KITAMBAA CHANGU CHA UBATIZO BADO CHEUPE

 



Adeladius Makwega-MWANZA

Hivi karibuni Mwanakwetu alitembelea ukurasa wa Instagram wa Julius Mtatiro ambaye ni kijana wa Kitanzania ambaye Mwanakwetu anamfahamu , Julius Mtatiro akiwa kijana pekee mwanasiasa wa Tanzania ambaye alipachika Nyaraka ya Kanisa Katoliki, inayoeleza kuhusu kuundwa kwa mahakama ya kijimbo ajili ya kutangazwa Mwenye heri na Mtakatifu -Mtumishi wa Mungu Julius Kambarage Nyerere.

Ukurasa huu ni miongoni mwa kurasa maarufu kiasi, mpaka Novemba 19, 2023 unamatukio ya kupachikwa 5791, ukifuatwa na watu 287K na akiwafuata watu 2862. Kwa tabia ya ukurasa wake na tabia za uandishi wa Mtatiro, zamani kijana huyu alikuwa anapachika habari ya ukosoaji kwa serikali sasa anaweka habari za kijamii mno maana yeye sasa ni sehemu ya serikali na ukosoaji wake upo likizo.

Kitendo cha Mtatiro kuipachika Nyaraka hiyo katika ukuta wa mtandao wake wa kijamii, kilimsaidia Mwanakwetu aliiona na kuisoma taarifa hiyo na baadaye kubaini kuwa Julius Mtatiro aliinakili kutoka ukurasa mmojawapo Instagram wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dare s Salaam.



Taarifa hiyo katika aya ya pili inasema,

“Tunawaalika waamini wote kuwasiliana nasi moja kwa moja au kutuma kwenye Mahakama ya Jimbo Kuu la Dar es Salaam inayoshughulikia mchakato huu, taarifa yoyote Iwe ya kufaa au isiyofaa-kuhusu maisha na fadhila kubwa sana za mtumishi wa Mungu, kama mwamini mlei mkatoliki na baba wa familia, pia taarifa kuhusu sifa zake za utakatifu na nguvu ya maombezi yake.”

Msomaji wangu taarifa hiyo ya Kanisa Katolilki iliongeza kuwa,

“Kwa taratibu za ushahidi wa kisheria, maandiko yote yanayodhaniwa kuwa yake yanapaswa kukusanywa, Kwa Tangazo hili tunaelekeza kwamba yeyote ambaye ana maandiko hayo ayatume kwa umakini kwa mahakama hiyo iliyotajwa, nyaraka zozote zilizoandikwa na mtumishi wa Mungu ambazo bado hazikabidhiwa kwa mratibu wa mchakato.”

Msomaji wangu hayo maandishi yaliyokaa kwa milazo ni aya ya pili na ya tatu ya barua hiyo kwa waamini iliyosainiwa na Askofu Mkuu wa Dar es Salaam Jude Thaddaeus Ruwa’ichi.

Kwa hakika waraka huo Mwanakwetu aliona unaomba nyaraka, maandishi na miswada yote ya  Mtumishi wa Mungu Julius Kambaraege Nyerere , pia umeyatazama maisha binafsi ya Mtumishi wa Mungu huyu kwa kuomba anayefahamu tabia zake njema na hata tabia zisizofaa.

Huku ukitaja taarifa za kiroho za nguvu za maombezi yake kwa sasa kama zipo.

Mwanakwetu kama mwanahabari anatumia kalamu yake kukumbusha umma wa waamini kujitokeza tu kutoa ushirikiano kwa Mahakama hiyo ya kiroho, bila ya woga wowote, hilo ni suala la imani yetu na lenye heshima kubwa kwa kila mlei mkatoliki.



Kama Mtumishi wa Mungu Julius Kambarage Nyerere atakuwa Mtakatifu, vizazi vyetu vitajifunza kwakwe kwa matendo yake na ucha Mungu na hata kama jina la likagoma na kutupwa katika mchakato huo waamini tutajifunza ubora ya kuishi ucha Mungu kiwango cha juu zaidi.

Mwanakwetu anaona kuwa mbiu ya mgambo ya waraka huo wa Kanisa unahitaji kujua zaidi maisha ya kiongozi huyu yalikuwaje? Na Majibu hayo yapo kwa wanaombwa ambao walikaa na kuishi na Mwalimu Nyerere wakati wa uhai wake.

Mwanakwetu kwa heshima zote anauombea heri mchakato huo, kwanza uweze kuzifikia nyaraka zote alizawahi kuandika Mwalimu Nyerere hasa hasa zile za siri, hapo wanaweza kumfahamu kwa karibu Mwalimu Nyerere na hapo hata hotuba zake za siri katika vikao ambavyo havikuwa wazi na pengine hadi kesho zinawezekana kuwa bado ni siri.

Mathalani mjadala wa waliwahi kunyogwa wakati wa utawala wake, mahakama iliamua kwa mujibi wa sheria,je alipopelekewa hati hizo Mwalimu Nyerere alikuwa anatoa maelezo gani kwa walio chini yake ? Je alikuwa anasikitishwa na hali hiyo au alikuwa anafanya hivyo kama kuwalipizia kisasi waliuwa wenzao?

Maana mafaili ya kiserikali yanakuwa na hoja, alafu mjadala unaanza  kwa dokezo hadi kukamilika na kwa utaratibu wa zamani mafaili hayo na mjadala huo mhusika (kiongozi ) na wenzake walio chini waliandika kwa mikono yao mwenyewe, miandiko yao itaonekana.

Je mijadala hiyo ilikuwaje? Mwalimu Nyerere alikuwa mtu wa namna gani?

Hapa shauri la mfano ni la kunyongwa kwa Said Abdalah Mwamwindi aliyempiga risasi alyekuwa mkuu wa mkoa wa Iringa Dkt .Kreluu. Je Mwalimu Nyerere alikuwa analipiza kisasi kunyongwa Mwamwindi ili kumkomesha ndugu huyu kwa alichokifanya kwa mkuu wa mkoa wa Iringa wakati huo?

Hapo Mwanakwetu anakubaliana kabisa na nyaraka hizo ziifikie mahakama hiyo, kama ilivyosisitizwa na waraka huo wa Kanisa katika aya yake ya tatu kwa walei wanaofahamu hayo na maisha ya kiongozi huyu wafanye hivyo.

Msomaji wangu katika aya pili ya waraka huu inayataja maisha ya Mwalimu Nyerere kama Baba wa familia.Kwa hakika Mwalimu Nyerere akiwa ni mkewe Mama Maria Nyerere, walikuwa na watoto kadhaa.



Kwa muda mrefu kumekuwa na mjadala juu ya maisha ya ndoa ya Mwalimu Nyerere. Kumekuwa madai juu mahusiano ya Mwalimu Nyerere na Waziri wake mdogo wa Afya Bi Lucy Lameck Somi, ambaye alikuwa muuguzi awali na mzaliwa wa Mkoa wa Kilimanjaro, akiwa ni Waziri wa kwanza mwanamke wa Tanganyika huru (1962) na baadaye Tanzania 1964.

Je hayo ni kweli?

Kama ni kweli mwalimu alikuwa mtu wa upendeleo kwa kumuhonga uwaziri Bi Lucy Lameck?

Mwanakwetu anaamini jibu moja kati mawili lipo kama ndiyo au hapana.

Kama ni kweli, Je Mwalimu aliungama katika hilo?



Hapo mchakato huu utakuwa na majibu.

Mwanakwetu anatambua kuwa suala la mitala kwa walei waliopitia mchakato wa Kanisa Katoliki kuwa Watakatifu linaonekana sana kwa Mashihidi wa Uganda (22) wale waliuwawa na Kabaka Mwanga(1885-1887) japokuwa baadhi ya watakatifu hao wengine hawakuwa na wake kabisa. Waliokuwa na mitala hiyo baada ya kuwa Wakatoliki walichagua mke mmoja na kufunga ndoa .

Mashahidi wa Uganda walikwenda mbali na kuwagawia ardhi na mifugo wake zao wa zamani kwa haki bila upendeleo wowote na hakukuwa na malalamiko yoyote baada ya kuwa Wakatoliki.Tena hawa mashahidi wa Uganda-walikuwa na watoto waliozaliwa na wake wengine kabla ya kuwa Wakatoliki.



Mwanakwetu anasema nini siku ya leo?

Katika maisha ya Mwalimu Nyerere yapo ambayo yatabaki ya kujifunza sote kwa ndugu yetu huyu baada ya mchakato kukamilika, kwa hiyo kuna umuhimu wa kutoa ushirikiana mkubwa katika mchakato huo.

Mwanakwetu anapuliza kipenga chake kuelekea katika mahakama hiyo, huku akijiuliza je Mtumishi wa Mungu Julius Nyerere wakati wa Ubatizo alipewa kitambaa cheupe, je kitambaa chake kilibaki kuwa cheupe?

Swali hilo Mwanakwetu anajiuliza na yeye mwenyewe

“Je tangu nibatizwe mwaka 1974 je Kitambaa changu cha Ubatizo bado Cheupe ?”

Jamani tujitokeze kutoa ushirikiano kwa mahakama hiyo inayosimamiwa na Buruda(kaka) Reginald D Cruiz wa Shirika la Wamisionari wa Afrika aliyeteuliwa na Vatikani kusimamia mchakato huo.

Mwanakwetu Upo?

Kitambaa Changu cha Ubatizo Bado Cheupe?Cha Mwalimu Nyerere tutapata majibu.Je wewe msomaji wangu chako je ?

Nakutakia Siku Njema

makwadeladius @gmail.com

0717649257

Huyu ndiye msimamizi wa mchakato huo Bruda  Cruizi(Kama picha ilivyotafutwa na Mwanakwetu kama siyo hiyo tunaomba radhi)





0717649257

0/Post a Comment/Comments