Rafiki Watatu wa Mwanakwetu

 



Adeladius Makwega –MWANZA

Mwanakwetu alifika katika eneo kilipo Chuo Cha Maendeleo ya Michezo Malya, Kwimba- Mkoani Mwanza mwishoni mwa Aprili 2023, alipokanyaga katika mandhari ya chuo hiki alikaribishwa na sauti la ndege waliokuwa wakipiga kelele sana katika mti iliyokuwa mingi katika eneo hilo lenye viwanja kadhaa vya michezo, madarasa na ukumbi mkubwa wa michezo mbalimbali.


Mwanakwetu katika shajara yake ya mwaka 2021 anakumbuka aliwahi kufika Malya akiambatana na aliyekuwa Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo wakati huo mhe Pauline Gekul.Shajara ya Mwanakwetu inaeleza kuwa safari hiyo ilikuwa ngumu sana maana gari alilopanda Mwanakwetu la Serikali injini yake ilifia njiani wakielekea Malya, huku wakifika hapo na kurudi Dodoma kwa gari la hisani.

Sasa Mwanakwetu yu Malya mara ya pili. Akiwa anazunguka katika viunga vya eneo hilo alikutana na kijana mmoja, mwembamba , mrefu na mweupe.

“Kaka samahani, Shikamoo! Wewe ni Kazimbaya Makwega? Kama ninakufananisha! Samahani sana kwa kuuchukua muda wako, mimi ninaitwa mwalimu Hamza Jafari, mwalimu wa Shule ya Msingi Ubiri iliyoyopo katika Halmashauri ya Lushoto Mkoani Tanga, nipo hapa chuoni ninasoma Stashahada ya Michezo, mwaka wa pili na wa mwisho.”

Hapo Mwanakwetu kasimama anayasikiliza maelezo hayo na kweli  Mungu bahati Mwanakwetu alimkumbuka mwalimu Hamza Jafari vizuri, wakayazungumza mengi, huku Mwanakwetu akimuuliza mwalimu Hamza Jafari aliwezeje kufika Chuo cha Maendelea ya Michezo Malya kilichopo umbali mrefu na Halmashauri ya Lushoto?

Mwalimu Hamza alimjibu,

“Kuna mwalimu anaitwa Secilia Ngovu, Unamkumbuka? ninayefundisha naye shule moja pale pale Ubiri, aliwahi kusoma hapa Malya miaka ya nyuma, aliponiambia juu ya chuo hiki nikavutiwa, nilitambua nina elimu ya cheti cha ualimu na nina alama za ufaulu wa kidato cha nne na nina alama za ufaulu nzuri za kidato cha sita, hivyo nikawa na sifa za kujiunga na Stashahada, nikakata shauri, baada ya taarifa hiyo nikafika hapa, nikajiunga na chuo hiki ndiyo maana tumekutana.”

Msomaji wangu hiyo ilikuwa ni siku ya kwanza ya Mwanakwetu akiwa hapa Chuo Cha Maendeleo ya Michezo Malya, huyu mwalimu Hamza Jafari alifahamiana na Mwanakwetu kwa mara ya kwanza mwaka 2016 huku Lushoto Tanga, miaka nane iliyopita.



Kumbuka msomaji wangu Mwanakwetu alikaribishwa na milio ya ndege juu ya mti, kwa kuwa mwalimu Jafari Hamza yeye alikuwa mwenyeji hapa Malya zaidi ya Mwanakwetu, Mwanakwetu akamuuliza juu ya ndege hawa waliokuwa wakipiga kelele.

Mwalimu Hamza alimtafuta binti mmoja wa Kisukuma anayefahamika kama Neema Masunzu ambaye alicheka sana pale alipoulizwa juu ya ndege hao, alafu akasema,

“Hao hawa ndege ni jamii ya Flamingo, huku tunawaitwa Kimelanzoka maana wanakula sana nyoka na wanapenda kukaa katika miti inayofahamika kama Msina, humu juu yake hujenga matundi yao na hizo kelele juu ni zao na mkinda yao.”

Hapo Mwanakwetu ni kuku mgeni, akasikiliza vizuri maelezo hayo Neema Msunzu akaongeza  kuwa,

“Ndege hawa huwa wanafika katika eneo jirani na Chuo cha Malya na maeneo mengine, yenye miti mingi ya Msina mwezi wa 4 na 5 na hukaa hapo na kutaga mayai hadi kutotoa watoto wao wakiwa wakubwa mwezi wa 9 na 10 ambapo mvua zikianza kunyesha huwa wanaondoka kuelekea maeneo ambayo hayana mvua kama sana wakati huo kama vile Morogoro, miezi hiyo hapa Malya huwa hawaonekani tena hadi mwezi 4 wa mwaka mwingine.”




Mwanakwetu hiyo ni siku ya kwanza hapa Malya, alifika kwa wakubwa wa Chuo hiki na kukutana na Makamu Mkuu wa Chuo ndugu Alex Mkenyenge na baadaye akapelekwa kwa Mkuu wa Chuo ndugu Richard Mganga ambaye alimueleza Mwanakwetu haya,

“Karibu sana Malya Mwanakwetu, hapa tupo, tunachapa kazi, tunaijenga Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hapa tunatoa kozi mbalimbali kama vile; Stashahada ya Elimu ya Uongozi na Utawala katika Michezo (Ordinary Diploma in Sports Development & Adrminstration), Stashahada ya Ufundishaji Michezo (Ordinary Dipoloma in Sports Coartching Education), Stshahada ya Elimu ya Michezo(Ordinary Diploma in Physical Education & Sports na Kozi ya Astashahada ya Elimu ya Michezo kwa Wanamichezo (Basic Techinician in Certificate in Physical Education and Sports).”

Mwanakwetu yu Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya, sasa ana marafiki watatu; wakazi wa Malya , wakufunzi, watumishi wa chuo hiki, Wanachuo wanaosoma chuo hiki na ndege hawa Kilimanzoka ambao  walikuwa wa kwanza wa kumuimbia wimbo wa ukaribisho alipofika Malya.

Mwanakwetu akapata marafiki wengi kama alivyokudokeza mmojawapo ni Faraja Msigwa huyu ni mzaliwa wa Pwani lakini kwa asili yeye ni Mhehe wa Iringa jirani na Lilinga Ngome ya Chifu Mkwawa, yeye ni mtumishi wa umma huko Mkoani Kagera, kwa kuwa Mwanakwetu anamfahamu Binti Msigwa miaka mingi akamuuiliza haya ulifikaje huku ?

“Mimi nilikuwa na rafiki yangu tunafanya nae kazi huko huko Kagera, alinieleza na mimi nikaingia katika mtandao ya kijamii nikachukua fomu na kuijaza na ndiyo mama sasa ninasoma hapa. Maana nina cheti cha ualimu kwa hiyo sifa hiyo ninayo na nitasoma hapa hadi nikapomaliza Stashahada yangu, alafu nitajiunga na Chuo Kikuu.”

Mwanakwetu pia alipata marafiki zake wengine watatu Grace Mpokonya, Elias Mashenzi na Mohamed Mussa, kumbuka hawa ndugu anawafahamu miaka mingi .

Mohamed Mussa yeye anatokea mkoani Dodoma

“Mimi nimeshamaliza mitihani yangu, hapa nipo njiani kuelekea Dodoma Makao Makuu ya nchi, sisi tumekaa miaka mingi tangu 2021, nimeshapata ujuzi wangu mkubwa wa michezo na  kiu yangu ilikuwa kuufahamu, kuucheza na kuufundshia mchezo wa mpira wa kikapu, kwa hiyo ninarudi Dodoma kazini. nitaendelea kujituma na kufuata  taratibu zote ili niweze kuwa mahiri zaidi katika mchezo huo kuufundisha ndani na nje ya Tanzania.”

Msomaji wangu upo?

Rafiki kadhaa wa Mwanakwetu sasa wanaondoka, Mohammed Musa anarudi Dodoma kamaliza masomo yake , Hamza Jafari anarudi Lushoto kamaliza masomo yake , Grace Mpokonya anakwenda zake Rukwa likizo, naye Elias Mashenzi anakwenda zake Geita likizo lakini huyu na Faraja Msigwa anakwenda  zake Kagera likizo.



Mwanakwetu anabaki na rafiki zake Kimelanzoka pekee ambapo ameambiwa mwezi wa 9-10 na wao watakuwa wanaondoka kuelekea maeneo yasiyo na mvua. Mwanakwetu anapata matumaini ya kutokuwa mpekwe maana mwezi wa 8 na 9 Kimelanzoka watakuwa angani hadi hawa rafiki zake ambao hawajamaliza chuo watakaporudi akiwamo Elias Mashenzi, Grace Mpokonya na Faraja Msigwa.

Msomaji wangu Mwanakwetu siyo mpekwe, yeye sasa na Kimelanzoka jamii ya Korongo, katika kipindi hicho anatoa ahadi kwako msomaji wake kuwa atakusimulia simulizi nyingi za  rafiki zake hao watatu hapa Chuo Cha Maendeleo ya Michezo Malya umbali wa KM 100 kutoka Mwanza mjini.

Mwanakwetu Upo?

Nakutakia siku njema.

makwadeladius@gmail.com

0717649257













0/Post a Comment/Comments