FENESI TUNDA LA MKARIMU

 



Adeladius Makwega-MWANZA

Ndugu huyu alikuwa akihamahama na familia yake kutoka eneo moja kwenda lingine, kumbukumbu za mwanakwetu zinanukuu uhamisho wa awali ulikuwa ni wa kutoka Tambi kwenda Berege alafu ukaja uhamisho wa kutoka Berege Kuelekea Sagara. Hayo yakiwa ni majina ya vijiji vilivyopo kwa sasa katika Wilaya za Mpwapwa na Kongwa mkoani Dodoma.

Maisha yake katika vijiji vya Tambi na Berege huko mwanakwetu alikuwa mtoto mdogo, hapo hakumbuki kitu lakini alipohamia Sagara sasa mwanakwetu alikuwa kidogo akijitambua. Mtoto anayejitambua si vizuri kushinda nyumbani na kuwinda vipepeo na ndege, iliamuliwa awe anakwenda shuleni kujifunza kusoma, kuandika na kuhesabu na wenzake.

“Hapo sasa walimu wake walikuwa wakimsaidia kuumba herufi na kurekebisha silabi na irabu zilizokuwa zinapiga tikitaka.Wakiandika angani , ardhini na baadaye katika vibao vyeusi.”

Shule ya Msingi Sagara ilikuwa na wanafunzi wengi kutoka maeneo ya vijiji kadhaa wengine wakitoka milimani huku wengine wakitoka mabondeni. Eneo hili lilikuwa na hali ya hewa ya tafauti na maeneo mengi ya Dodoma maana mvua zilikuwa zinanyesha huku vyanzo kadhaa vya maji yaliyosambazwa maenneo jirani, hilo liliambatana na kiimo cha nyanya vitunguu, kabichi na mboga mboga zingine.

Hiyo ilikuwa mwkaa 1981, mwanakwetu anakwenda shuleni kusoma lakini hajaandikishwa kuanza darasa la kwanza nia aweze kujua mbinu za shuleni. Wanafunzi wote wa Shule ya Msingi Sagara walifanya mitihani yao ya kufunga shule muhula wa kwanza, walimu wakaipa alama mitihani hiyo na siku ya kufunga shule ilifika. Utaratibu ulikuwa ikifika siku ya kufunga shule wanafunzi wote na walimu wanakutana pamoja katika Baraza la Shule na mara nyingi eneo lenye kivuli au kwenye mti mkubwa, walimu wakikaa katika meza na madawati machache mbele, huku wanafunzi wote wakikaa chini katika mchanga.

“Jukumu la kikao hicho lilikuwa kwanza kuyasomwa matokeo yote ya shule nzima kutoka darasa la kwanza hadi la saba, alafu ikiambatana na kutaja wanafunzi wa kwanza hadi wa tatu wa kila darasa wakipewa zawadi mbalimbali kama vile mikebe, madaftari kalamu za risasi na kalamu za wino wa kujovya, zawadi hizo na zingine nyingi zilitoka katika stoo ya shule ambazo zililetwa na serikali mashuleni nchi nzima jukumu la mwanafunzi/mtoto ilikuwa kusoma tu yeye na kichwa chake.”

Mkuu wa Shule alipomaliza kufanya zoezi hilo aliwapongeza waliofanya vizuri na kutaja tarehe ya kufungua shule.

Kwako msomaji wangu ngoja nikuume sikio kuwa siku hiyo ndugu yetu mwanakwetu alikuwa mwanafunzi wa 72 katika darasa lililokuwa na wanafunzi zaidi ya 100. Hii msomaji wangu ni siri kubwa kaa nayo moyoni, usimwambie mtu. Mwanakwetu shule hiyo ilifungwa, wakiwa katika likizo baba wa mwanakwetu alipata uhamisho aliouomba ili aweze kurudi kwao Pwani huku yeye na mkewe wakiwa watumishi wa umma. Kweli mizigo ilifungwa huku wakiuza mifugo kadhaa kama vile mbuzi, kondoo na ng’ombe waliokuwa wakifungwa katika vijiji vya Berege na Sagara .

Walisafiri kutoka Dodoma hadi Dar es Salaam, wakafika Mbagala nyumbani kwao na kukaa kidogo na baada ya siku kadhaa walianza safari ya huko Mkerezange Kisarawe Mkoa wa Pwani. Walipanda basi hadi Kimanzichana na hapo wakashuka na mizigo yao akiwepo baba, mama na wadogo wawili mwanakwetu.

Wakiwa Stendi ya Kimanzichana kugonja usafiri wa kwenda Mkerezange ambacho ni kijiji lilichopo kati ya Kimanzichana na Mkamba lilinunuliwa tunda mojawapo ambalo lilikuwa na vipele vipele. Baba wa mwanakwetu akachukua vipande kadhaa na kumgawia mwanakwetu na wengineo. Mwanakwetu alichukua punje ya njano ya tunda hilo na kuanza kula tunda moja.Baba wa mwanakwetu akasema ,

“Mwanangu hizo mbegu usizile, wewe kula nyama ya njana na mbegu ngumu unaitupa, hizo mbegu huwa zinaliwa kama zinachemshwa, ni tamu kama gimbi au kiazi mviringo , mbegu yake ni chakula kamili chenye wanga.”

Tunda hilo likamshinda mwanakwetu kula kabisa maana lilikuwa na sukari nyingi. Hapo akamrudisha baba yake . Kwani tunda hilo linaitwajwe? Alimuuliza mama yake. Mama yake akamwambia muulize baba yako hata mimi limenishinda kula.

“Hili tunda linaitwa fenesi linatokana na mti unaoitwa mfenesi linaliwa likiwa limeiva, unaweza hata kulila na uji na chai, yanastawi mno katika mikoa ya Pwani yenye joto na mvua kiasi japokuwa hata katika maeneo baadhi yenye baridi mfenesi unastawi. Mti mmoja unakuwa na matunda kati ya 100-200 ambapo tunda moja lina KG kati ya 20-30. Wanagu haya siyo matunda ya uchoyo, ukipanda mti wake utakula na wengi na ndiyo matunda ya Pwani. Kama zilivyo furu Dodoma. Kama limewashinda leo kulila mtalizoea tu haya ndiyo matunda ya kwenu.”

Baba huyu aliyeyasema maneno hayo kwa hakika  kwa sehemu kubwa ya utoto alikulia Mbagala na Kilindoni Mafia hivyo matunda kama fenesi, matope tope , mabungo, mastafeli madoliani yalikuwa si mageni kwake, shida ilikuwa kwa mama wa mwanakwetu mzaliwa wa Kilimatinde Manyoni Singida ambaye hapo alikuwa anaambatana na mumewe kuhamia Pwani.

“Mwanamke akiolewa, kwake ni ada kumfuata mumewe popote alipo labda kwa makabila mengi ya Lindi na Mtwara ambayo ukoo ni wa mama, je hiyo inatambulika Kiserikali kwa mwanaume kufuata mkewe?”

Kumbuka mwanakwetu hapo alikula fenesi kwa mara ya kwanza, baadaye alizoea mno akila zaidi na zaidi huku akibaini kuwa mti huu una asili ya India na mbao zake zinatumika kama kuni na hata kutengenezea samani mbalimbali za majumbani.

Maisha ya Mkerezange yaliendelea vizuri, hiki kilikuwa kijiji chenye matunda mengi kama machungwa, machenza, ndimu nyingi, minazi na mikorosho. Sagara na Mkerezange zilitafautiana kiasi. Sagara wakiwa na mifugo wakati Mkerezangu haikuwepo, Mkerezange walikuwa na matunda ya pwani lakini Sagara walikuwa na zambarau na matikiti mengi.

Wazazi wa mwanakwetu walikaa hapo kwa muda mchache na kuhamishiwa Kijiji cha Kimanzichana ambacho kwa hakika kilikuwa kijiji kilichochangamka mno kuliko kijiji chochote kutoka Mbagala maana wakati huo biashara mbalimbali zilifanyika saa 24.

 Je hali hiyo ipo mpaka leo?Hilo mwanakwetu anajiuliza na hajafika huko muda mrefu.

Hapo mwanaketu ilikuwa ni mwaka 1983 na aliandikishwa darasa la kwanza na kuanza kusoma rasmi maana mkono wake ulikuwa sasa umeshika sikio vizuri bila ya kujilazimisha.

Masomo ya darasa la kwanza yaliendelea vizuri huku mwanakwetu akimkumbuka rafiki yake Mohamedi Kindundusi (Kindundusi-Mfupi) na Tatu Ali, hapa sasa muhula wa kwanza ulikuwa unakaribia kumalizika, walifanya mitihani ya darasa hilo katika masomo matatu Kusoma, Kuandika na Kuhesabu. Mitihani ilipomalizika walimu walisahihisha na kujiandaa kuyasoma matokeo katika Mkutano wa Baraza la Shule.

Mwalimu Mkuu aliyefahamika kama Mwalimu Sitta ambaye alikuwa na mkewe mama mmoja mwalimu Mpare aliongoza mkutano huo wa kufunga huku wanafunzi wote kukusanyika na kukaa chini huku wengine wakiwa wamechuchumaa. Utaratibu ulikuwa ule ule wa kusoma matokeo ya mwanafunzi wa kwanza hadi mwisho . Ukianzia na darasa la kwanza ambalo ndilo darasa la mwanakwetu wakati huo.

“Mwanafunzi kwa kwanza kwa darasa la kwanza ni Tatu Ali  akipata 100 ya Kusoma, 100 ya Kuhesabu na 100 ya Kuandika, mwanafunzi wa pili ni Mohammed Kindundusi yeye amepata 100 katika Kuandika, 100 katika hesabu na 95 katika kusoma na jina la kumi ni mwanakwetu amepata Kusoma katika 0, 100 Kuandika na 100 katika kuhesabu.”

Hapo mwanakwetu alistajabu inakuwaje nimepata sifuri katika kusoma ambalo ndilo somo jepesi kuliko yote? Akasima na kuanza kulia mbele ya Mkutano wa Baraza la Shule

“Hapo haiwezekani, alama niliyopewa siyo yangu , mimi kusoma ninafahamu, inakuwaje niweke sufuri?”

 

Mkutano mzima wa Baraza la Shule kimya, Mkuu wa Shule Mwalimu Sitta akaelekeza mwalimu wa darasa la pili azungumze na mwanafunzi huyu mara moja. Hapo pia wakafika walimu watatu wa kike.

Somo la kusoma nilisoma vizuri maneno yote sikukosea hata neno moja, mwanakwetu alisema. Mwalimu aliyepewa jukumu hilo alimuliza je unakumbuka hata neno mojawapo ulilopewa kusoma? Mwanakwetu alijibu kuwa ni neno JOGOO.

Mwalimu wa darasa la kwanza aliombwa kuuleta mtihani huo wa kusoma mara moja hapo upenuni na kuingia ofisini huku Mkutano wa Baraza la Shule unaendelea.Hapo sasa walikuwapo mwalimu wa nidhamu, mwalimu taaluma, mwalimu wa darasa la pili na mwalimu wa darasa la kwanza. Mwanakwetu alisoma maneno yote vizuri bila ya kukosea hata neno moja

Matokeo mbele ya walimu hao alikuwa amepata alama 100 ya kusoma lakini tayari Mkutano wa Baraza la Shule ulikuwa umemalizika. Mwalimu Mkuu akafika walipo walimu hao akauliza ehee imekuwaje? Kweli mwanafunzi wetu ameyasoma vizuri nadhani mwalimu mwenzetu alipitiwa kuipachika alama 0 na kusahau kuiweka nambari moja na sufuri ili iwe 100.

“Mwalimu kuwa makini, jitahidi sana usiwe unapanda gari ya dhuruma, yenyewe uwa inapinduka sehemu ambayo hauitegemei. Mwanafunzi wetu nenda nyumbani matokeo tumeyasharekebisha.”

Alipotoka nje na hapo mwanakwetu alimkuta rafiki yake Mohamedi Kindundusi akimgoja na alipokuwa akirudi nyumbani alimsimulia kilichotokea upenuni na ofisini.



Mwanakwetu siku ya leo anasema nini?

Kumba kuliko yote ni kuyakumbuka mno maneno ya Mwalimu Mkuu Sitta,

“Mwalimu kuwa makini, jitahidi sana usiwe unapanda gari ya dhuruma yenyewe huwa inapinduka sehemu ambayo hauitegemei.”

Mwanakwetu kama unautamani usalama wako katika maisha ya ulimweguni na akhera ogopa sana kulipanda gari hilo la dhuruma. Kumbuka haki ni sawa na kulila fenesi mara zote huwa linapandwa na mtu mmoja lakini huliwa na wengi ukitaka kula mwenyewe lazima litakushinda tu maana fenesi ni tunda la wakarimu .

Mwanakwetu upo?

Nakutakia siku njema.

makwadeladius@gmail.com

0717649257

 

0/Post a Comment/Comments