ANGEPATA RADHI YA MWANAKWETU

 



Adeladius Makwega-MWANZA

Mwanakwetu alifika katika taasisi hiyo mapema kidogo , siku hiyo ilikuwa ya mvua kubwa ikinyesha, hivyo mwili wake wote ulikuwa umelowa kwa mvua hiyo. Kwa kuwa ulikuwa wito wa kisheria kutokwenda lilikuwa kosa moja kubwa .

Alipofika hapo alipokelewa na ndugu mmoja ambaye sura yake haikuwa ngeni machoni mwake. Mwanakwetu alikaa kimya lakini ndugu huyu alisema ‘Naona kama ninakufahamu vile.’ Mwanakwetu nayeye akasema hata mimi naona sura yako si ngeni.

Mwanakwetu alipewa huduma hiyo vizuri na ndugu hao , hapo walionekana ni watumishi waungwana na alipomaliza alitoka zake kupanda basi kurudi nyumbani kwake.

Safari ya kurudi nyumbani kwake ilikuwa ndefu kidogo, ambapo Mwanakwetu alibahatika kupata kiti jirani na dirisha huku akipigwa na upepo wa eneo hili.

Baada ya mwendo wa dakika 20 hivi, Mwanakwetu ikamjia picha ya tukio moja la zamani.

“Baba wa Mwanakwetu anasafiri kwenda ng’ambo, mshahara wake mzee huyu anawaachia watoto wake, kazi hiyo ya kupokea mshahara huo anapewa dada/shangazi wa Mwanakwetu-anayeitwa Otilia Makwega , sasa Mwanakwetu anatakiwa kwenda shuleni, Shangazi wa Mwanakwetu akasema ’Mwanangu ngoja mshahara wa baba yako utoke, ili nikununulie vifaa vya shuleni na karo yako. Nakuomba ugoje mwisho wa mwezi.’ Kweli Mwanakwetu anagonja mshahara huo . Mazungumzo haya ya Mwanakwetu na shangazi yake yanafanyika huko Mbagala Kibonde Maji. Mwanakwetu akala ugali wa usiku huo kwa shangazi yake huyu alafu na kuanza safari ya kurudi Mbagala kwa Mangaya. Alifika Mbagala Mangaya majira ya saa 4. 30 usiku. Alipofika hapo nyumbani alipokuwa akiishi yeye na wadogo zake, alipewa ujumbe na rafiki yake anayefahamika kama Idi Mangaya kuwa ’Hapa wamefika jamaa wawili, wanashida nawe . Wamesema watarudi tena’. Kweli Mwanakwetu na Idi Mangaya walikaa hapo barazani kwa nusu saa na ndugu hao wawili walirudi alipo Mwanakwetu.

‘Kaka kwema? Tunakuomba chemba kidogo.’

Mwanakwetu alimuacha Idd Mangaya na kuongea na ndugu hao.

‘Kaka sisi tumekuja kwako, tuna shida, mimi unanifahamu nilisoma Shule ya Mtakafifu Peter Morogoro(ST Peter Seminary) na huyu ni ndugu wa shemeji yangu na huyo bwana mdogo ni mtoto kwa kaka yangu, anasoma shule ya sekondari Makongo. Huko shuleni kumetokea vurugu, hivyo wamesimamishwa shule na kesho wanatakiwa waende na wazazi wao, kwa namna tunavyomfahamu kaka, tukimwambia kesi hii itakuwa mbaya na kijana huyu atapoteza masomo yake ,kaka hatoweza kulipa ada tena, atarudi kijijini kwa mama yake, tunakuomba wewe ukamuwakilishe kaka yetu , wewe tunakuamini kazi hii utaifanya vizuri.’

Mwanakwetu akasema, sasa baba yake akijua kuwa mimi ndiye niliyeubeba ubaba bila idhini yake itakuwaje ? Na kama huko shuleni mambo yakiharibika hilo litakuwaje? Jamaa hawa wakajibu kuwa hilo halina neno maana wameshirikisha mama wa kijana huyu na babu yake na hayo ni maamuzi ya familia kumuokoa na balaa kijana huyo.

Mwanakwetu akakubaliana kuwasaidia, hivyo jamaa kuondoka zao na kulipokucha Mwanakwetu akavaa vizuri na kupanda basi na kijana huyu hadi sekondari ya Makongo. Mkuu wa Shule hii wakati huo alikuwa nadhani Kanali Kipingu , wakati huo shule hii haikuwa maarufu sana maana jina lake la zamani lilikuwa ni Lugalo Jioni. Jina la Makongo ndilo linaanzaanza , wazazi walioitwa walifika katika ofisi ya mkuu huyu wa shule na wanafunzi hao kutengwa katika makundi mawili wenye wazazi wale ambao wazazi wao walichelewa kufika. Wale wenye wazazi waliingia kwa Kanali Kipingu na kuelezwa shida ya kila mmoja alafu ikatolewa adhabu hiyo na kila mzazi kukubaliana nayo akiwamo Mwanakwetu .

Kijana alipewa adhabu hiyo mbele ya umati wa wanafunzi wa Makongo na baada ya tukio hilo Mwanakwetu alitoka hapo shuleni alitembea kwa mguu hadi Mwenge na akapanda basi hadi Mbagala. Alipofika kwake alienda nyumbani kwa hii familia na kutoa mrejesho kwa yule mseminari wa zamani na kuwaeleza kama ilivyotokea na wao kushukuru sana.

Mwisho wa Mwezi ulifika Mwanakwetu alipewa ada na shangazi yake na kuelekea shuleni  huko Ndanda Sekondari.”

Kumbuka msomaji wangu Mwanakwetu yupo katika basi anarudi nyumbani kwake kutoka ofisi hii ya umma ambapo aliitikia wito wa kisheria na hayo ameyakumbuka tu , maana kijana huyu sasa ni afisa mkubwa ambaye amemuhudumia Mwanakwetu siku hii.




Mwanakwetu ndani ya basi akasema moyoni,

“Mungu amemsaidia yule kijana alisoma, kumbe na mimi nimetia mkono wangu na sasa ana mamlaka katika taasisi hiyo ya umma.”

Mwanakwetu akafika kwake salama salimini huku akiikumbuka mno familia hiyo. Siku akienda Mbagala ataitafuta hii familia.

Je siku ya leo Mwanakwetu anasema nini?

Kijana huyu kwa sasa anaonekana ni mkubwa sana kwa mwili na pia ni mkubwa kwa mamlaka kuliko Mwanakwetu. Kwa ukweli wa Mungu Mwanakwetu ni kaka mkubwa wa ndugu huyu kama tukio hilo linavyosimuliwa maana yeye alikuwa kidato cha tatu huku Mwanakwetu kidato cha sita.




Kwa dunia namna ilivyo ndugu huyu anaweza kumtendea mema mtu aliyemsaidia au anaweza hata kumfanyia mabaya kwa sababu nyingi, mojawapo ni kusahau ule wema.Wako watu wanafanya ubaya si kwa kupenda bali wanafanya ubaya huo kwa kushinikizwa kufanya hivyo.

Ndiyo maana Jaji Joseph Warioba katika Ripoti yake ya Tume ya Rushwa ya mwaka 1996 alisema,

“Hakuna askari mbaya kama yule mwenye cheo cha juu, maana anaweza kuamrisha chochote kikafanyika kwa amri yake tu. Tujitahidi kuepukana na hilo lazima tuwe na askari kwa ngazi za juu wenye maadili mema na tabia njema.”

Huo ni mfano wa Jaji Warioba kwa Jeshi la Polisi,  Mwanakwetu anautumia kulinganisha tu hilo hata kwa taasisi zingine za uchunguzi  na hata mahakama ni vizuri kuwa na viongozi waadilifu , wema, wenye huruma , wenye mioyo ya heshima , mioyo ya utu,wenye mioyo ya kumuogopa Mungu, ilikukwepa kutoa maagizo ambayo yanakiuka hayo.

Mwanakwetu anatambua kuwa Jeshi la Polisi Tanzania linajitahidi mno katika hilo maana tangu mkoloni limepitia changamoto nyingi, hivyo Polisi Tanzania wanayo mifano kedekede ya kukumbukwa ambayo inabaki kuwa darasa kwao ambapo taasisi zingine zinapaswa kujifunza katika hayo.

Makala haya leo yanasema nini?

“Mwanakwetu anayatumia kukumbusha tu kwa kila mmoja wetu, kulipiga chapuo hasa hasa kwa wenye nafasi kujitahidi kutoa maagizo ya haki , maagizo halali ili haki iweze kustawi katika jamii ya Tanzania, haki itamalaki maana hawa Watanzania ni ndugu wanakutana na  ndugu zao wa damu pengine hata bila ya mtoa maagizo kufahamu hilo. Pata picha kama huyu kijana angemfanyia ubaya Mwanakwetu, pengine huyu kijana angeweza hata kupata radhi, duu angepata radhi ya Mwanakwetu.”

Mwanakwetu Upo?

Wengine ni Ndugu wa Damu, angepata radhi ya Mwanakwetu.

Nakutakia siku njema.

makwadeladius@gmail.com

0717649257



0/Post a Comment/Comments