NYERERE AKIWA TABORA ALIPEWA MKE

 



Adeladius Makwega-MARA

Wanachuo kutoka Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya kilichopo Kwimba mkoani Mwanza, Mei 26, 2023 wametembelea makazi ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere yaliyopo Mwitongo Butiama mkoani Mara, wakisali kando ya kaburi lake na wakizunguka kuona maisha halisi ya kiongozi huyo wa Tanzania aliyeliongoza taifa hili kwa miaka 23.

Ziara yao hiyo iliyotumia zaidi ya saa sita kuzunguka katika makazi hayo, kutembelea maeneo mbali, wakipiga picha kupata maelezo kadhaa na kuuliza maswali na yaliyojibiwa na wasimamizi wa makazi hayo kwa kina.

Akiambatana na wanachuo wake, mkufunzi mwandamizi wa chuo hiki Denis Kayombo akizungumza kando ya makazi hayo alisema kuwa kwa sehemu kubwa wakurufunzi wake wamejifunza mengi juu ya maisha ya Mwalimu Nyerere katika somo la Historia katika ngazi kadhaa za elimu ya Tanzania, hapa Mwitongo wapo kuuona uhalisia wa maisha ya Mwalimu Nyerere.

“Kubwa ni kuona baadhi ya kumbukumbu zilizohifadhiwa na kupata uhalisia wa maisha ya kiongozi wetu.”

Wakurufunzi hao walielezwa kuwa Mwalimu Nyerere akiwa anafundisha Shule ya Sekondari ya Pugu somo mojawapo alilolifundisha ni Elimu ya Viungo na Michezo (Phisical Education) ambalo linasomwa na wakurufunzi hao kwa sasa. Huku Mwalimu Nyerere akifundisha somo Viumbe Hai (Biology) na Historia.

“Watu wengi wanashangazwa ilikuwaje Mwalimu Nyerere alifundisha masomo ambayo ukiyaangalia hayaendani, lakini sisi tunafahamu kuwa Elimu ya Viungo na Michezo inalingana fika la Elimu ya Viumbe Hai, kama vile misuli na viungo vya binadamu inavyofanya kazi.”

Alisema Mkufunzi Monika Kalonga ambaye nayeye aliambatana na wakurufunzi hao.



Wakiwa katika hatua za mwisho za ziara hiyo hapo hapo Butiama walifika upande wa Makumbusho ya Baba wa Taifa hapo waliona vifaa kadhaa ambayo vilitumika na Mwalimu Nyerere; mavazi, viatu, majembe, vigoda na zana nyingine huku redio kubwa yenye uzito wa Kilogramu 20 ikiwavutia wengi.

“Tumeambiwa Mwalimu Nyerere wakati wa ziara zake zote alikuwa akitembea na redio hiyo ambayo alipewa huko Ujerumani na akitumia kusikiliza taarifa mbalimbali za kidunia, kumbe Mwlaimu Nyerere alikuwa mpenzi wa kufahamu ulimwengu unavyokwenda.”

Haya yanasemwa na Tabu Masele ambaye ni mkurufunzi wa chuo hiki huku akiwa mratibu msaidizi wa ziara hiyo.



Awali kabla ya kuingia ndani ya makumbusho hayo walipiga picha ya pamoja iliyotanguliwa na maelezo mengi na marefu yakiulizwa na kujibiwa maswali kadhaa ambapo Tabu Masele aliuliza kama Mwalimu Nyerere alikuwa na watoto wengine zaidi ya hawa wanaotajwa? Hilo likiwa swali la maisha binafsi ya kiongozi huyo. Swali hilo lilijibiwa kuwa Mwalimu Nyerere hana watoto wengine zaidi ya hawa wanaotajwa nah ata yule asaari aliyefariki katika vita vya Uganda hakuwa mtoto wa Mwlaimu Nyerere bali alizaliwa katika kijiji jirani na Mwitongo, huku maswali kadhaa yakiulizwa ambayo yaliibua maelezo haya,

“Mwalimu Nyerere akiwa mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Tabora alipewa mke na familia yao ambaye hakumuoa wala kuishi naye , huku akimtunza kwa kipindi chote cha uhai wake, mwanamke pekee aliyemuoa na kuishi naye ni Mama Maria Nyerere.”

Majibu hayo yaliibua maswali ya namna maisha ya Mwalimu Nyerere alivyoweza kumtunza mama huyu ambaye ilielezwa yu hai hadi leo. Huku mjadala huo ukinoga mno kwa Wakurufunzi hao wakiwa ndani ya basi wakisema kuwa kwao Mwalimu Nyerere ni babu, kwa hiyo lazima kufahamu maisha binafsi ya babu yao na kiongozi wao wa zamani.







 

0/Post a Comment/Comments