FURAHA NA MATUMAINI II

 


Adeladius Makwega-MWANZA

Sura yake ya kwanza inaeleza hadhi ya binadamu yeyote: ingawa karibu wote wanakubali kuwa mtu ni kiumbe bora duniani, Kanisa linasisitiza ukweli huo kwa kumuona na kumuita “sura ya Mungu” hata baada ya kuathiriwa na dhambi.

Ndio msingi wa heshima anayostahili katika mwili na zaidi katika roho ambayo kwa akili inaweza kujipatia ukweli na hekima, kwa dhamiri inasikia wito wa Mungu, na kwa hiari inaweza kuuitikia.

Lakini Kanisa, pamoja na kusisitiza hiari kama wanavyofanya wengi siku hizi, linahimiza pia kuitumia vizuri, kwa kuwa mwishoni kila mtu atahukumiwa juu ya matumizi ya vipawa vyake.

Baada ya kukabili suala la kifo kwa kutangaza habari njema ya ufufuko, hati inakabili janga mojawapo la siku hizi, yaani kwamba wengi wanakanusha uwepo wa Mungu au wanaishi bila ya kumjali yeye.

“Mtaguso ulifikiria hasa ukomunisti na misimamo mingine ya kupinga na kuzuia dini zote, lakini badala ya kuilaani tu, umehimiza Wakristo wajadiliane na kushirikiana nayo, pamoja na kutoa ushuhuda wa maisha bora, ukikiri kuwa pengine mifano yao mibaya ndiyo iliyosababisha wengi wakose imani.”

Mwisho inachorwa taswira ya Yesu Kristo,mtu mpya, ambaye pekee yake anaangaza fumbo la binadamu pamoja na uchungu na kifo.

Katika sura ya pili kwa kifupi inatoa mafundisho kuhusu jamii yanayozingatia mpango wa Mungu wa kuwa watu waishi kwa ushirikiano: kuukamilisha kwa msingi wa haki ni muhimu kuliko maendeleo ya ufundi tu.

“Kwa ajili hiyo kila mtu awajibike kuhusu wenzake wote bila ya kumsahau hata mmoja, akiwa jirani na wa wenye shida na kujitahidi kustawisha usawa kwa kutumia nafasi yoyote aliyonayo katika jamii.Maadili ya kibinafsi hayakubaliki, bali wajibu mkuu mmojawapo ni kujihusisha na ustawi wa jamii na mshikamano ili wote kwa neema ya Kristo waishi kijamaa.(kidugu).”

Sura ya tatu yenyewe inalipigia chapuo msimamo kuhusu utendaji wa binadamu ulimwenguni.Hasa leo ambapo maendeleo ni ya haraka watu wanajiuliza kuhusu maana ya juhudi zao na namna ya kuziendeleza. Ni hakika kuwa Mungu amewaagiza wafanye kazi na kutawala ulimwengu ili wote wapate hali ya maisha wanayostahili walio sura yake.

“Wakristo wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika  kutafuta ushindi wowote wa binadamu juu ya maadui wake ambao ni ujinga,maradhi na ufukara na ushindi huo unatangaza ukuu wa Mungu aliyemuumba binadamu .”

Pia hapa imesisitizwa binadamu asisahau kuwa ubora wake hautokani na wingi wa vitu anavyojipatia, bali unategemea tunu za kiadili anazostawisha kwa kazi yake, hasa haki na udugu.

Shida ni kwamba mara nyingi akishindwa na dhambi anafuata ubinafsi au utaifa na kuanzisha miundo ya dhuluma na vita hata kutengeneza silaha za kutosha kuangamizia uhai wowote duniani.

Mbele ya hali hiyo Wakristo wameombwa wanapaswa kutofuata mitindo ya ulimwengu bali njia ya upendo nyuma ya Kristo, wakiwa tayari kubeba msalaba wanaotwishwa wale wanaotafuta haki na amani.

Tumaini la uzima wa milele lisipunguze bidii za kuboresha maisha ya binadamu wa leo, kwa kuwa huyo anaandaliwa hapa duniani kuingia katika ufalme wa mbinguni. Katika utendaji wake mtu ana haki ya kufuata taratibu zaelimu dunia,siasa n.k.


Imani haiogopi kumuachia nafasi hiyo, kwa kuwa Mungu yuleyule aliyejifunua kwetu kwa imani ameumba pia vitu vyote na kutujalia akili na uvumbuzi. Mtaguso umelaumu mawazo finyu yanayogonganisha imani na sayansi.

Katika sura ya nne, hii inaeleza yatokanayo na zile zilizotangulia, yaani uhusiano wa Kanisa na ulimwengu.

Kanisa likiwa na lengo la milele, linaishi duniani na wanae pia raia wa nchi zao. Hivyo linachangia ustawi wa binadamu pamoja na kupokea kwa shukrani misaada mbalimbali ya walimwengu. Lina ujumbe kwa watu wote kuhusu wokovu, lakini pia kuhusu maisha haya, hasa hadhi na haki za kila mtu.

“Kwa hiyo, ingawa utume wa Kanisa ni wa kidini hasa, linashughulikia pia ustawi wa jamii na umoja wa mataifa. Wakristo wasisahau tena majukumu yao ya kidunia, wala wasiyaone hayahusiki na imani.Mojawapo kati ya makwazo makubwa zaidi ya nyakati zetu ni utengano huo kati ya imani na maisha ya Wakristo wengi. Kwa namna ya pekee, walei wanapaswa kushughulikia malimwengu yote kwa mfano wa Yesu huko Nazareti. Wasisubiri kuagizwa na wachungaji wao, kwa kuwa kuratibu hayo ni kazi ya walei hasa.”

Mtaguso umekiri tena ukosefu wa wanakanisa na kuwahimiza kujirekebisha wasije wakazuia uenezaji wa Injili. Vilevile umeshukuru kwa juhudi za watu wowote kwa ajili ya ustawi wa familia, utamaduni, uchumi, jamii, amani na mshikamano wa kimataifa, hata ukakiri Kanisa limefaidika sana na upinzani na dhuluma za maadui wake.

Inaendelea sehemu ijayo.

makwadeladius@gmail.com

0717649257



 

0/Post a Comment/Comments