Vijana Chapeni Kazi

 



Adeladius Makwega-MWANZA

Vijana wametakiwa kuwa wachapakazi, kazi iwe sehemu ya maisha yao, kupenda kuwajibika na huko kutasaidia kuweza kupata mahitaji yao yote ya kila siku kwa haki.

Hayo yamesemwa na Padri Samson Masanja, Paroko wa Parokia ya Malya, Jimbo Kuu Katoliki la Mwanza katika Kanisa la Bikira Maria Malkia wa Wamisionari, ndani ya azimisho la misa ya somo ya Jumuiya ya Mtakatifu Yosefu Mfanyakazi, Julai 29, 2023.

“Mungu alifanya kazi kutoka siku ya kwanza hadi siku ya sita, akifanya uumbaji, hata tendo la uumbaji wa mtu mme na mtu mke kwa sura na mfano wake, hilo ni tendo la kufanya kazi, tujifunze katika kufanya kazi ambayo ni heshima, Mtakatifu Yosefu ni yule anayatoka katika ukoo wa Daudi, ni yule aliyemposa Bikira Mariamu, tunatakiwa kufanya kazi kama alivyokuwa mtakatifu huyu ambaye ni somo wa jumuiya yenu.”

Padri Masanja alisema kuwa Yosefu alimtunza Bikira Mariamu na Yesu kwa nguvu zake zote na kwa jasho lake lote bila ya kuchoka , hata Yesu alitambuliwa na jamii yake kama ni mwana wa seremala , kazi ya baba wa Yesu ilitambuliwa vizuri, kazi ya Useremala ilitumika kuitunza familia yake.

“Nawaombeni mtambue kuwa kazi mnazofanya ziwe na heshima katika jamii unayoishi, usikubali mtu yoyote haidharau kazi yako au kuikejeri, kazi ni kitu kizuri. Je sisi ni wakereketwa wa kufanya kazi?  Sisi ni Wakereketwa wa kuipenda kazi ? Muepuke kupiga soga ambao ni uvivu, huo uvivu unaweza kuwapeleka kuwa wezi na ombaomba.”

Katika misa hiyo pia kulikuwa na nia kadhaa ikiwamo kuombea wahitimu kadhaa wa mafunzo mbalimbali Chuoni Malya, huku viongozi kadhaa wa Jumuiya ya Mtakatifu Yosefu Mfanyakazi wakila kiapo.





Akizungumza mwishoni mwa misa hiyo Mwenyekiti wa Jumuiya ya Mtakatifu Yosefu Mfanyakazi mwalimu Denis Kayombo alimshukuru Padri Masanja kwa kusalisha misa hiyo huku akinukuu maneno haya,

“Mungu alituumba bila ya matakwa yetu , lakini hatuwezi kufika kwake bila ya kuonesha ushirikiano.”

Hiyo ikiwa ni tafakari ya Mtakatifu Agustino inayosistiza kila mmoja kutekeleza wajibu wake pahala alipo.










0/Post a Comment/Comments