KIJANA ALIYETUWAKILISHA VEMA

 



Adeladius Makwega –MWANZA

Mwanakwetu alilala katika iji la Arusha vizuri na kuamka asubuhi sana ya siku iliyofuta ambapo alitoka hapo nyumba ya wageni na kufika stendi, alipokaribia stendi ya Arusha Mjini ambayo ni stendi ya miaka mingi, haijaboreshwa alipokelewa na wapiga debe kadhaa, mpiga debe wa siku hii alikuwa baba mmoja mnene, mrefu na mtu mzima.

Mwanakwetu alipoulizwa unakwenda wapi? Alijibu kuwa anakwenda Musoma, mpiga debe huyu alisema kuwa mabasi yapo mengi yale yanayopitia Singida, Mwanakwetu alijibu kuwa yeye anapitia Serengeti,naye mpiga debe alijibu haya,

“Njia ya Serengeti inaruhusiwa basi moja tu kwa siku, ngoja tuangalie kama lipo kwa kuwa basi moja linatoka Musoma na lingine likitokea Arusha, yanakutana katikati.”

Walitoka hapo hadi linaposimama basi hilo, palikuwa wazi, hivyo Mwanakwetu alimuuliza mpiga debe huyu sasa ninafanyaje? Alijibiwa kuwa,

“Unaweza kupanda kwa kupitia Singida, njia ya Arusha Serengeti Musoma ni fupi inakaribia KM 400 tu lakini kupitia Singida ni KM 1100.Hapo basi linatumia mafuta mengi na hata nauli inakuwa kubwa sana, maana kama KM 400 na barabara ni nzuri nauli ingekuwa kidogo, na piamafuta yangetumika kidogo. Kumbuka wanyama wangekufa sana. Kama inatengezwa basi wangeweka sheria kali, na taa nyingi bungani.”

Mwanakwetu alielekea na mpiga debe huyu upande zilipo basi za Arusha Singida Musoma/Mwanza na alilipa shlingi 40,000/= na kupanda basi ya Arusha-Mwanza. Basi hilo lilikuwa na jina Loliondo. Mwanakwetu akapewa kiti namba 46 kikiwa cha mwisho mwisho.


Akiwa humo ndani ya basi amekaa alikuwa kando na kaka mmoja jirani yake, jirani huyu wa Mwanakwetu alisema haya,

“Nimekuona unatafuta mabasi ya Musoma kupitia Serengeti, pole sana kwa kulikosa, njia hii ingewekwa lami ingetuingizia pesa nyingi sana, lakini ndiyo hivyo tena, tuombe Mungu tu.”

Wakiwa wanazungumza Mwanakwetu na jirani yake katika kiti chao, pembeni yao kwa mkono wa kushoto alikuwa amekaa dada mmoja na mara akaingia dada mmoja mzungu. Dada huyu mzungu alimwomba dada mweusi ampishe katika kiti chake cha dirishani. Dada mweusi alijibu kuwa kiti chake ndiyo cha dirishani. Hapo yakawa mabishano kwa lugha ya Kiingereza, Mwanakwetu alipomtazama binti mweusi alikuwa kama ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu huku akizijenga sentensi zake za kiingereza vizuri sana.

Binti mzungu akasema ngoja nikae kiti cha nyuma akija kondakta ataamua ugomvi huu, dada Wakitazania akasema ndiyo. Kumbuka Mwanakwetu na jirani wanafuatilia ugomvi huo kwa kina, Msomaji wangu kumbuka unapokuwa na mgeni kando kutoka taifa lingine wewe unakuwa balozi wa taifa lako.

Mwanakwetu akamwambia abiria mwenzake kwa sauti ya chini,

“Huu mjadala wa kiti dirishani atashinda mzungu, nakwambia , hawa jamaa wako makini mno kwa mambo yao, kama anakidai kitu tambua ni haki yake. Sisi unaweza ukamwambia kondakta nikatie kiti cha dirishani, wala uhakikishi, ngoja tuone mchezo utaishaje?”

Kweli baada ya dakika tano alifika kondakta na kuangalia tiketi zao na kumwambia dada mzungu akae dirishani, naye dada yetu wa Kitanzania akakaa kiti cha pembeni mkabala na Mwanakwetu.

Abiria waliendelea kuingia ndani ya basi hilo, alifikia kijana mmoja ana begi lake, akajaribu kulingiza katika sehemu ya kuweka mizigo ndani ya basi hilo juu kwa nguvu, kondakta akafika na kuyatoa maneno haya,

“Wewe hauoni basi ni mpya, unataka kuvunja taa bure.Taa hizo ni nzima kwa kuwa zimetunzwa”

Kijana aliyeambiwa hivyo aliuliza sasa aweke wapi mzigo wake? Kondakta aliseme kauweke chini buti, kijana akapinga hilo akisema kuwa begi lake halikai huko, mjadala ukawa mkubwa, kijana akaomba arejeshewe pesa yake. Hapo kondakta alikuwa mzito kwa dakika tatu hadi nne, baadaye walimuwekea mzigo vizuri na kijana akakaa katika kiti chake. Hapo huyu kondakta mkorofi akashuka hakuonekana tena ndani ya basi. Kumbe basi hilo lilikuwa na kondakta binti mmoja mwelevu, makini , mpole na anaipenda kazi yake.

Msomaji wangu kumbuka dada mzungu na dada mswahili wapo kiti kimoja je wataongea safarini? Mwanakwetu safari ilianza wapo kimya safari nzima kimya kikuu kila mmoja akichezea simu yake, jirani wa Mwanakwetu akasema,

“Dada huyu wa kizungu ningekaa naye mimi, ningempa simulizi zote za Tanzania, kaja hapa kutalii ili aifahamu Tanzania lakini kama akishuka Mwanza nitazungumza nae .”

Basi hili lilikata mbuga na kuvuka mikoa kadhaa na hata lilipofika Singida dada jirani na mzungu alishuka, kwa hiyo kiti kile kikawa kitupu, hivyo jirani wa Mwanakwetu aliamua kuhamia kwa dada mzungu.

Mwanakwetu kwa simu alizokuwa anaongea dada huyu wa kizungu alibaini kuwa alikuwa Muitaliano maana maneno kama Monasela, Tuti, Caza na  Bambino yalisikika mno katika sentensi zake alizoongea kwenye simu.

Mwanakwetu akatulia tuli huku akiyafuatilia mazungumzo ya jirani yake na dada mzungu, kwa kuwatazama huyu jirani wa Mwanakwetu na dada mzungu walikuwa ni mzao mmoja, hapo mambo yalikuwa safi kabisa.

Mwanakwetu alitazama tabasamu la dada wa kizungu lilikuwa kubwa, sasa akicheka pale huyu jirani wa Mwanakwetu akitupa maneno ambayo Mwanakwetu hakuyasikia. Baadaye Mwanakwetu alianza kusikia mazungumzo yao na huyu dada akisema anatokea Milano-Italia amekuja Tanzania kutalii na anakwenda Mwanza.

Jirani wa Mwanakwetu alimuliza dada mzungu mbona umegombana na jirani yako Je mnafahamiana ? Dada mzungu alicheka akisema hamfahamu dada huyo aliyeshuka Siongida. Jirani wa Mwanakwetu akimwambia dada huyu mzungu kuwa hapa Tanzania ukiwaona wanawake wanagombana fahamu kuwa wanamgombania mwanaume, Je umemchukuliwa mumewe ? Dada mzungu alicheka sana alafu akasema maneno haya,

“Tanzania sijakuja na mume niko mwenyewe.”

Maneno yalikuwa matamu huku jirani ya Mwanakwetu aliomba nafasi hiyo apewe yeye, dada mzungu alicheka sana akisema kuwa yeye hawezi ugomvi kugombana ugenini, maana, jirani wa Mwanakwetu alionekana kama ana mke.



Jirani wa Mwanakwetu alisema hana mke, hivyo hapo msomaji wangu darasa la mapenzi lilipamba moto kweli kweli. Kwa bahati mbaya Mwanakwetu alipitiwa na usingizi mzito akalala kwa saa kadhaa, baada ya muda kondokta wa basi hilo binti alifika kumuamsha Mwanakwetu kwa kuwa alikuwa amefika Hungumalwa.Mwanakwetu wakati anajiandaa kushuka aliona sasa mazunguzo  ya dada mzungu na jirani yake yalikuwa ya ujirani zaidi, Mwanakwetu akawaaga na kushuka zake.

Mwanakwetu aliposhuka katika basi hilo akilini mwake alifurahia mno namna kijana huyu wa KItanzania alivyotuwakilisha vema kwa binti mtalii wa Kiitaliano kutoka Milano. Kijana huyu aliweza kuyafuta yote mabaya kwetu kutoka wa abiria yule binti mwanzoni mwa safari.

Mwanakwetu upo? Nakutakia siku njema.

makwadeladius@gmail.com

0717649257



0/Post a Comment/Comments