NUSURA KUTOKA SHIDANI

 



Adeladius Makwega-MWANZA

Mei 25, 2023 Mwanakwetu alipigiwa simu ya rafiki yake mmoja anayeitwa Ustadh Kuandika kutoka Lushoto, Mwanakwetu alipoona simu ya Shekhe Kuandika aliamini kuwa msomi huyu wa dini ya Kiisilamu alikuwa akiuliza kutaka kununua nyumba moja ya Mwanakwetu ambayo ipo jirani na msikiti wao, ambapo mara nyingi mawasiliano na shekhe huyu huwa ni ushawishi wake kwa Mwanakwetu kuuza nyumba hiyo.

Mara zote Mwanakwetu anamwambia Shekhe Kuandika kuwa nyumba hiyo si yake, bali ni mali ya watoto wake, kama Shekhe Kuandika anaweza kuwashawishi vijana wa Mwanakwetu wamuuzie, hilo litakuwa kazi kwake.

Shekhe Kuandika mara zote anacheka sana akisema,

“Tunahitaji nyumba ile, ili wageni wa msikiti wetu wakifikie pale wawe jirani na nyumba yetu ya ibada, siyo kukaa mbali mno, maana tunapata wageni kutoka mbali mno hadi Arabuni, yaani wageni wa Arabuni tunawaweka nyumba za wageni zinazokaliwa na kila mtu? Kwa heshima ya msikiti wetu na dini yetu lazima tuwe na makazi jirani.”

Shekhe Kuandika aliyempigia simu Mwanakwetu leo hii, awali akisema mengi,

“Umetupa mtihani mzito, hivi Shekhe Makwega jukumu la kuwakusanya watoto wako wote, alafu tuongee nao, hilo jukumu zito. Tunaweza kuzungumza na wawili, kumbe wako wanne, siku wakiibuka hao wengine? Hapo itakuwa kesi, alafu tuonekane siye tumedhulumu? Sisi tunaendelea kuombea dua jambo hili.”

Kwa hiyo haya mara zote simu hiyo ikipigwa hoja ya shekhe ni manunuzi ya nyumba hiyo tu lakini simu ya Mei 25, 2023 ilikuja kivingine, huku ikiwa simu ya kwanza ya Ustadh Kuandika kwa Mwanakwetu.

Msomaji wa Mwanakwetu ni vizuri kuelewa kuwa urafiki wa Mwanakwetu na Ustadhi Kuandika unatoka mbali kidogo , Shekhe huyu alidhulumiwa eneo lake biashara na mtu mmoja , kwa hiyo Mwanakwetu alipelekewa hoja hiyo na suala Ustadhi huyu likakamilika.

Mwanakwetu alikuwa pia anampenda sana Ustadhi Kuandika kwa hoja nyingine kwa kuwa Wilaya ya Ulanga kuna kina Kuandika Wapogoro iweje Ustadhi Kuandika awe Msambaa? Utani wa Mwanakwetu kwa Ustadhi Kuandika ulikuwa ni kwamba pengine Mpogoro wa Mahenge alifika Lushoto na kuoa wamama wa Kisambaa ndipo Shekhe Kuandika akazaliwa.Hilo likikataliwa kabisa na shekhe huyu.

Shekhe huyu ni mfanyabiashra mkubwa wa bidhaa za dini ya Kiisilamu kama vile marashi, vitabu vya juzuu, Udi, Korani, tasbii, kanzu , kofia nakadhalika, kuna wakati Mwanakwetu aliwapeleka sunna watoto wake, alipita kwa Ustadhi Kuandika kuwanunulia kanzu za kuvaa kipindi hicho, huku Shekhe Kuandika akisema,

“Wanao wawe wanavaa kanzu kila siku, siyo siku ya sunna tu.”

 

Kumbuka msomaji wangu hayo yote ni maelezo ya awali juu ya Ustadhi Kuandika na ujirani wake na Mwanakwetu, mara zote ukimwona shekhe huyu huwa amevalia kilemba kikubwa, kanzu maridadi na joho moja kubwa sana lenye nakshi nyingi.



 Je Mei 25, 2023 Mwanakwetu alipokea simu hiyo ya Ustadhi Kuandika ikiwa na maneno gani?

“Wewe ndugu yangu tunafahamiana miaka mingi, leo nina shida moja inanisumbua, kuna kijana wangu mmoja, katika maisha yangu ya umasikini nimewasomesha vijana wangu wengi elimu ya dini na elimu ya dunia vizuri sana, kijana wangu mmoja niliyemsomesha alipata kazi ya ualimu katika Halmashauri moja huko Handeni Tanga. Sasa ni mwaka wa nane unakwenda hali yake ya maisha si ngumu mno. Hivyo nimechunguza nimebaini kuwa Handeni huko ametekwa na mambo ya kidunia. Nimefika huko na nimeongea na majirani zake akiwamo mkuu wake wa shule. Nilibaini kuwa  anahitaji kuwa karibu na familia yake ili awe na maendeleo yake na familia . Nimebaini kuwa Handeni siyo eneo sahihi kwake maana anahitaji kuwa jirani nami kwa uangalizi zaidi, maana kwa Handeni ametwekwa na maisha ya kidunia huku mama mmoja wa Mzigua Handeni na mama mmoja Mchaga wa Marangu wamemteka. Shida yangu kukupigia unipe ushauri nataka kumkomboa mwanangu hivi nafanyaje ahamishiwe Lushoto? Na je nikiwafuta wakubwa wake watanielewa?”

Mwanakwetu alipomsikiliza nduguye huyu akamwambia pole kwa hayo yote, akisema kwa kuwa  dini yako ya Uisilamu inaruhusu kijana wako kuwa na mke zaidi ya mmoja kwanini usimuozeshe hao mabinti awe na wake watatu akiwamo yule Msambaa wa Lushoto, huyu Mchaga na huyu wa Mzigua wa Handeni.

“Ni kweli dini yangu inaruhusu hilo, lakini nimebainia kuwa kijana wangu bado hana maendeleo binafsi ndani ya miaka hiyo nane ya utumishi wake na ndiyo maana nataka awe chini ya himaya yangu kwa uangalizi zaidi.”

Mwanakwetu akamwambia hilo suala la kijana wake kurudi Lushoto linaweza kuwa ngumu maana kijana wake ni mtu mzima anaweza akagoma kurudi nyumbani hata kama akimuona mwajiri wake, inawezekana kijana wake akawa na shida lakini je shida hiyo anayoiona kwa kijana wake kama mzazi je mtoto mwenyewe anaiona kama ni shida?

Mwanakwetu akasema unapotaka kumkomboa mtu ambaye unadhani yupo katika shida kuna ulazima wa huyo aliye katika shida anawajibu wa kutambulishwa kuwa yu shidani ili atoe ushirikiano wa kumnusuru kutoka shidani.

Mwanakwetu simu hiyo ilikatika na baadaye Ustadhi Kuandika walikubaliana jambo ambalo kubwa lilikuwa  nusura kutoka shidani kwa kijana wa ustadhi huyu. 

makwadeladius@gmail.com

0717649257

0/Post a Comment/Comments