MWANAFUNZI MWENYE MWANDIKO MZURI

 



 Adeladius Makwega-MWANZA

Shule ya Msingi Mtoni Kijichi ni shule iliyopo jirani sana na Bahari ya Hindi-Dar es Salaam huku kwa miaka mingi ikipokea wanafunzi kutoka Mtoni Kijichi na eneo kubwa la Mbagala, wanafunzi wengi waliokosa nafasi shule za Mbagala , Mtoni, Vijibweni na Kurasini waliweza kusoma huko japokuwa ilikuwa ni safari ndefu sana ya zaidi 45 kwa mguu na hata ngalawa.

 

Wenyeji wa asili wa Mtoni Kijichi tangu enzi ni Wandengereko na Wamakonde wakijishugulisha na uvuvi kidogo na kilimo cha kawaida. Wanafunzi waliokuwa wanatoka Mbagala walikuwa wakitembea umbali mrefu kufika shuleni hasa hasa kwa kutumia njia ya mkato ambayo ilianzia Mbagala Sabasaba(sasa Mbagala Mpili), wanashuka Bonde la Mzee Mafko, wanapita Shamba la Maua la Kadozo(Magoha) kisha wanapita kando kando ya Mbagala Spritual Centre, kando ya mashamba ya miwa na mipunga, wanapanda mlima wa Kijichi wanafika shuleni hapo na h ii ni safari ya asubuhi na alasiri kila siku jumatatu hadi ijumaa.”

 

Msomaji wangu kumbuka sana hilo hapo juu



Mwaka 1986 shule hii darasa la kwanza iliwapokea watoto wawili kusoma shuleni hapo Lydia Mwambene na Mohamed Mwarami na mwaka 1990 ilimpokea mwanafunzi mmoja anayefahamika kama Bartazary Milanzi wote kutoka Mbagala Kizinga, huku tangu awali walikuwepo wanafunzi wengi wanaotoka Mbagala Kizinga kusoma Mtoni Kijichi kama Martini Mkapa na Mwanakwetu.

Wanafunzi hawa wakiwa watoto walipita njia hiyo iliyohitaji hekima na ubabe muda mwingine ilikuweza kufika salama shuleni na kurudi nyumbani salama salimini.

Bartazary Millanzi (Kushiwa kwa jina la nyumbani sasa ni nahodha wa Meli ) na wenzake waliokuwa wanakaa Mbagala Misheni kuna siku wakati wanarudi nyumbani walikata miwa katika shamba la mkulima mmoja na kula kwa sababu ya njaa ya darasa la kwanza maana walizoe kushinda nyumbani, sasa wanatembea umbali mrefu zaidi ya saa moja njiani kwa mguu, kwenye mashamba yenye miwa tele , walipokata miw ahiyo mingi wenye shamba wakawa wanawawinda kweli kweli.

 

“Kuna watoto wamekata miwa yetu hapa shambani, wanasoma Mtoni Kijichi, tunawatafuta, waambieni tunawasaka ama zao ama zetu.”

 

Aliambiwa Mwanakwetu.

Hawa darasa la kwanza siku iliyofuata kwa kuwa walifahamu lililotokea wakabadilisha njia na kupita njia ndefu yaani njia amabyo sasa ina lami tangu kijichi hadi Mbagala Misheni, wakafika shuleni vizuri wakasoma, saa tano wakaruhusiwa, kurudi nyumbani, watoto hawa wakakubaliana jambo .

 

“Jamani tusiondoke tutapita njia ndefu hadi lini? Tumngoje kaka Adeladius tuondoke naye.”

 

Hawa darasa la kwanza walikaa hapo hadi saa nane ya mchana.

Mwanakwetu alipotoka darasani akasimama mstarini wakaruhusiwa kurudi nyumbani, akiwa anaondoka akakutana nao-Kushiwa( Bartazary Milanzi ) na wenzake watatu.

 

“Wewe Kushiwa , mnatoka saa tano, mpaka saa hizi mnafanya nini?”

 

Wakajibu,

 

“Kaka tulikuwa tunakungoja tuondoke sote.”

 

Kwa bahati nzuri huyu Kushiwa familia yake yote ilikuwa inaifahamiana kwa muda mrefu na familia ya akina Mwanakwetu huku wakisali pamoja.

Mwanakwetu akasema twendeni, wakaanza safari hiyo ya kurudi nyumbani.

Sasa kundi likawa kubwa Mwanakwetu (VII) , Mikidadi Chite(VI), Lydia Mwambene(V), Mohamed Mwarami (V) Bartazary Millanzi (Kushiwa) na wenzake watatu (I).(Namba za Kirumi Kwenye Parandesi ni Madarasa waliyokuwa wakisoma wakati Huo).


(Lydia Agrey Mwambene)

Wakiwa wanarudi nyumbani kushoto kulia na wengine kulia kushoto, njia ile ile, mara baada ya nusu saa wakafika katika mashamba ya miwa na mpunga, jamaa wakatokea wakataka kuwakamata na kuwapiga akina Kushiwa na wenzake.

 

Jamaa waliyovamia akina Mwanakwetu wakadhibitiwa

 

“Hawa wamevunja miwa yetu, lazima walipe.”

 

Ndugu hawa watoto wa darasa kwanza ndiyo mmejipanga kabisa kuwapiga?Wakaulizwa miwa mingapi ?

 

“Miwa minne angalia haya mashina moja , mbili , tatu na nne, hasa huyu bwana mdogo mweusi“

 

Wakimlalamikia Kushiwa.

 

“Kaka hawa watoto wadogo wana njaa, waacheni.”

 

Haya maneno Mwanakwetu anakumbuka alisema Mikidadi Chite, alafu akatoa shilingi tano akawapa wale jamaa wa shamba la miwa.Ugomvi ukamalizika hivyo wakaondoka zao kuelekea majumbani mwao.

Wakati mazungumza na wenye shamba yanafanyika Mwanakwetu alikuwa anawafahamu kwani walikuwa wanasali nao Kanisani Katoliki la Mtakatifu Antony wa Padua Mbgala Misheni lakini  hakuwazoea sana  zaidi ya kuziona sura tu.


Mohamed Mwarami hakusema kitu, alikuwa kimya, yeye na Lydia Mwambene katika tukio hilo. Wazungumzaji alikuwa Mikidadi Chite na Mwanakwetu na hata kwa umri na madarasa wao walikuwa wakubwa kuliko wote.

Ilipofika mwezi sita siku ya kufunga shule mwaka 1990 wanafunzi wote walikalishwa chini ya mwembe dodo mkubwa, uliokuwa na kivuli sana walimu waliwekewa madawati mbele, wakasomewa matokeo tangu darasa la kwanza hadi la saba na wale waliofanya vizuri watatu kila darasa walipewa zawadi: peni , kalamu za risasi na madaftari.

Wanafunzi wa darasa la tano aliyefanya vizuri taaluma alikuwa Mohamed Mwarami . Aliyefanya vizuri kwa darasa la saba nafasi ya kwanza alikuwa Ali Ngondo akachukua zawadi yake akatajwa wa pili na watatu.


(Bartazary Milanzi-Kushiwa)

 

(Hawa wawili wa darasa la saba simulizi zao zitazisimulia siku nyengine)

Huyu Mohamed Mwarami, mwalimu mkuu alimsifia zaidi kwa sifa zingine tatu na jumla zikiwa nne; kwanza monita bora, mwanafunzi mtulivu,Golikipa bora wa timu ya shule kwa mpira wa miguu na mwanafunzi mwenye mwandiko mzuri.

Shule nzima ilifahamika kwamba Mohammed Mwarami ni kiongozi darasani (monita), Mohammed Mwarami ana akili darasani , Mohammed Mwarami ni Golikipa Mzuri lakini hili la mwandiko mzuri waliokuwa wakifahamu ni wale waliokuwa wanasoma nae darasa moja akina Lydia Mwambene, mwalimu mkuu ambaye alikuwa mgeni wakati huo aliumwaga mtama kwenye kuku wengi.

Utani sasa ukawa ni huu wa mwanafunzi mwenye mwandiko mzuri, Mwanakwetu baadaye alikuja kufahamu kuwa Mohamed Mwarami anakaa Mbagala Kizinga jirani na kwao na mama yake akiitwa Mama Mzungu au Nyambonde-Asia Abdala Mandingo (mluguru/Mndengereko).

Mama huyu alijulikana kwa jina hilo la Mama Mzungu kwa kuwa alizaa watoto wengi weupe sana akiwamo Mohamed Mwarami mwenyewe golikipa wa timu ya shule na mwanafunzi mwenye mwandiko mzuri.

 

“Wakati Martini Pius Mkapa yupo uwanjani na Mohamed Mwarami golini, shule yoyote iligwaya, tulipokuwa tunashindana na Shule ya Mtoni Kijichi tulishindwa tu .”

 

Wanafunzi wa shule zingine walisema.



Mwanakwetu akaenda kusoma Tambaza, wakati wote huo Mohamed Mwarami alikuwa akichezea Timu ya AFC Tesema, Abuja FC na Agaton FC zilizokuwa zinafanya mazoezi pamoja.Baadaye Mohamed Mwarami anakacheza Simba alafu akacheza soka Msumbiji, Mungu bahati alipofika kocha Marcio Maximo alimchagua kuwa Golikipa namba moja wa Timu ya Taifa ya Tanzania-Taifa Stars na mechi mojawapo aliyowahi kukaa  golini ni ile ya Tanzania(1) VS Brazil (5)

Kwa kuwa mwanakwetu ni mwingi wa simulizi leo hii akasema ngoja amkumbuke ndugu yake huyu Mohamed Mwarami ambaye alikuwa mwanafunzi mwenye mwandiko mzuri wakatu huo Shule ya Msingi Mtoni Kijichi.

Mwanakwetu Upo?

Nakutakia Siku Njema.

 makwadeladius@gmail.com

0717649257


(Mohammed Mwarami)


0/Post a Comment/Comments