UTENGUZI GEKUL UMEHARAKISHWA

 


Adeladius Makwega-MWANZA

Mwanakwetu amekuwa akitafakari utenguzi wa aliyekuwa  Naibu Waziri wa Katiba na Sheria wa Tanzania Bi Pauline Gekul umefanyawa kwa haraka sana, huku akisikiliza hoja mbalimbali na mazingira ya kazi ya mwanasiasa huyu wa Tanzania ambaye ana asili ya upinzani na sasa yu chama tawala cha taifa hilo lililopo Mashariki ya Afrika.

 Mwanakwetu yupo upande wa wanaoamini kuwa jambo hilo lilipaswa kupewa muda mrefu ili kuweza kutambua shida ya tukio hilo linalodaiwa kufanya na mheshimwa Gekul linatokana na nini?

Katika hoja hiyo, kumekuwa madai kuwa Pauline Gekul ni mwanachama wa Umoja wa Wanawake Tanzania(UWT). Wanaodai hivyo wanakwenda mbali na kuyataja majina ya waliokuwa na nafasi za juu wakati wa kura za maoni CCM mwaka 2020, walikuwa pia wanachama wa UWT, yakitajwa pia majina mawili ambayo inadaiwa miongoni mwao ni Wakuu wa Wilaya katika serikali ya sasa ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo ni nafasi ya kuteuliwa na rais, lakini pia hoja hiyo inasindikizwa na bashilafu ya hata Rais mwenyewe wa sasa wa Tanzania Samia Suluhu Hassan anayo kadi ya UWT na ni mwanachama wa umoja huo wa wanawake unaotokana na bendera ya CCM yenye nyundo na jembe.

Huku utenguzi huo uikitazamwa kama nyundo ya kumponda Pauline Gekul na jembe kujimba shimo na kumfukia mwanasiasa huyu katika kaburi la kwa heri siasa mapema kabla ya 2025 ambapo uchaguzi Mkuu wa Tanzania unatarajiwa kufanyika.

Watoa hoja hii akiwamo Mwanakwetu wanaamini kuwa viongozi wajuu wa Serikali katika mataifa masikini na yale yanayosonga mbele wajitahidi mno kuwa wavumilivu kuelekea kufanya maamuzi maana katika mataifa hayo, nyadhifa/cheo ni chanzo cha kipato na kupoteza nafasi ni kupoteza kipato, watu wanapigania nafasi hizo kwa uvumba na ubani.

Mtazamo huu unakwenda na ukimtazama Pauline Gekul akiwa na asili ya upinzani,

“Je anafanyiwa hivyo kwa kuwa hana asili ya CCM?"

Hilo ni swali .

Madai hayo yanachagizwa pia na hoja kuwa Pauline Gekul ni miongoni mwa wanasiasa ambao waliandaliwa katika ulimwengu wa siasa za Tanzania na Dkt Wibload Slaa ambaye nayeye alifutiwa hati ya heshima ya kibalozi mwaka huu huu 2023 na rais wa sasa wa Tanzania.

Malalamiko hayo juu ya maamuzi hayo yanajengwa na dhana moja juu ya mgogoro wa Pauline Gekul na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Manyara wakati huo ndugu Charles Makongoro-Nyerere juu ya hoja ya mwekezaji aliyetaka kuwekeza katika mojawapo wa maeneo hapo Babati Manyara ambapo Bi Pauline Gekul alipinga.



Kwa hakika Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan alimuhamisha ndugu Makongoro na kumpeleka mkoa mwingine. Hapo hapo kukiwa na maswali ya hulka za Charles Makongoro-Nyerere , kwa desturi huwa ni mtu mpenda furaha ambaye hapendi mikwaruzano. Swali iweje kutokee mikwaruzano baina ya Charles Makongoro Nyerere na Pauline Gekul wakati hao wote waliwahi kufanya siasa za upinzani kwa nyakati tofauti?Huku Charles Nyerere siyo kiongozi mwoga?

Hapo wapo wanasiasa wengi wa upinzani ambao ni rafiki wa Charles Makongoro Nyerere na marafiki wa Pauline Gekul? Charles Nyerere amewahi kuwa Mbunge wa Arusha Mjini na anaifahamu mno Babati na wapo rafiki zake kadhaa wa NCCR Mageuzi wakati huo na sasa wapo CHADEMA?

Mwanakwetu anamfahamu Charles Makongoro Nyerere wa mwaka 1996 wakati Augustine Mrema anagombea Jimbo la Temeke kupitia NCCR Mageuzi ambapo Mwanakwetu alikuwa anaishi jirani na ofisi ya Wilaya ya NCCR Mageuzi Keko Magorofani.

“Charles Makongoro tangu wakati huo alikuwa anashiriki siasa, anafanya mikutano ya wazi, akimaliza wanarudi NCCR Mageuzi Ofisini wilayani Temeke wanaingia ndani, wanakaa kidogo alafu wanaingia mitaani kuishi vizuri na jamii ya Keko na baadaye usiku kuondoka zake nyumbani kwake, yeye alikuwa ni mtu furaha na siyo mtu wa ugomvi na mashindano yasiyokwisha.”

Katika hili juu, maswali yakiwa mengi, hasa hulka za Charles Makongoro Nyerere, hapa kuna ufanyaji wa kazi wa Mkuu wa Mkoa yoyote katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, unaongoza kwa karibu na wajumbe wa kamati ya ulinzi a usalama ya mkoa huo. Je walikuwa wanamshauri nini Mkuu wa Mkoa Charles Makongoro Nyerere?

Je hao wajumbe ndiyo waliweza kubadilisha hulka za Charles Makongoro Nyerere? Je hao wajumbe wa kamati hii ya usalama wilaya na mkoa ndiyo walikuwepo wakati kura za maoni CCM 2020 zinafanyika?

Je wakati Charles Makongoro Nyerere anahama kwenda mkoa mwingine, je wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama tangu wilaya ya Babati na mkoa walibaki wangapi? Je mwenendo wa utoaji wa taarifa dhidi ya Pauline Gekulwa wajumbe hao ulikuwaje ?



Je ulikuwa na mazuri mengi au mabaya mengi?

Jeshi la Polisi Tanzania ni miongoni mwa wajumbe wa kamati hizi za Wilaya na Mkoa, nakuomba msomaji wangu hawa mara nyingi Wakuu wa Polisi Wilaya na Mikoa wanahamishwa sana sana , katika hili tunawaondoa na hatupaswi kuwasonta kidole hata mara moja. Hapo zinabaki idara na taasisi zingine je mwenendo wao ulikuwaje tangu mwaka 2019 hadi kutokea utenguzi wa Pauline Gekul Novemba , 2023.

Nakuomba msomaji wangu tusema, wajumbe hao wa kamati hii walibaki wakapata mkuu wa mkoa mpya, je mgogoro huo wa Charles Makongoro Nyerere na Gekul utakuwa umeondoka au umebaki?

Msomaji wangu jibu unalo.

Mwanakwetu ana hakika kuwa Gekul kwa muda mrefu alikuwa na mahusiano mazuri na Katibu Tawala wa Wilaya hiyo, maana akiwa Naibu Waziri wa Habari na baadaye Naibu Waziri wa Utamadani , huyu katibu tawala ndiye mwenyekiti kamati ya michezo ya wilaya  na mara nyingi alishiriki vikao vya kiongozi huyu, hapo Mwanakwetu ameona kwa macho yake.

Hadi tukio hilo lililosababisha Gekul kupokwa Unaibu Uwaziri, Rais Samia Suluhu Hassan alifanya mabadiliko ya Baraza la Mawaziri ambapo Waziri Dkt .Damas Ndumbaro alihamishiwa Wizara ya Utamaduni Sanaa na Michezo naye Pindi Chana kuhamishiwa Katiba na Sheria. Kupelekwa Pindi Chana Wizara ya Katiba na Sheria maana yake Pauline Gekul alikuwa chini ya akina mama mwenzake.

Kwa hakika Pauline Gekul kule jimboni, jimbo hilo ni la mkoani, Gekul yupo chini ya mama mwenzake Mkuu wa Mkoa.

Swali ni je mahusiano baina ya Pauline Gekul na wanawake wenzake yakoje? Je Pauline Gekul anaweza kufanya kazi vizuri akiwa chini wanaume au chini ya wanawake wenzake? Katika hilo yupo anayefahamu jibu.

Je kuwa chni ya wanawake, mwanasiasa huyu ilikuwa ni makusudi au ilitokea tu?

Kwa bahati nzuri Mwanakwetu hilo alilifanyia kazi kwa kina na kuzungumza kwa kirefu na mwanasiasa mmoja wa Tanzania ambaye ni mwanamke anawafahamu kwa karibu Gekul na hata aliogombea nao kura za maoni CCM na huyu aliyeongea na Mwanakwetu ni mwenyeji wa huko huko.

“Kaka Makwega, kusema ukweli wa Mungu mahusiano ya Gekul na wanawake wenzake yana shida.Hilo ndiyo lilivyo kwa wanawake wengi na hata mimi naamini huwa hatupendani.”

Hilo Mwanakwetu lilimpa picha kuwa kama hilo ni kweli, Je Pauline Gekul kuzungukwa na akina mama wenzake ulikuwa mtego wa kumkwamsia ili aharibakiwe?

Hilo ni swali la kujiuliza.

Hapa tunaweza kwenda mbali zaidi, hawa akina mama waliongoza kura za maoni miongni mwao ni Wakuu wa Wilaya Je waliteuliwa kipindi cha John Magufuli ? Je hao akina mama hao wana mahusiano gani na mwenyekiti wa sasa wa CCM taifa?

Msomaji wangu Mwanakwetu ameukumbuka wimbo huu wa CCM wenye jina Kuzaliwa Kwa Chama.

.........................................................................................................................................

“Kuzaliwa Kwa Chama,

Cha Mapinduzi,

KImetuongezea Wananchi Imaniiii,

Matumainiiiiiii Na nguvu Mpya ,

Katika Kuendeleza Mapambano ya Ukombozi wa Afrika,

Sisi WanaCCM Lazima Tujenga

Siasa ya Kweli ya Kijama,

Tujihadhalishe na Tabia Mbaya,

Kama Vile Rushwa, Wizi Magendo Upendeleo na Ulevi  ooo Jamaa

Kwani Vitendo Hivyo Hudhohofisha Lengo Letu

Kwani Vitendo Hivgo Hudhofisha lengo Letu

La Kujenga Ujamaa na Kujitegemea.

..........................................................

Mwanakwetu anasema nini siku ya leo?

Msomaji wangu kwa hakika utenguzi wa Pauline Gekul ulifanywa kwa haraka, viongozi wetu wajenge tabia ya uvumilivu kwa wenzao, wananchi wa Tanzania ni wavumilivu mno kwa viongozi wao. Huko mtaani nchini Tanzania yapo mengi. Kwa hakika kila kiongozi wa taifa hilo tangu mkubwa na hata mdogo afahamu hilo, jamani vumilianeni.

Mwanakwetu Upo?

Mtaani Yapo Mengi, Kwa Wakubwa na Wadogo, Vumilianeni, Utenguzi Gekul Umeharakishwa.

Nakutakia siku njema.

makwadealdius@gmail.com

0717649257




0/Post a Comment/Comments