Kwenye Nia Njema Mungu Hufungua Milango


Adeladius Makwega-MWANZA   

Julai 29, 2023 Mwanakwetu aliposhituka usingizini dakika 15 baadaye alichukua simu yake na kuingia katika kundi mojawapo la mitandao ya Jamii, kundi hilo ni la huko wa Songwe. Alipoingia humo alikaribisha na sentensi hii,

“Mungu adhihakiwi, yetu macho na masikio.”

Mwanakwetu alipoitazama sentensi hiyo vizuri alibaini ilikuwa imepachikwa chini ya sentensi nyingine iliyokuwa na maneno haya,

“Ukweli unachelewaga na wakati ukifika, nao huo unakuja.”

Mwanakwetu akawa anafuatilia huo mjadala kutokana na ujumbe aliyoupokea karibuni hadi ujumbe aliyoupokea mapema katika kundi hilo. Wakati anaendelea kusoma ujumbe huo akakutanna na ujumbe mwingine,

“Kichaa huyu.”

Msomaji wangu kumbuka Mwanakwetu anaendelea kusoma ujumbe huo taratibu, hatua kwa hatua, sasa akakutana na ujumbe huu,

“Pale unapogundua aliyekupiga risasi yupo ndani ya nyumba yenu.”

Huu ujumbe juu ulikuwa umepachikwa katika picha ambayo ilimuonesha mwanasiasa wa CHADEMA, Makamu Mwenyekiti wa CHADEMA, Wakili wa muda mrefu wa kujitegemea na mwanasiasa ambaye aliwahi kuwa mbunge huko Singida, mhe. Tundu Lissu.

Hapo Mwanakwetu akabaini kuwa anayezungumziwa ni mhe. Tundu Lissu.

Mwanakwetu akatupa jicho tena tena katika kundi hilo akakutana na picha kama ya ile ile iliyopachikwa katika ujumbe lakini ilikuwa ni video, akaigonga, ikafunguka na kuanza kuitazama.

“Nyie mnamjua mambo yake, nyie si mnamjua mambo yake ! Lakini kwenye hili tumsimlaumu, kwenye hili hayupo na mimi nitakwenda kufanya mkutano Chato, nilikuwa nafikiria nisiende Chato kumuombea, nisiende kumuasha, nitakwenda, nitakwenda kumwambia amka, amka uone (kelele za walihudhuria mkutano zikisikika)amke amke usilale…”

Mwanakwetu akabaini kuwa katika video ile mhe. Tundu Lissu alikuwa akihutubia mkutano mmojawapo wa siasa wa hivi karibuni.



Kumbuka msomaji wangu Mwanakwetu yu nyumbani kwake Asubuhi ya Julai 29, 2023. Mara baada ya video hiyo kukatika, Mwanakwetu akapigiwa simu na kiongozi wa Jumuiya ya Mtakatifu Yohane Mbatizaji,

“Kaka wahi jumuiya, viongozi wa Parokia wamefika, leo ni siku ya mavuno.”

Mwanakwetu akakurupuka kukimbilia jumuiya yake, akakuta wanasali na viongozi wa Parokia wapo mbele akiwamo Padri, ibada ilikuwa fupi ambapo mwisho walimwagiwa maji ya baraka na kupewa baraka ya mwisho ya ibada hiyo ya jumuiya na ibada hiyo ilikuwa fupi. Tamati ya yote viongozi wa Jumuiya wakagawa stakabadhi za michango ya mavuno hayo huku Mwanakwetu akipata stakabadhi yake namba 129.

Mwanakwetu akarudi nyumbani kwake, alipofika tu akachuku simu zake alizoziacha mezani, huku video aliyoitazama awali ikiwa bado katika kioo cha simu hiyo.

Mwanakwetu alipoiona video hiyo mara ya pili, akasema maneno haya,

“Maoni yoyote yale ya mhe. Tundu Lissu dhidi ya John Pombe Magufuli ambaye amefariki dunia, yanapaswa kutiliwa maanani leo hii sana sana na yataendelea kutiliwa maanani kwa miaka mingi. Wale tulipobahatika kuishi kipindi hichi ambao tumewaona hawa ndugu wawili, chochote tulichofanya au tunalofanya hata tunavyoongea tutabeba mzigo ya hayo hapo kesho. Hawa ndugu wawili wataendelea kuifikirisha dunia kwa kipindi kirefu sana. Vizazi vijavyo vitatamani kama vingewashuhudia hawa ndugu.”

Kumbuka Mwanakwetu yu nyumbani kwake, akaamua kufanya usafi wa nyumba yake, asubuhi hiyohiyo huku akiwatafakari ndugu hao akilini mwake.

 Hapo hapo zikamjia picha za watu watatu; Dereva wa Tundu Lissu siku ya Septemba 7, 2017, Katibu Mkuu wa Wizara wa Afya wakati huo na  pia Mbunge mhe. Salim Hassan Turky.

Mwanakwetu akamtilia maanani mno mhe Salim Turky aliyezaliwa Februari 11, 1963, ambaye alikuwa Mbunge wa CCM Jimbo la MPENDAE-ZANZIBAR.Mwanakwetu aliwaweka kiporo dereva na Katibu Mkuu wa Wizara yaAfya wakati huo kwa sababu nyingi,kumbuka mhe  Turky alifariki dunia Septemba 15, 2020.



Mwanakwetu akiwa bado akifanya usafi huo, akakumbuka mara baada ya tukio la shambulio la mh Lissu , mhe. Turky alisema maneno haya,

“Kwanza napenda kuiweka Tanzania katika hali ya usalama na ukweli, maneno mengine siyo vizuri kuzushiana, tusifanye tukio la Tundu Lissu tukataka kufanya siasa. Mimi binafsi tukio la Tundu Lissu, mbunge mwenzangu limenisononesha sana na limenisikitisha sana na nikiwa kama kamishina wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini kabla ya hapo pia mimi ni binadamu, ninaamini kuna kuzaliwa na kufa. Kwa hiyo tukio lilivyotokeza, tuliitwa na spika wetu(Job Ndugai), makamishina tukakaa na bahati nzuri Bwana Mbowe na Bwana Msigwa, spika(Job Ndugai) na timu yake, waziri wa afya na madaktari, sote tukashirikiana pale. Yaliyopita, yamepita mengi.  Swali lako ni dogo tu ni kuniuliza kuhusu ndege, kwanza nikujibu ilikuwapo pale airport ambayo ilikuwa imeshaagizwa na Bunge kupitia Bima yaAfya, ilikuwa stand bye kumchukua mgonjwa huyu, kumpeleka Muhimbili, sasa kilichotokelezea, wenyewe walivyoamua huyu mgonjwa lazima aende Nairobi, ndege ile ilikuwa haina kibali cha kwenda Nairobi, ili uende Nairobi inabidi uwe na marubani wawili, bahati nzuri spika(Job Ndugai) alihangaika kuipatia kibali, iweze kumchukua kumpeleka Nairobi yule mgonjwa. Kilichotokelezea, rubani akasema kuna kitu kinaitwa Landing Instrument ndege hii haina kwa kule Nairobi, kwa hiyo haitoweza kuruka, hapo tukaingia katika dilemma tunafanyaje katika hali kama hiyo? Kwa hivyo mimi nikatumia uwezo niliyojaliwa na Mungu,  nikatafuta ndege kwa Flight link, kwa ndugu zetu tunaofanya nao biashara sana,wakatoa bei za juu sana lakini kwa kuwa tunafahamiana, wakatoa bei hizo watakusaidia kwa dola 9200 pamoja na ambulace, kwa hiyo ile ndege mimi ndiye niliyeiita kwa kukubaliana na mwenyekiti wa CHADEMA,  Bwana Mbowe na Bwana Msingwa wakisema, ‘Turky ! haya mambo yasimamie, sisi baadaye tutakuja kuyasatled’ na ndicho kilichotokelezea, kwa hiyo wao walipofika kule, siku ya pili ilibidi warekebishe mambo yale, lakini walipofika kule hawakuweza, siku ya tatu imepita, Jumanne imepita , Jumatano jana imepita naona leo Bungeni watu wameanza kuzungumza, na nafikiri katika taarifa ya Spika (Job Ndugai ) alizungumza, ‘Bwana Turky alitoa pesa hizo na CHADEMA watalipa.’ Hii ni kauli ambayo haina matatizo kwa sababu kama CHADEMA wasingelipa mpaka leo, lazima mimi ningetoa pesa zangu, niwalipe kwa sababu wale mabwana wangekuwa wameshapitiliza zile siku, siku zingeshakuwa nyingi. Kwa bahati nzuri mchana huu wa leo, saa sita na nusu, nimempigia mwenye ndege, akasema ‘CHADEMA wamekwenda kumlipa.’ Kwa bahati mbaya siku ile ndege isingeweza kuruka kama zisingeweza kupata dola 9000, maana lazima pesa zile ulipe ndipo ndege ile iruke na hapo Dodoma hakuna hata mmoja ambaye alikuwa na dola 1000, ilikuwa kidogo, hali ngumu! Lakini tunamshukuru mwenyezi Mungu. Kwenye Nia njema Mungu hufungua Milango Yake.”





Mwanakwetu Upo?



Mwanakwetu hayo ni maelezo ya mhe. Salim Turky aliyekuwa mbunge wa CCM, aliyefanya kitendo cha utu kwa mbunge CHADEMA, mbunge wa upinzani. Utu , uungwana wa hali ya juu na funzo kwa walio wengi; watu wa kawaida na viongozi wetu. Funzo hilo ndiyo limekuwa hamira kwa Mwanakwetu kuandika matini haya leo hii likichochewa na mjadala wa kundi lile la Songwe.

Mwanakwetu anasema kuwa linapotokea tukio lolote kwa mwanadamu mwenzako, wewe kama mwanadamu uliye kando unatakiwa kuokoa jahazi kamaaliyofanya mhe Turky ambaye nayeye leo ni marehemu.

Msomaji wnagu yakumbuke maneno ya mhe Turky kuwa Kwenye Nia Njema Mungu Hufungua Milango Yake.Msomaji wangu tena na tena kumbuka Septemba 15, 2023 itatimia miaka mitatu tangu alipofariki dunia mhe Salim Turky, aliyekuwa mbunge wa MPENDAE. Staki kuweka neno linguine lakini Kwenye Nia njema Mungu hufungua Milango Yake.

Nakutakia siku njema.

makwadeladius@gmail.com

0717649257



0/Post a Comment/Comments