KIONGOZI WA MICHEZO TULIYEMPOTEZA NJIANI

 



Adeladius Makwega-MWANZA

Aprili 27, 2023 Mwanakwetu alifanya mazungumzo na Philemoni Kelvin Felix ambaye ni miongoni mwa Watanzania waliosoma Shule ya Sekondari ya Tambaza hapo zamani na miongoni mwa kaka zake. Felix pia alisoma Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kushiriki karika kulicheza kabumbu la Tanzania, uchezaji wake huo wa soka akikutana na watu wengi maarufu katika soka na siasa za Tanzania.

Katika mazungumzo hayo kwa njia ya simu yaliyotumia dakika 16 na sekunde 43 mengi yalizungumzwa likiwa hili,

“Katika kile kipindi chetu sisi, huyu Charles Kitwanga ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, huyu huyu, yeye alikuwa anacheza mpira wa kikapu na yeye ndiye alikuwa Waziri wa Michezo katika Serikali ya Wanafunzi pale Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.”

Hawa vijana wa UDSM wakati huo walimchagua Charles Kitwanga kuwa Waziri wao wa Michezo kwa hoja mojawapo, alikuwa anacheza mpira wa kikapu, yeye alikuwa miongoni mwa wanamichezo hapo chuoni.

Mwanakwetu kwa sasa hajaonana na Mzee Kitwanga kwa muda, kama akikutana naye atamuuliza vipi bado anacheza mpira wa kikapu? Kwa wale ambao hamfahamu Charles Kitwanga kwa namna alivyo mrefu, kwa hakika alikuwa mchezaji mzuri wa mchezo huo , japokuwa wapenzi wa mpira wa kikapu walikuwa wachache pale UDSM, Mpira wa Kijapu ukitazamwa kuwa mchezo wa mabishoo siyo mchezo wa magangwe kama soka na ngumi.

Japokuwa tangu Kitwanga na wenzake waliyohitimu UDSM sasa ni miaka mingi lakini vijana wote wa wakati huo hapo UDSM wanamkumbuka Kitwanga kama kiongozi wao hodari wa michezo hadi leo. Huku wakikumbuka hata shule alizosoma kabla ya UDSM,

“Charles Kitwanga alikuja UDSM, awali alisoma sekondari za Same- Kilimanjaro na baadaye hapo Tosamaganga Iringa.”

Kwa mtu ambaye hakusoma naye kiongozi huyu hapo UDSM kama ilivyo kwa Mwanakwetu anamtambua ndugu huyu kwa nafasi zake alizokuwa nazo za Mkurugenzi Msaidizi pale Benki Kuu na Uwaziri wake wa Mambo ya Ndani ulivyokuwa. Ndiyo kusema yule aliyekuwa naye UDSM anamfahamu katika sura nyingi zaidi kama ilivyo kwa ndugu Felix,



Kwa mtu anayelifahamu jambo katika sura mbili ni mtu mzuri zaidi kulielezea tafauti na yule anayeliona kwa sura moja, jambo linapotazwa katika sura mbili hapo unapata picha kamili ilivyo. Inawezekana ukayafahamu mazuri mengi, huku pia ukipata picha ya kuyafahamu mabaya zaidi. Kubwa na la msingi ni kulifahamu jambo kwa kina, siyo kwa kubabiababia. Ndugu Philimone Kelivin Felix anawakumbuka wanamichezo kadhaa wa wakati huo hapo UDSM huku akiwataja mmoja baada ya mwingine.

“Pale Chuoni tulikuwa na mtu anaitwa Charles Gasper, huyu pia alikuwa anachezea Yanga, yeye ndiye alikuwa beki nambari tano wa Chuo Kikuu lakini pia akichezea timu ya Yanga ya Dar es Salaam, hapo alikuwapo pia Lawrence Mwalusako ambaye alikuwa nyuma yetu, kwa mwaka mmoja, wao walitakiwa kumaliza mwaka 1989, walipata shida ya kumtukana Rais Ali Hassan Mwinyi wakapewa adhabu ya kuhitimu mwaka 1990. Katika kundi letu walikuwepo Mtemi Ramadhani, na Leodger Tenga, huyu Tenga yeye alisoma Shahada ya Uhandisi lakini alikuja pale kusoma Shahada ya Uzamili ya Uongozi wa Biashara(MBA), kwa maana alikuwa Mkurugenzi wa Land Rover Tanzania. Pia kulikuwa na jamaa mmoja aliyeitwa Shah Hanzuruni (marehemu sasa), wakati huo alikuwa anachezea Waziri Mkuu ya Dodoma, alikuwa ni mchezaji mzuri sana, alikuwa mchezaji muhimu na hata katika timu ya taifa alikuwa anaitwa kuichezea Taifa Stars. Hata huyu Mtemi Ramadhan na yeye alitokea Dodoma kabla ya kwenda Simba, hao walikuwa wachezaji muhimu sana, wachezaji wengine ni Jaji Francis Mutungi yeye alikuwa kipa wetu, huyu Msajiri wa Vyama vya Siasa. Jaji Mutungi alikuwa kipa tangu Tambaza na tulisoma naye. Kipa mwingine alikuwepo kijana mmoja aliyesoma Forodhani Sekondari Endrew Maro (kaka wa Anna Mkapa), wachezaji wengine waliokuwa wanaingiaingia ni Erick Shitindi aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Kazi, amestaafu akiwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Njombe.”

Msomaji wangu maelezo haya juu yanatoa picha ya vijana hao wa Tambaza na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam namna walivyokuwa wanashiriki michezo na namna walivyokuwa jirani tangu wakiwa wanasoma. Kwa kutazama kwa kina majina hayo yote yameshika nafasi mbalimbali za Kitaifa lakini aliyeongoza katika michezo ni Leodger Tenga Pekee.



Mwanakwetu siku ya leo anasema nini ?

Katika utafiti wake amebaini kuwa japokuwa Charles Kitwanga alikwa waziri katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lakini hakuwai kuwa waziri wa michezo katika serikali yetu. Hilo Mwanakwetu anaona kuwa hakuna aliyeona kuwa ndugu Kitwanga anaweza kuifanya kazi hiyo vizuri.

Mwanakwetu anayasonta makosa yetu katika hilo akiamini kuwa tulikosea mno, maana Kitwanga alikuwa na uwezo wa kuifanya vizuri kazi hiyo ya Uwaziri wa Michezo kuliko mtu yoyote kwa hoja nyingi sana, leo msomaji wake anakutajia moja ambayo ni kuwa na mahusiano makubwa na wanamichezo wengi wa wakati huo ambao aliwaongoza pale UDSM katika michezo akiwamo Leodger Tenga ambaye aliongoza vizuri TFF na BMT.

 Charles Kitwanga kama angekuwa Waziri wa Michezo hawa wenzake waliosoma nao wangezungumza lugha moja na pengine michezo yetu ingesonga maradufu. Hesabu za Mwanakwetu zinakwenda hata kwa Jaji Francis Mutungi hata yeye kama angekuwa kiongozi wa michezo pengine soka letu lingeenda mbali zaidi maana alishawahi kukaa golini pia anaifahamu mno michezo yetu kuliko hata alipo katika Vyama vya Siasa.

Mwanakwetu anaiweka chini kalamu yake siku ya leo akisema kuwa Charles Kitwanga ni kiongozi wa michezo ambaye tumempoteza njiani.

makwadeladius@gmail.com

0717649257



0/Post a Comment/Comments