FURAHA NA MATUMAINI III

 


Adeladius Makwega-MWANZA

Baada ya kumaliza kueleza kwa jumla jinsi Kanisa linavyohusika na wito wa binadamu, hati hii katika sehemu ya pili inakabili masuala kadhaa yaliyo muhimu zaidi kwa watu wa leo.

Kati ya hayo sura ya kwanza inafafanua kwanza hadhi ya ndoa na familia na namna ya kuzipa nafasi za kufaa, kwa sababu mengine mengi yanategemea hali ya familia. Baada ya kueleza utakatifu wa ndoa, kwa kuifananisha na hali ya kuwekwa wakfu kwa njia ya sakramenti za kudumu, mtaguso umeonyesha ubora wa upendo kati ya mume na mke na namna ya kuutekeleza, ukisisitiza unavyoelekea uzazi.

Hivyo watu wa ndoa wanapaswa kupanga kwa pamoja mbele ya Mungu na kwa kuzingatia mafundisho ya Kanisa ili wazae kwa busara na ukarimu.

Kwa namna ya pekee inasisitizwa kuwa ni lazima uhai wa binadamu kisha kuanza ulindwe kwa bidii zote: kuua mimba au mtoto ni maovu ya kutisha.

Katika magumu yanayohusu uzazi wa mpango, wanandoa wajitahidi kuwa na kiasi na kufuata usafi wa moyo jinsi inavyowafaa.

“Hata jamii nzima inatakiwa kuchangia ustawi wa familia: viongozi watunge sheria na kufanya mipango kwa ajili hiyo; wanasayansi waendelee kutafuta njia halali za kupanga uzazi; mapadri wafanye juu chini familia ziishe kwa utulivu.”

Sura pili hii inafikiria namna za kustawisha utamaduni, yaani zile namna maalumu ambazo binadamu anakabili maisha katika mazingira na nyakati mbalimbali kulingana na orodha ya tunu anazothamini. Tofauti na wanyama, yeye hawezi kufikia hali ya maisha ya kumfaa kweli asipoyafanyia kazi mema yaliyoumbwa na Mungu ndani mwake na kandokando yake.

Kila kabila na kundi la watu lina utajiri wake ambamo binadamu achote ili kujiendeleza na kuwaendeleza wenzake.

Lakini huu wa leo ni wakati mpya wa historia kwa sababu ya mabadiliko ya haraka mno. Upande mmoja zimefunguliwa njia mpya za kukuza na kueneza elimu na za kuunganisha aina tofauti za utamaduni. Upande mwingine kuna hatari za kufuta hekima na sura maalumu za kila jamii, kuvuruga mafungamano kati ya vizazi, kuacha elimu ya juu mikononi mwa wataalamu tu n.k.

Kufuatana na amri ya upendo Wakristo wanatakiwa kuchangia na wenzao ujenzi wa ulimwengu ili wote waone vizuri kazi ya Mungu na namna ya kuiendeleza.

“Kama vile yeye alivyotumia utamaduni wa watu ajifunue kwao, ndivyo Kanisa pia lilivyofanya na linavyopaswa kufanya katika kueneza habari njema. Lenyewe limetumwa kwa mataifa yote, hivyo halibanwi na utamaduni wowote, bali linautumia na kuuchangia, linausafisha na kuuinua lisiishie ndani yake.”

Ni wajibu wa wote kujitahidi kufuta ujinga kwa kueneza elimu hasa ya msingi ili kila mtu aweze kuchangia zaidi ustawi wa jamii. Vilevile kila mtu aelewe wajibu wa kujiendeleza kiutu na Kiroho bila ya kutawaliwa na kazi za mikono tu, akitumia vitabu na vyombo vingine vya upashanaji habari, muda huru ulio nje ya kazi n.k.

Sura ya tatu inafundisha kuhusu maisha ya kiuchumi na ya kijamii ya mtu wa nyakati zetu.Ni lazima huyo awekwe juu kabisa kuliko maendeleo ya vitu, kwa kuwa ndiye mtendaji, kiini na lengo la uchumi na la jamii.



Kumbe wengi wanazingatia sheria za uchumi tu ili kutajirika iwezekanavyo.Matokeo ni kwamba mtengo kati ya mataifa, na kati ya matabaka ndani ya nchi, unazidi kuwa mkubwa. Anasa za wachache zinaleta ufukara wa kutisha wa umati hata kuhatarisha amani duniani.

Binadamu wa leo anaweza kurekebisha hali hiyo, lakini yanahitajika mageuzi mengi katika mitazamo, mazoea na miundo pia. Hapo tu ongezeko la uzalishaji litasaidia kweli, yaani litamsaidia mtu yeyote katika mahitaji yake yote ya mwili, ya nafsi na ya roho. Kwa ajili hiyo ni lazima uchumi usiachwe uende zake wala usitawaliwe na wachache, bali wote waweze kuuchangia ustawi na uongozi wake bila ya ubaguzi, wakisaidiwa kushika nafasi yao hasa kwa njia ya ustadi.

Kazi ya binadamu iheshimiwe kuliko mengine yanayohusu uchumi kwa mfanomtaji aumalighafi.Wote wana wajibu na haki ya kufanya kazi na kujipatia hivyo riziki za kutosha.

“Vilevile wana haki ya kupata muda kwa maisha ya kifamilia, hasa akina mama.Wafanyakazi ni haki yao kuchangia uongozi wa kampuni, na vilevile kuunda vyama vya kutetea haki zao hata kwa migomo.”

Mojawapo kati ya mambo yaliyozingatiwa zaidi na mtaguso ni njaa ya umati; kwa ajili hiyo umekumbusha kuwa Mungu ameumba vyote kwa ajili ya wote, basi ni lazima mali zigawiwe kwa haki na upendo.

“Ingawa mtu yeyote ana haki ya kumiliki vitu kadhaa, ni lazima kila mmoja awe na mali za kutosha, wasiwepo wenye kujipatia mali nyingi kiasi cha kuacha wengine wakose hata mahitaji.Matajiri wawajibike haraka kuwashirikisha wengine, la sivyo watakuwa wauaji wa wenye njaa.Hao wa mwisho ni haki yao kujipatia riziki kutoka utajiri wa wenzao.”

Kadiri ya mazingira tunaweza kuwa na njia mbalimbali za kuhakikisha wote wapate riziki zao  kwa desturi za ukarimu,pensheni n.k.

“Mashamba yagawiwe kwa wakulima wasiyonayo. Pesa zitumike ili kuandaa nafasi za kazi kwa watu wa leo na wa kesho wa nchi zote.Wakristo watafute ufalme wa Mungu hata katika uchumi na shughuli nyingine za kijamii.”

Inaendelea katika matini ijayo

makwadeladius@gmail.com

0717649257



0/Post a Comment/Comments