WENGI LINAWASHINDA KUNG’AMUA

 


Adeladius Makwega-MWANZA

Kijana mmoja alikuwa akifanya biashara katika Mji wa Lushoto, mkoani Tanga Tanzania. Kwa utaratibu wa biashara za mji huo wafanyabiashara wana maduka mjini, vijijini na kwenye magulio yanayozunguka kama yalivyo maeneo mengine duniani.

Mizigo yao inapomalizika basi wao hufunga safari katika miji mbalimbali kufungasha bidhaa hizo na kusafirisha mizigo hiyo hadi Lushoto eneo lenye milima na mabonde.

Ufungashaji huo huwa Zanzibar, Dar es Salaam, Tanga, Kilimanjaro, Arusha, Mombasa na hata Ulaya na Asia.

Siku moja kijana mmoja bidhaa zake zilikuwa zinakaribia kuisha hivyo alikusanya fedha kutoka kwa watu aliyokuwa wamekopesha na kununua kwa mali kauli au taslimu. Zoezi hili lilipokamilika safari ya kwenda kuchukua mzigo wake iliwadia, huku maamuzi yalikuwa afunge safari hadi Tanga.

Kweli alifika Tanga na kununua na kufungasha mizigo yake vizuri akiwa katika kununua bidhaa hizo hapo kwa tajiri huyo alikutana na mwenye mali binti mmoja mrembo, alipomtazama alivutiwa na urembo wake kijana wa Kisambaa akatia neno la mapenzi. Usumaku wa mapenzi uliwateka wote na pingamizi la mapenzi hayo halikuwepo.

Urafiki huo wa kijana huyu aliona una tija sana kwake akivutiwa na binti huyu namna anavyofanya biashara nyingi. Sasa biashara ziliendelea na huku mapenzi yakiendelea, sasa kijana huyu alituma pesa kwa mabasi yanayofanya kazi Lushoto Tanga na dada huyu kuzipokea na kumfungashia mzigo na kutumwa na kumfika bila shida yoyote ile. Jambo hilo lilisaidia mno kupunguza gharama za kusafiri , kulala na chakula.

Jambo hilo likawasaidia biashara zao kushamiri huku binti huyu akiunganishwa na wafanyabaishara wengine wa Lushoto waliokuwa na urafiki na kijana huyu na wakawa wateja wa binti huyu.

Biashara ikaendelea na huku mahusiano hayo ya kimapenzi yalipamba moto, binti huyu wa Tanga sasa akawa anafika Lushoto kwa mpenzi wake katika makazi ya familia ya kijana huyu yaliyopo kando ya Deustch iliyokuwa shule ya Wajerumani.



Mahusiano hayo yalipamba moto zaidi Binti wa Tanga na safari za Lushoto zilikuwa kedekede, hata mama na ndugu wa kijana huyu walimfahamu huku marafiki wa kijana huyu walikuwa wanafanya biashara Lushoto waliaminiwa kukopeshwa bidhaa kwa mali kauli ambapo walikweda kuuza alafu walirudisha fedha hizo kwa udhamini wa ndugu yao mwenye mahusiano ya kimapenzi nab inti wa Tanga.

Wakati mahusiano hayo yanapamba moto yanayokwenda sambamba na biashara binti huyu mfanyabiashara aliamua kumueleza neno kijana huyu wa Kisambaa.

“Mpenzi wangu nashukuru sana kwa kunipenda, lakini sasa siku zinasonga mbele , mimi nakufahamu wewe , wazazi wako, ndugu zako na kwenu Lushoto lakini wewe haukufahamu kwetu hivyo nakuomba sasa umewadia wakati sahihi na wewe ukapafahamu nyumbani kwetu na kwa wazazi na ndugu zangu ili tuweze kufunga ndoa.”

Kijana huyu mfanyabiashara wa Lushoto alivutiwa mno na kauli hiyo,

“Hilo ni jambo sahihi kabisa kwani wapendanao ni kufahamiana na kujua nyumbani kwa mpenzi wako, maana kwenye mapenzi kuna uzima na mauti linapotokea shida kila mmoja anakufahamu kwa mwenzake na vibaya kuishi bila ndoa.”

Kweli walikubaliana na kijana huyu alimwambia mpenzi wake kuna atakuwepo Tanga juma linalofuata ambapo atafungasha na mzigo, akimaliza mzigo utatumwa Lushoto na yeye atakwenda huku kwa ndugu wa mpenzi wake.

Msomaji wangu sasa kijana huyu alikuwa na maduka kadhaa katika maeneo yote yaliyochangamka katika Wilaya hiyo huku maisha yake yakiwa bora kuliko awali.

Siku zilisonga na kijana huyu kufika Tanga na kufunga mzigo vizuri na kuituma kwa Malori yanayokwenda Lushoto Milimani.

Binti huyu akamwambia mpenzi wake,

“Leo nakuomba tulale katika nyumba ya wageni alafu kesho tutaondoka kuelekea nyumbani kwetu maana muda umeshasonga itakuwa si vizuri kufika nyumba kwetu wakati jua limezama.”

Mwanakwetu hilo lilifanyika hivyo hivyo wakala chakula na wakaenda kulala katika nyumba ya wageni.

Wapendanao sasa wapo katika nyumba ya wageni , watu wenye mahusiano ya mapenzi ya muda mrefu wamezoeana na kuaminiana kabla ya kulala binti huyu aliingia kwenda kuoga bafuni. Kijana huyu nayeye kama siku zote alitamani aoge pamoja na mpenzi wake huko bafuni huku joto la Tanga likiwashawishi waoge maji ya baridi.

Binti huyu aliingia bafuni naye kijana huyu akasogelea mlango wa kioo wa bafu hilo la kisasa,

“Siku ya leo nataka nioge mwenye, naomba nisubiri huko kitandani nimalize kuoga na wewe utakwenda kuoga baadaye.”

Kijana huyu alirudi kitandani baada ya kupewa ilani hiyo mpya, akajilaza kitandani, kwa kuwa alikuwa na uchovu wa safari na kazi kubwa ya kufungasha mizigo siku nzima, akiwa hapo kitandani usingizi ulimpitia akalala fofofo.

Akiwa amelala kwa saa kadhaa gafla mbele akashituka mbona nipo mwenyewe? Mwezangu yu wapi? Mbona nasikia maji kama mtu anaoga? Kweli tangu muda ule anaoga tu? Kijana huyu alimuita jina lake dada huyu hakuna aliyeitika, akaamka kitandani na kwenda bafuni kuchungulia kulikoni?

Mwanakwetu huyu alipofungua mlango alibaini kuwa yule binti alikuwa bado anaoga, lakini cha kustajabisha katika sinki la kupigia mswaki chooni aliona kuna vitu vimerundikwa , alipotazama vizuri aliona moyo , maini figo na matumbo ya binadamu, huku tumbo la binti huyu likiwa wazi , binti huyu akiendelea kulisafisha sehemu ya wazi ya tumboni tu .

“Eee mwezangu vipi? Bado unaoga tu, kulikoni tena mbona hivyo? Hayo mazingaombwe gani?”

Kijana huyu alistajabu anachokiona.

Binti huyu alimtazama kwa jicho kali alafu akamwambia ,

“Si nimekwambia leo naoga mwenyewe kitu gani kimekuleta huku bafuni?”

Kijana huyu alishituka mno na akarudi kitandani katika namna ya ajabu bila yeye kufahamu. Akapatwa na usingizi wa ajabu bila ya kutaka kama mtu aliyechomwa sindano na nusu kaputi. Gafla alijiona yupo katika ulimwengu mwingine kabisa chini ya bahari na yupo na huyu binti akimtambulisha kwa nduguze.Kijana huyu alishangazwa na mandhari hayo ya kuzungukwa na maji mengi, wakati yeye amezoea mandhari ya mabonde na milima ya Lushoto huku maji yakipita katika vijito tu.

“Huku ndiyo kwetu na hawa ni ndugu zangu na hawa ni wazazi wangu, kama nilivyokwambia tunakuja kwetu ndiyo hapa chini ya bahari, si unaona samaki wale wakubwa kwa wadogo hao ni jamaa zetu hawana madhara na sisi. Usinione kule dukani, huku ndipo ninapotoka. Sasa hapa hapa tunafunga ndoa.”

Kweli ndoa hiyo ilifungwa chini ya bahari, muda huo huo na huku kijana huyu akijiuliza mbona wazazi wangu kule Lushoto hawafahamu kama ninafunga ndoa? Lakini alijipa moyo kuwa wazazi na ndugu zake wanamfahamu binti huyu kwa muda mrefu?

Harusi hiyo ilipomalizika kijana huyu alishituka kutoka katika usingizi huo wa ajabu na kumekucha ni asubuhi wapo kando ya bahari yeye na huyu binti. Kijana huyu sasa anashangaa anamuuliza huyu binti mbona tupo hapa? Si tulikuwa tupo hotelini na wewe ulikuwa unaoga? Binti akamjibu huku tunatoka kwetu kama nilivyokueleza na tumeshafunga ndoa.

“Mbona inu n’deuzi ni ya mazingaombwe!”

Kijana huyu alijisemea moyoni kwa Kisambaa kwa kustajabu akimaanisha kuwa mbona ndoa hii ni ya mazingaombwe.

Kijana huyu akawa amekasirika kwa anachokiona siku hiyo, wakagombana hapo ufukweni, binti akimwambia kijana huyu warudi hotelini lakini kijana huyu akagoma akisema kuwa yeye anarudi Lushoto nyumbani kwao. Alifika sehemu yanaposimama malori ya mizigo ya Lushoto hapo alikutana na Lori linapakia mzigo, lilipomaliza alipanda mbele na wenzake kuelekea Dochi. Alipofika hapo alimfuata mama yake mzazi ambaye alikuwa mama mtu mzima sana, mama huyu aliamfuata Sharifu na kumueleza kilichotokea kama kilivyo kwa kijana wake, hiyo sasa ilikuwa usiku wa siku hiyo aliyotoka Tanga.

Sharifu alimwambia kuwa kesho yake asubuhi kukicha tu jambo lake la kwanza aende akanunue ubani Sokoni alafu afike nyumbani kwa Sharifu akiwa yeye na mama yake ili mambo wayamalizwe.Kweli kulipokucha mama huyu alitangulia kwa Sharifu huku kijana huyu alidamkia sokoni, akanunua ubani na kupanda vigari vidogo akafika eneo linalofahamika kama Mbura na Kushuka sasa ili aenze safari ya kwenda kwa Sharifu.

Aliposhuka hapo kulikuwa na mtu yupo upande wa pili wa barabara alimuona akasema ngoja nimsalimie, akavuka barabara akamsalimia akamuaga na wakati anavuka barabara ili aelekee kwa Sharifu, kijana huyu aligongwa na gari hapo hapo akafariki dunia.

Kumbuka mama yake yupo kwa Sharifu wanamgonja kumbe kijana wake amegongwa na gari na kufariki dunia. Mama huyu alijulishwa hilo huku ubani ulimwagika katika ajali hiyo na hata kilichotaka kufanywa hakikufanyika. Nyumba kukawa na msiba na kijana huyu akazikwa.

Kweli alizikwa huku mama yake akisimulia kilichotoikea ndunguze kama kilivyosimuliwa na mwanakwetu hapo juu.


Mwanakwetu anasema nini siku ya leo?

Unapotaka kuwa na kitu kuwa makini sana, zipige picha kwa umakini mkubwa nia zako je zinalingana na nia za upande wa pili? Je hakuna nia ovu kwa mwenzako? Je mwenzako huwa anatabia yakuwa na nia ovu katika mambo yake? Kwa kufanya hivyo kunaweza kukusaidia kutojiingiza katika matatizo kama ya huyu kijana.

Kibinadamu unaweza kuyaona manufaa ya leo tu katika mahusiano yoyote na mtu, kikundi, taasisi au upande mmoja na mwingine. Baadhi ya mambo yanaweza kukuaminisha kuwa upande fulani ni wema kumbe hilo ni chambo tu kama yalivyotumiwa mahusiano ya kimapenzi na biashara katika kisa hiki.

Mwanakwetu tuwe makini kwa maana jambo hilo wengi linawashinda kung’amua.

Nakutakia siku njema

makwadeladius @gmail.com

0717649257

 

 

 

0/Post a Comment/Comments