WAKWE WA NDUGU KIONGOZI

 



Adeladius Makwega-MWANZA  

“Ndugu mmoja alichaguliwa kuwa kiongozi pahala fulani, alifika pahala hapo na kufanya kazi vizuri na kwa juhudi zote. Katika kufanya kazi hapo kulikuwa na changamoto nyingi. Kwa hakika ufanyaji kazi wake ulikuwa kikwazo kwa baadhi ya watumishi wa idara za umma na wafanyabiashara wajanja wajanja. Misimamo ya kiongozi huyu ilibadilisha kabisa mwenendo wa maisha yao. Hivyo hilo kuwa kero kwao, hapo hapo changamoto zilianza kuibuka baina ya ndugu huyu na watu hao kuanza kumuwekea  vigingi na vikao tele.

Kwa bahati mbaya ndugu huyu alifanya kazi katika eneo ambalo wakweze ndipo wanapoishi. Kwa hakika hata mke wa ndugu huyu alikuwa akifanya kazi katika eneo hilo na yeye akiwa pia mtumishi wa umma. Huku kukiwa na mapambano ya hapa na pale kwa pande mbili zinazoshindana udhalimu na haki. Eneo hilo lilikuwa linapokea wageni wenye nyadhifa mbalimali kila mara . Kuna siku eneo hilo likapata ugeni wa Mkuu wa Mkoa na siku moja kabla ya ugeni huo. mke wa kiongozi huyu alienda kazini akakutana na bahasha juu ya meza ya ofisi yake. huku imeandikwa jina lake. Akajiuliza bahasha hiyo imewekwa na nani asubuhi hiyo? Akajaribu kuwauliza wafagiaji na walinzi hapo hakupata majibu . Akadhani kuwa ni hapo hapo ofisini, akakata shauri na kuifungua, ’Tunakuandikia barua hii , sisi ni wasamaria wema tu , tunakupenda sana, hiyo orodha ndefu ni ya wanawake ambao mumeo anatembea nao, hayo ni machache pambana nae.’

Mama huyu aliibeba barua hiyo na kurudi nayo nyumbani kwake na kumueleza mumewe na baadaye kumuonesha barua hiyo. jambo hilo likaibua ugomvi nyumbani hapo na kesho yake Mkuu wa Mkoa kufika na kuupokea ugeni huo vizuri huku kiongozi huyu akiwa na amani kubwa.

Ugeni uliondoka vizuri na kazi kuendelea vizuri, eneo hilo likapata ugeni mwingine Waziri wa anayeshughulia Serikali za Mitaa alitaja tarehe ya kufika hapo. Asubuhi ya siku moja kabla ya ugeni huo, huku mumewe akiwa ofisini kwake, mama huyu akiwa ofisini kwake akaingia ofisini akakakutana barua kama ile ya kwanza, huku ikimwambia,’Wewe ni mjinga kila siku tunakwambia juu ya mwanaume wako, kutembea na wanawake wengi, wewe unakaa kimya utakuwa mjinga? Jitambue mama, hapo unakuja kuondolewa.  Sasa mumeo kaamua kumuoa mwanamke huyu na wewe hauna chako.’

Mama huyu aliichukua barua hiyo na kwenda nayo nyumbani  kumuhoja mumewe ambaye alikuwa kiongozi katika eneo hilo. Baadaye kuleta taharuki nyumbani hapo na kumbuka siku iliyofuata ugeni wa waziri huyo ulifika na kukaa hapo kwa siku mbili na kuondoka salama.

Baada ya jambo hilo kupita salama. Ikapita muda kiasi na siku moja kukawa na maandailizi ya mwenge wa uhuru . Hapo mumewe akiwa miongoni mwa viongozi wa juu wa eneo hilo, aliendelea na kazi na huku nyumbani kwake maelewano hayapo na mandalizi ya mwenge wa uhuru yakipamba moto, siku moja kabla ya mwenge wa uhuru kufika hapo, mama huyu alifika ofisini mwake mapema akakutana na barua moja ndefu ikiwataja wanawake wote anaodaiwa mumewe anatembea nao na kumwambia, ‘Huyo mumeo ameathirika na VVU tayari, tunakwambia hivyo kwa kukupenda achana na habari za ujinga, pambania haki yako wewe.’

Mama huyu alipaombiwa hayo alitoka analia, akazimia ofisini kwake, kukimbizwa hadi  hospitalini , kupewa mapumziko , wazazi wake wakafika alipozinduka wakasimuliwa kilichotokea. Hapo hapo hapo wazazi wakaomba vipimo vifanyike. Wazazi wa huyu mama walikuwa washika dini mno, wakasali pamoja na kuimba wimbo wa TUFANI INAPOVUMA.

Wazazi hao walituma ujumbe wa ndugu wa kiongozi huyu wakafika nayeye kufanyiwa vipimo, alafu kikaitishwa kikao cha wanandugu

Huku zikiwa mezani zimekusanywa barua zote tatu kutoka kwa wafitini, familia ziliambiwa kuwa nyinyi wenyewe mnafahamu afya zetu, je haya yanayosemwa ni ya kweli au uwongo? Jibu lilitolewa kuwa ni uwongo. ‘Jamani kuweni makni na maneno ya watu, barua hizo ziliandikwa kimkakati , kwanini wasingesema kwa mdomo ?Iweje wawe wanaandika barua tu? Iweje wawe wanafanya hivyo  kipindi jirani na ugeni mkubwa katika eneo hilo?’

Jambo hilo lilikwisha na kuondoa mzizi wa fitna katika familia hii.”

Maswali ni mengi, je barua hizo  ziliandikwa kwa manufaa ya ushahidi wa nani?

Je nani mwingine alikuwa akipokea nyaraka hizo na zilitumwa wapi?



Haya ni baadhi ya maswali ambayo familia ya Wakwe wa Ndugu Kiongozi walihoji , jamani tuweni makini sana hawa wanaofanya kazi ni watoto wa watu.

Kwa nini Mwanakwetu anasimulia kisa hicho leo hii?

Yote hayo ni juu ya tukio la mheshimiwa Pauline Gekul ambalo mpaka sasa limegharimu Unaibu Waziri wa Sheria na Katiba.

Kikubwa kwako msomaji wangu unapoona jambo lolote linafanywa na watu , tambua dunia ina watu wazuri kwa wabaya na watu wabaya wana mahesabu makali mno kuliko mahesabu ya watu wema.

Kama kweli tukio hilo siyo njama kwanini lisingefanywa muda mfupi baada ya uchaguzi mkuu wa 2020? Watu wanatambua kuwa 2024 ni wakati wa uchaguzi wa Serikali za Mitaa wanajiandaa mapema kabla ya 2025 kumpoteza mhe. Pauline Gekul.

Mwanakwetu ana hakika hata mhe Pauline Gekul akiwa Naibu Waziri wa Habari mara nyingi  alikuwa anatembelea jimbo lake na muda mwingi alikuwa anahangaika na kufanya vikao vingi na wapiga kura wake huku akipambania jimbo lake na wakati mwingine hata kulala ilikuwa tabu..

Mwanakwetu anamlinganisha Pauline Gekul na yule kiongozi wa serikali aliyekuwa anafanyiwa visa vya fitna za barua zile kwa mkewe ambapo wafitini walipata aibu.

Mwanakwetu upo?

Jamani wafitini huwa wanapata aibu sana, kubwa na kumuomba Mungu tu wafitini kuwashinda na tusiweze kuingia katika mitego yao kama ilivyokuwa kwa Wakwe wa Ndugu Kiongozi

Nakutakia siku njema.

makwadeladius@gmail.com

0717649257



0/Post a Comment/Comments