NYAMA ZA MHESHIMIWA MBUNGE

 

Adeladius Makwega-MWANZA

Mwanakwetu juma lilipopita alisafiri kutoka Lushoto Mjini kuelekea Arusha, kwa kuwa ilikuwa siku ya Jumapili aliona ni vema asali misa ya Jumapili kabla ya kuianza safari ndefu kwenda huko aendapo. Misa ilipomalizika alikuwa chakula cha mchana ndipo alianza safari hiyo muda wa mchana na kufika Mombo majira ya jioni. Hapo Mombo alishuka na kupata gari ndogo ya vijana ambao walikuwa wakielekea Arusha Mjini.

Vijana hawa walikuwa wanakwenda Arusha lakini walikuwa hawakufahamu, kwa hiyo walihitaji mtu ambaye anaifahamu njia hiyo, kwa hiyo Mwanakwetu alikuwa ni mtu sahihi sana. Vijana hawa walisema kuwa Mwanakwetu atoe shilingi 10000/=, kweli alifanya hivyo. Kwa bahati nzuri walipatikana watu watatu wanaoifahamu Arusha mmoja alipanda gari la mbele na wawili akiwamo Mwanakwetu walipanda gari dogo la nyuma na safari ikapamba moto. Wakiwa ndani ya gari hiyo, viti vya mbele alikuwapo dereva na binti mmoja, kwa kuwatazama walikuwa ni wapenzi. Msomaji wangu niseme nisime? Hapo lazima unipe mji nikusimulie , maana mwanzako nililipa shilingi 10000/ kuyaona haya .

Natambua msomaji wangu umenichagulia Mbagala-Temeke au Ulanga Morogoro, huko nakupenda sana, ngoja nikusimulie uhondo.

“Watu wenye ndoa wakiwa pamoja ndani ya gari, mara nyingi kila mmoja anakuwa na luake,wananuniana mno, hawawezi kuongea wala kucheka , wala kusomeana ujumbe, lakini wapenzi, wasio na ndoa au mtu kamuiba mke wa mtu mwingine, Mwanakwetu wataongea mengi, mikumbatano na mabusi teletele juu yake hao.”

Msomaji wa Mwanakwetu unahitaji mtama umwage katika kuku wengi ujue kilichokuwa kinaendelea safarini? Natambua umeshaelewa. Mwanakwetu sasa ni mzee hawa walikuwa ni rika za watoto wake wa kuwazaa kabisa yeye yake macho ukawakaripia unarudishiwa nauli yako.

Kumbuka kuwa kiti cha nyuma alikuwapo Mwanakwetu, abiria mwenzake na kijana mwingne ambaye alifanana sura za dereva. Safari iliendelea vizuri, walipofika Hedaru hawa vijana wenye gari walisimama magari yote mawili wakashusha mzigo wakawapa wahusika, hapo walikaa kama dakika tano hivi. Mwanakwetu na abiria mwenzake eneo hilo walishuka chini kukanyaga ardhi ya Wapare wa Hedaru.Huku huyu abiria mwezake Mwanakwetu akasema,

“Kaka naona hedaru inabalidilika sana na inaendelea kwa kasi mno, maana sasa hata nyumba za maghorofa zinajengwa.”

Dereva na wenzake walirudi, wakaingia garini kuendelea na safari yao Arusha, sasa walikuwa wakiitafuta Same Mjini. Hapo kando abiria mwenzake Mwanakwetu akasema,

“Kaka unaiona Same? Sasa inatanuka mno, mji unazidi kuwa mkubwa, nyumba mbalimbali za ibada zinajengwa za kila kona, shule na vyuo pia zinainuka kama uyoga.”

Sasa gari hizo dogo ndiyo zinaingia Same Mjini, madereva waliingia kituo cha mafuta ili waweke mafuta. Hapo Mwanakwetu na huyu abiria wakashuka kuchimba dawa na kununua Korosho ,alafu wakawa kando ya gari hilo.

Mwanakwetu akamwambia huyu abiria mwenzake,

 “Mimi nimesoma hapa mwaka 1994/95, palikuwa duni sana, pakame, mno, ukitafuta hata ndizi, chungwa au embe ilikuwa tabu kupata , kulipatika miwa migumu tu. Shuleni kwetu pale Same Sekondari alikuwepo Mwalimu aliyefahamika kama Miss Yona ailifundisha somo ya Kiingereza na pia alikuwa mwalimu wa darasa. Huyu alikuwa bibi mmoja wa Kipare, alinipenda sana mwalimu wangu huyu. Mara nyingi kila wiki siku ya ijumaa tulikuwa na vipindi vichache ananitumamjini kumchukulia nyama katika mabucha ya Chediel Mgonja-ambaye alikuwa Waziri wa Elimu ya Taifa na Mbunge wa zamani wa Jimbo la Same.Huku nikipata nafasi ya kula nyama hiyo baada ya Miss Yona kuipika.Miss Yona alikuwa mwalimu mmoja msafi sana huku akiwa na ania kadhaa za viatu, vile vya kutembelea nje ya nyumba na vile vya kuvaaa ndani ya nyumba. Kwa kuwa nilikuwa naingia ndani ya nyumba yake alinipa hata viatu vya kuvaa ndani ya nyumba yake akinituma kwa mheshimiwa Chediel Mgonja.Baadaye nilibaini kuwa Miss Yona binti yake aliyekuwa anasoma sekondari mkoa mwingine alikuwa na ubini wa Chediel Mgonja.Kwa hakika kila siku ya Ijumaa maharage meupe kwa Mwanakwetu yalikuwa likizo maana Miss Yona alinpa bakuri la nyama.”

Gari likaendelea na safari, huku kijana huyu akimuuliza Mwanakwetu juu ya Miss Yona, mwalimu wake wa darasa yupo wapi? Mwanakwetu aliibu kuwa ni miaka mingi sasa, hafahamu mama huyu yu wapi lakini anakumbuka tu mheshimiwa Chediel Mgonja alifariki dunia.



Abiria mwenzake Mwanakwetu akasema kweli sasa Same hata kijani kibichi kinaonekana, safari inaendelea sasa wakawa wanakaribia Mwanga. Kijana huyu akaongeza kuwa Mji wa Mwanga hauendelei unabaki vile vile naona kuna dalili ya Same kuizidi Mwanga. Naye Dereva wa gari hilo akasema naona Mwanga barabarani hawana miti mingi, labda kule nyuma, huyu kijana abiria mwingine akasema hapa panaitwa Kisangara na wao wana maendeleo kidogo na huu ni mji wa matajiri wa Mwanga.Safari inaendelea huku dereva huyu akawa na nidhamu kidogo kwa kutambua kuwa kumbe ndani ya gari wamepanda wazee.

Mwanakwetu akasema,

“Mimi naifahamu Mwanga na Same ya vipindi tafauti, maana miaka 1980 nilikuwa napita na mama yangu kuelekea Kilimanjaro Babu yangu mzaa mama alikuwa akifanya kazi, ukipita na treni pale Same usiku unakutana na taa chache cha eneo hilo hasa stesheni , Shule ya Sekondari Same na Gereza la Same wakati ukipita Mwanga zilikuwa nyingi .”

KIjana huyu abiria mwenzake aliungama kwa Mwanakwetu kuwa yeye ni Mpare wa Mwanga, hapo ni nyumbani kwao.

“Ninafanya biashara Moshi Mjini, shida ya Mwanga ndugu zangu hawa wanataka kufanya biashara wenyewe, hatutaki kuwakaribisha wageni, hilo ndilo changamoto. Kama unataka eneo liendelee tunatakiwa kuchangamana na wengine mathalani kama mnachagua hata viongozi wa vijiji au nyumba za ibada wachanganike mgeni-mwenyeji, mwenyeji -mgeni.”

Kumbuka msomaji wangu safari inaendelea Mwanakwetu akatamani kufahamu kati ya Mwanga na Same Halimashauri zao zina hali gani ya kimapato?Aliiingia hapo,

https://ngaradc.go.tz/storage/app/media/uploaded-files/TAARIFA%20YA%20UKUSANYAJI%20MAPATO%20YA%20NDANI%20KWA%20HALMASHAURI%20184%20KWA%20KIPINDI%20CHA%20JULAI%202021%20HADI%20JUNI%2030%202022.pdf

Kubaini kuwa,

“Kwa mwaka wa fedha 2021/2022 Halimashauri ya Mwanga ilikusanya asilimia 97 ya makusanyo yake yote ikiwa ni shilingi 3,074421,566.97 (Bilioni 3.07) wakati malengo yalikuwa shilingi 3,166,000,000 (Bilioni 3.17) na Same walikusanya asilimia pia 97 ambapo mapato yao ya mwaka ni shilingi 2,508,407,143 (Bilioni 2.51) wakati malengo yalikuwa ni shilingi 2,589,000,000 (bilioni 2.51).”

Hapo akilini mwake alikumbuka kuwa kuna wakati Halimashauri ya Same iliongozwa na mwanasheria Anne Clear Shija(dada wa Mwanakwetu) na mkuu wa Wilaya  alikuwa Mhe.Rosemary Senyamule ambaye ndiye Mkuu wa Mkoa wa Dodoma leo hii.




Mwanakwetu hapo alisema nini?

Mwanga iliizidi Same kwa tofauti ya milioni 500 kwa mwaka huo wa fedha huku malengo ya Mwanga yakiwa zaidi ya Same, huku uchumi wa Mwanga ukiwa juu ya hiyo nusu bilioni.Huku Mwanga wakiwa na kiwanda cha Spirit na Same wakiwa na Mkonge na mbuga ya Mkomazi. Walipofika Moshi Mjini abiria huyu alishuka na kwenda zake naye Mwanakwetu na hawa wenye gari waliendelea na safari kuitafuta Arusha Mjini.

Mwanakwetu aliona wazi kuwa Anna Clear Shija na Mhe. Rosemary Senyamule walifanya kazi kubwa kuisuka Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro wakati huo na kuna kila dalili Same itaivuka Mwanga ndani ya kipindi cha miaka mitano kuanzia sana hilo Mwanakwetu analitabiri wazi wazi.

Mwanakwetu alifika Arusha Mjini na kuuchapa usingizi kungoja kuche aendelee na safari yake huko aendapo akiitafakari mno wilaya ya Same na Mwanga, mawazo yake pia yalimkumbuka Miss Yona mwalimu wake wa darasa na somo Kiingereza huku Nyama ya Mheshimiwa Mbunge na waziri zamani ikimjia akilini mwake wakati ule akiwa mwanafunzi pale Same sekondari.

Mwanakwetu wakati anaandika matini haya alitambua fika wapare wa Mwanga watasema tu Mwanakwetu anaisifia Same kisa kala nyama za Chediel Mgonja, hiyo ni kweli lakini amekula nyama kupitia kwa mwalimu wake  Miss Yona,isitoshe Mwanakwetu kasoma Same pia hakuna ubishi Same inakua kwa kasi mno.

Mwanakwetu upo?

makwadeladius@gmail.com

0717649257



0/Post a Comment/Comments