Ili Mwezi Uandame Lazima Uliotangulia Udondoke

 


Lucas Masunzu- MAKOLE

Ilikuwa inakimbilia kuwa saa mbili na nusu usiku. Kabla ya kulala Nduguyetu aliwasiliana na rafiki yake mmoja ambaye walifahamiana muda mrefu. Rafikiye huyo anaishi mji wa Kano nchini Nijeria ambako wanapatikana waigizaji wa filamu waliowahi kukonga nyoyo za watazamaji wengi ndani na nje ya nchi akina Aki na Ukwa. Walizungumza mambo mengi huku mazungumzo yao ya kijamaa yakitamatika kwa kufufua ahadi yao ya kutembeleana.

Baada ya mazungumzo hayo ndugu yetu alijitupa kitandani kwake, alichelewa sana kupata usingizi siku hiyo akajikuta kumbukumbu zake zinamkimbiza mpaka kwa Mchungaji Dkt. Paul Enenche ambaye naye anatoka huko huko Nijeria mzawa wa mji wa Orokam alikutana naye tarehe 24 Juni, 2023 katika jiji la Dodoma. Mchungaji huyo ni mwandishi wa vitabu, mhubiri, na kajaliwa talanta ya uimbaji mwenye uwezo wa kupiga vizuri mno baadhi ya ala za muziki.

Nduguyetu alikumbuka vizuri siku hiyo namna ambavyo Mchungaji huyo alivyotengeneza darasa kwa vijana na watu wote waliokamia kuwa viongozi katika maeneo mbalimbali. Alizungumza mambo mengi huku nyundo yake ya msisitizo iligonga zaidi msumari wa tabia kwa kuwa tabia ina nguvu kubwa na inatazamwa mno kwa kiongozi yeyote yule.

“Ili uwe kiongozi lazima uwe na wafuasi, tabia yako nzuri itafanya watu wengi wakufuate tena kwa hiari. Tabia nzuri huaminisha na kukupa mamlaka.  Kiongozi yeyote mwenye tabia nzuri ana mamlaka huamrisha watu katika kufanya majukumu mbalimbali na watu hao hutii. Kijana yeyote anayetaka kuwa kiongozi lazima awe msafi wa tabia maana usafi wa tabia humfanya kiongozi awe jasiri, kama hakuna ulichoficha hakuna cha kuogopa. Uchafu wowote wa tabia hupunguza ubora wa kiongozi. Mathalani uchafu ukiingia kwenye mafuta hupunguza ubora wa mafuta na ukiondolewa thamani ya mafuta hayo huongezeka. Ndivyo ilivyo kwa kiongozi tabia yoyote chafu inapoishi moyoni mwa kiongozi mathalani ya udanganyifu hupunguza ubora na thamani ya kiongozi huyo”

Kumbukumbu za ndugu yetu zilichokoza hamu ya kuandika makala haya. Nduguyetu anasema kuwa kiongozi akikosa sifa bora, ni vigumu mno hata kwa walio chini yake kufanya wajibu wao, migogoro, kutokuelewa, hujuma, utegeaji, kukosa hamasa ni baadhi ya mambo anayoweza kutaga  kiongozi huyo mwenye tabia ovu. Ili uwe kiongozi bora mathalani kanisani, kwenye biashara, kwenye siasa au kwenye utumishi wa umma dondosha tabia zote ovu kwa maana ili mwezi uandame ni lazima uliotangulia udondoke hivyo huwezi kuwa viongozi bora wakati bado unang’ang’ania tabia, hulka na mienendo mibaya.

Nakutakia siku njema, Kwa heri!

theheroluke23@gmail.com

0762665595

2023.



0/Post a Comment/Comments