WATU WANACHELEWA SERIKALI HAICHELEWI

 


Adeladius Makwega-MWANZA

Mei 29, 2023 Mwanakwetu alikuwa katikati ya Jiji la Mwanza ambapo alitumia muda wake mwingi wa siku hiyo katika ofisi moja ya serikali, mara baada ya kumaliza kilichompeleka huko alipanda daladala kutoka katika ya Jiji hilo kuelekea Nyamuhongolo ambapo kuna kituo kikubwa cha mabasi yanayokwenda maeneo mbalimbali ikiwamo Kwimba.

Hapo Nyamhongolo alifika saa nane na dakika ishirini za mchana huku ukiwa ni muda wa mabasi ya mwisho mwisho, akiwa upande wa mabasi yanayokwenda Kwimba, Sumve na Ngudu alimpa utingo shilingi 5000/=na kumwambia,

“Ninakwenda kula, narudi mara moja, tiketi yangu nakuja kuchukua, natambua basi lenu ni la mwisho, msiniache.”

Kondakta alipokea pesa hiyo na akamwambia Mwanakwetu maneno haya,

“Mzee nakukumbuka sana, nakukumbuka sana mzee wangu, tulikuja na wewe alfajiri, wewe ni abiria wetu, nakumbuka pale Malya saa 10 ya Alfajiri uliniuliza nauli hadi Mwanza ni kiasi gani ? Nikakujibu ni shilingi 6000/= Natambua wewe unatoka Chuo Cha Maendeleo ya Michezo Malya.”

Mwanakwetu akatabasamu si kwa kuwa Utingo huyo alizungumza kwa maneno yenye matamshi ya Kisukuma tu bali kutokana na utingo kumfahamu mno abiria wake mgeni.

Mwanakwetu akaenda kununua chakula chake katika mkahawa wa kando na stendi hiyo ambapo alikuwa na njaa ya siku nzima maana hakula chochote tangu Mei 28, 2023 na huku hakuwa na mfungo wa Kwaresma wala Ramadhani.

Akiwa anaagiza chakula hicho Mwanakwetu alisema maneno haya moyoni,

“Kituo hiki cha basi ni kizuri sana, lakini shida ni ukamilishaji wa miundo mbinu yake ya nje ya kituo, maana kisipomaliziwa mvua zikinyesha kinaweza kuharibika hasa eneo linalopokelea daladala la nje ya kituo bado halijakamlishwa, kinapaswa kukamilishwa mara moja kabla ya msimu wa mvua.”

Mwanakwetu akalipia chakula, akaanza kula, huku kwa kando yake walikuwapo jamaa wawili wakila chakula, jamaa hawa wawili aliwasikia wakijibizana na muuzaji wa mkahawa huu juu ya malipo ya umeme kwa kuwa walitumia kompyuta mpakato kwa kuichomeka katika umeme.

“Hapa utaratibu wetu hata kama umekula chakula cha gharama kiasi giani kama unachaji simu au unatumia kompyuta mpakato na umechomeka katika sokti yetu unatakiwa kulipa shilingi 1000/=“

Jamaa hawa walibishana na muuzaji wa kiume hivyo akaitwa mama mmiliki wa mkahawa huo wa kituo cha basi cha Nyamhongolo, alipofika akasema maneno haya,

“Jamani hapa tunalipia umeme na gharama ni kubwa, nawaombeni mlipie ili biashara zetu zisonge au mnataka turudi Musoma tukalime? Tena nyinyi ni kaka zangu ebu lipeni mara moja.”

Walizngumza maneno ya lugha moja ambayo Mwanawetu hakuitambua, wakacheka na hawa ndugu wakalipia shilingi 1000/= huku mama huyu akarudi alipokuwa ameketi katika sehemu ya kaunta.

Hawa jamaa waliolipa shilingi 1000/= mmojawpao akatoa simu yake akawa anasikiliza maelezo ambayo yalikuywa yakichezwa katika simu hiyo.

“Jamani mimi nimekuja hapa kuwaona, kuwasalimu na kuwapa pole kabla sijakwenda kule, nawaombeni kuwa ili kutatua mgogoro huu lazima nifike alafu nitakwenda kule na ndiyo maana leo nipo hapa, tambueni kuwa serikali yenu ya mhe. Rais Mama Samia haipendi migogoro…”

Jamaa hawa wakasema huyu ni mhe Said Mtanda mkuu wa mkoa wa Mara, anaonekana ni mtu mwema, kiongozi mzuri na mchapa kazi. Jamaa mmoja mwingine akasema muda wote tulikuwa tunachelewa wapi kumchagua ndugu Mtanda kuwa mkuu wa mkoa? Mwenzake akasema kuwa serikali huwa haichelewi. Mwingine yaani aliyelipa shilingi 1000/=ambaye ndiye aliyekuwa na simu iliyocheza video hiyo akasema sawa serikali huwa haichelewi lakini wananchi wake huwa wanachelewa akaendelea kusema,

“Unaweza kusema watu wa Mara ni wakorofi, hivyo aende mkorofi akawaongoze, hilo ni kosa, tunataka watu waungwana kama Mtanda. Kwa ninavyomuona huyu jamaa atatusaidia mno .”

Kumbuka msomaji wangu Mwanakwetu yu kando anakula wali wake, samaki na soda, mara akaona kwa mbali basi alilowapa nauli yake linaondoka, hivyo hawa jamaa wa mkahawa akawaomba wamfungie samaki wake haraka haraka katika mfuko na akaelekezwa alikimbilie getini kwa kulikatia denge basi hilo na kweli alikimbilia na kuwahi na kupanda, huku begi mgongoni na samaki mkononi. Akaoneshwa kiti chake na kukaa, akamla samaki na kunywa soda yake na kuendelea na safari ya Malya Kwimba.

Mwanakweu siku ya leo anasema nini?

Hawa jamaa wawili mkahawani walimkumbusha Mwnakwetu kumtakia kazi njema mhe. Said Mtanda katika kuwahudumia watu wa mkoa huu ambao ni nduguze mwalimu Julius Nyerere. Kwa hakika Mwanakwetu anaushaidi mkubwa wa uhodari wa mwanasiasa huyu (Said Mtanda) , ushahidi wa miaka karibu 12 wa kuwa kiongozi ambaye ukimwambia jambo analifanyia kazi na kulipatia ufumbuzi,yeye siyo kiongozi wa kumwambia jambo alafu aone unamsumbua.

Kwa ufupi tu na kwa faida ya wasomaji wa Mwanakwetu, mwaka 2011 Mwanakwetu aliwasiliana na ndugu Phares Magesa ambaye alikuwa mjumbe wa Halimashauri Kuu ya CCM Taifa wakati huo akitokea mkoa wa Dares Salaam, ndugu Phares Magesa ambaye alisoma Azania sekondari miaka 1990 na Mwanakwetu aliyesoma Tambaza kipindi hicho hicho wanafahamiana maana walikuwa vijana wa Dar es Salaam.



Waliwasiliana na mhe. Said Mtanda na alipopewa jambo hilo walilolilamikia mhe. Mtanda alilifanyia kazi na kuwasikiliza waliomfuta hadi jambo hilo likapatiwa ufumbuzi, wakati huo mhe.Mtanda hakuwa na nafasi yoyote kubwa, bali ni moyo wake wa kuwasaidia watu wenye shida na kuzipatia ufumbuzi kwa kuzikifikisha pahala husika na huo Mwanakwetu anasema ndiyo uongozi.

Mwanakwetu anatambua miaka hiyo 12 ni mingi inawezekana mh. Said Mtanda amesahau labda akumbushe na ndugu Phares Magesa ambaye alikuwa Rais wa Mpira Kikapu na Kiongozi wa Skauti Tanzania.Ndugu Phares Magesa kwa ambao hawamfahamu yeye ndiye mtoto wake amekubwa bingwa wa Hisabati hivi karibuni.

Mwanakwetu anaomba sana Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Mara kwa wanaopanga safu waitazame kwa umakini ili iwe na viongozi watakaendana na kumshauri vizuri mhe Said Mtanda. Mwanakwetu anatambua fika inapotazamwa kamati hiyo ya Ulinzi na Usalama wa Mkoa , Jeshi la Polisi halina shida maana wao kila mara wanabadilisha na kuhamisha makamanda wao. Idara zingine zipigwe picha kwa kina ili kuweka safu bora ili kuyafikia malengo ya wananchi na serikali, kumbuka sana maneno ya hawa jamaa wawili katika kituo cha Nyamuhongolo kuwa watu wanachelewa lakini serikali haichelewi. Mwanakwetu anasema kama watu wanachelewa na serikali inachelewa pia maana serikali ni watu na watu ni serikali.

Mwanakwetu upo ?Nakutakia siku njema.

makwadeladius@gmail.com

0717649257




0/Post a Comment/Comments