikate tamaa endelea kuwatumikia wananchi kama alivyofanya rafikiye Mgasi.

 

Nongwa ya pili imebaki kibindoni, NITAKUSIMULIA SIKU NYINGINE. Kwa heri.

0762665595

theheroluke23@gmail.com

2023.

0/Post a Comment/Comments