HESHIMA YA WATANZANIA

 


Adeladius Makwega-MWANZA

Mwishoni mwa mwaka 2009 Mwanakwetu alikuwa akiishi nyumbani kwao Mbagala Dar es Salaam na wakati huo akiwa mtumishi wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) Kama Mtayarishaji Vipindi vya Redio, siku iliyotagulia aliingia kazini zamu ya saa 4 usiku na kutoka saa 11 ya alfajiri na kurudi nyumbani kwao Mbagala.

Desturi ya zamu za usiku, ukirudi nyumbani unalala kidogo alafu kukicha unaamkia kufanya shughuli za hapa na pale.

Mwanakwetu siku hiyo kazi yake na mwisho ilikuwa ni kuwalisha wanyama wake ikiwamo kuku, bata na kanga alafu akatoka hapo nyumbani na kuelekea Mbagala Sabasaba, kuna kijiwe kinachoitwa kwa Gervasi kijiwe hicho ni kwa fundi viatu ambapo tangu miaka ya 1980 alikuwepo fundi viatu anayeitwa Mirusu ambaye alishiriki vita vya Kagera kama Mgambo, umri wake ulipokwisha akawa fundi viatu na mwishoni mwa 1999 alihamia shambani kwake huko Kisere akawa mkulima, huyu fundi wa zamani ndugu Mirusu ni Mndengereko wa asili ya Mbagala ambaye alisoma na Baba wa Mwanakwetu shule ya msingi.

Hapo Mwanakwetu anakwenda kushinda katika kijiwe cha baba yake mdogo(MIRUSU),baada ya Miruso kwenda shambani,  kijana wa Kimbugu Gervasi akarithi hiyo mikoba , akawa anafanya biashara zake hapo.

Mwanakwetu anashinda hapo mara nyingi tangu akiwa mdogo maana hapo kuna hadithi nyingi sana likiwa eneo jirani na Mbagala Kimicha.

Siku hiyo alipofika alikuta  jamaa zake wengi wakiwa katika taharuki kubwa wakisema,

“Afadhali Mwalimu Makwega umefika, siku hizi hauonekani sana, maana tangu uoe binti wa Kimbugu/Kisambaa Dada yake Gervasi umekuwa mbali na sisi.”

Kumbuka msomaji wangu hawa jamaa wanamfahamu Mwanakwetu kitambo tangu akiwa mdogo,kijana , mwalimu sasa ni Mtanganzaji wa RTD lakini ualimu bado ulikuwa umemvaa Mwanakwetu, Kumbuka hata Mtangazaji na Mwanahabari ni walimu wa umma, hivyo Mwanakwetu hadi sasa ni mwalimu wa umma.

“Sasa Mwalimu Makwega hapa kapita askari wa JWTZ, kamchukua jamaa kisa amevaa kaptura yenye mabaka mabaka , tumeongea naye hajatuelewa, tunakuomba tusaidie, yule yule, yule pale anaondoka naye pengine anaelekea naye Mbagala Maturubai(Polisi), tunakuomba Mwalimu okoa jahazi, kamuombee msamaha.”

Eneo hilo wakati huo kulikuwa na madereva na daladala wengi wakishuka hapo, wanapumzika na kula chakula kwa mama mmoja mama ntilie, huku daladala hizo wanapewa madereva wa dei waka(day work). Wakati madereva walidamka na mabasi hayo alfajiri wakipumzika.



Mwanakwetu akawauliza,

“Huyo kijana mnamfahamu?”

Wakajibu kuwa hata wewe unamafahamu. Mwanakwetu akauliza swali lingine ,

“Siyo mharifu?”

Wakamjibu ndiyo, Mwanakwetu akauliza swali tena,

“Hiyo kaptura aliitoa wapi?”

Jamaa mmoja anayeitwa Msofe , akiwa pia ni dereva daladala na Mpare wa Same akajibu,

“Kaka alikwenda kuipointi Tandika Mitumbani .”

Mwanakwetu akakumbuka akilini mwake ni kweli hizo nguo zinauzwa katika mitumba, zinapoingia wauzaji hawataki hasara wanazipeleka sokoni na wadau wananunua, maana wako baadhi ya watu walipokuwa wadogo waliulizwa swali hili shuleni

“What are you going to be?

Walijibu

“I shall be Soldier.”

Maisha yanavyokwenda na ndoto hizo hawazifikii kwa hiyo wanasikia fahari sana kuzivaa nguo hizo tu na si waharifu.

Mwanakwetu na Msofe wakaelekea huko alipoelekea askari na kijana huyo. Walipofika katika makazi ya mhe.Ramadhani Abdallah Zame ambaye awali aliikuwa Naibu Meya na baadaye akawa Meya wa Jiji la Dar es Salaam baada ya Kitwana Kondo (KK)Kushindwa kesi mahakamani na huyu Mwenyekiti wa CCM Dar es Salaam sasa Abbasi Mtemvu(Haya msomaji wangu nakwambia tu haya kwa hisani ya Shajara ya Mwanakwetu).

Hapa kwa Mhe. Zame pana Msikiti wa miaka mingi sana unaofahamika kama Masjidi Zame.

Mwanakwetuu akasema,

“Afande samahani, huyu ni kijana wetu, tunaungama mbele yako amefanya kosa kubwa kwa mujibu wa sheria, huyu kijana ni dereva wa daladala za Rangitatu-Kariakoo , hawa ni wadogo zangu, siyo waharifu, nakuomba msamaha kwako na kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kosa alillolifanya.”

Afande wa JWTZ muungwana sana akasema mbona unamuombea wewe msamaha yeye hana mdomo? Kijana huyu dereva wa daladala akaomba msamaha, askari huyu akaupokea msamaha huo na kusema  haya,

“Mimi ninamsamehee, siku nyingine asinunue nguo zenye mabaka mabaka kama haya ni kosa, maana hizi ni mali ya JWTZ na mtu yoyote harusiwi kuivaa, sasa hii nguo kwa kuwa nimeikamata hawezi kuondoka nayo, fanyeni utaratibu hii nguo nibaki nayo.”

Kwa kuwa eneo hilo lote Mwanakwetu ni mwenyeji akaingia nyumbani kwa mhe Zame(Meya wa Jiji la Dar es Salaam Mstaafu) akawasalimia shikamoni yeye na mkewe Zuweni Binti Huruga

“Haya mkina Makwega! Vipi kwangu kulikoni? Maana rafiki yako hayupo Tanzania, eee umekuja kusali katika msikiti wetu?”

Mwanakwetu akajibu na kueleza tukio hilo alafu akaomba kaptura ili kijana huyu ajihifadhi.

Mke wa Mhe Zame yaani Zuwena Omari Binti Huruga yeye anazaliwa Mbagala Sabasaba jirani na kina Mwanakwetu, huyu Binti Huruga amesoma na Shangazi wa Mwanakwetu anayefahamika kama Otilia Makwega.


(Mhe.Zame Meya -wa Zamani wa Jiji la Dar es Salaam na Mkewe Binti Huruga.)

Hapa kwa Mhe Zame, Mwanakwetu yupo kwa shangazi yake huyu  Binti Huruga,mama mheshimiwa, Mama mmoja mwembamba, mrefu, mweusi wa asili  na mpole.

Mama mheshimiwa akaingia chumbani kwa vijana wa kiume na kutoka na kanzu na kumpatia Mwanakwetu, naye kurudi mbele ya nyumba hii ambapo wakati huo kulikuwa flemu za maduka nyingi.Kanzu ile alipewa kijana huyu huku Meya wa Jiji wa zamani akitazama kwa mbali alafu afande akamsindikiza kijana huyu hadi katika choo cha Masjidi Zame na kijana huyu akavua kaptura yenye mabakamabaka na kumpa askari na kuivaa kanzu hiyo ya hisani ya mhe Zame.

Watu wa Mbagala kwa Makuka wakawa wengi, huku huyu Meya wa zamani anawasimulia kile kilichotokea baada ya kuambiwa na Mwanakwetu. Askari wa JWTZ aliomba kibiriti, akapewa akaiwasha kaptura hii na ilipoungua akaenda zake.

Mhe Zame ambaye sasa mzee sana akasema,

“Makwega mwambie huyo ndugu yako asiirudishe hiyo kanzu.”

Mwanakwetu akamshukuru sana mhe Zame na kurudi zao Mbagala Sabasaba, wakafika Kijiweni kwa Gervas wakawa wanamtania huyu kijana aliyekamatwa,

“Leo ungekiona cha moto, ungeenda kujaza karo la maji kwa kijiko cha chai sijui ingekuwaje, na hata huyo bosi wako Baniani daladala lake angempa dereva mwingine.”

Msomaji wangu kumbuka wadau hapo kando kijiweni wanacheka sana.

Mwanakwetu upo?

Huyu kijana kwa kuwa alikuwa dereva wa daladala, tangu siku hiyo Mwanakwetu alikuwa akipanda bure tu kila basi alilokuwa akiendesha huyu kijana na mabasi ya madereva wengine walishuhudia tukio hilo.

Mwanakwetu siku ya leo anasema nini?

Katika kisa hiki huyu kijana hata kama asinguruhusiwa na askari huyu kwa hakika angepelekwa kituo cha Polisi Mbagala Maturubai na shauri lingefunguliwa askari wa JWTZ angekuwa shahidi tu mbele ya mahakama. Hata nduguze huyu kijana wangeenda kumtafuta hapo polisi ndugu yao na siyo kambi ya JWTZ .



Mwanakwetu anakubali kwa asilimia 100 kuwa uvaaji wa nguo za kijeshi kwa mtu ambaye si askari ni kosa lakini analipiga chapuo lake kwa sauti ya juu akikumbusha kuwa kuna nguo zinazoingia nchini kama mitumba hivyo zinapaswa kudhibitiwa huko si kwa uraiani.

Pia Mwanakwetu anakumbusha majukumu ya msingi ya JWTZ,

“Kulinda Katiba na Uhuru wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ulinzi wa Mipaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kufanya Mafunzo na Mazoezi ili kujiweka tayari Kivita wakati wote, Kufundisha umma shughuli za Ulinzi wa Taifa, Kushirikiana na Mamlaka za Kiraia katika kutoa misaada ya kibinadamu na uokoaji wakati wa maafa, Kukuza elimu ya kujitegemea na uzalishaji kupitia Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na Kushiriki katika shughuli za Ulinzi wa Amani Kimataifa.”

Hoja ya kukamata sare na nguo hizo libaki mikononi mwa Jeshi la Polisi Tanzania na kufanya hivyo kunaepusha taharuki katika jamiii, JWTZ wanaweza kutoa matamko kama nchi imeiingia katika hali ya hatari na siyo masuala ya sare, haya yabaki kwa Jeshi Polisi Tanzania.

Mwanakwetu anaiweka chini kalamu yake siku ya leo anakumbuka kuwa Watanzania tangu baada ya vita vya Kagera vilinvyomtimua Nduli Idd Amini, Watanzania wenyewe waliamua kuwapa heshima kubwa JWTZ ambapo katika mabasi ya daladala hawatozwi nauli kama ile ngekewa aliyopewa Mwanakwetu na madereva wale wa daladala wakati ule, hii ni Heshima ya Watanzania.

 

makwadeladius@gmail.com

0717649257



 

 

 

 

 

 

 

 

0/Post a Comment/Comments