MAMA MPOGORO MBAGALA

 



Adeladius Makwega–MWANZA

Mwanakwetu ana dada zake binamu kadhaa ambao wanazaliwa kutoka kwa baba wa makabila mbalimbali, maana Mwanakwetu ni tajiri wa mashangazi, hata akiamua kuwataja dada zake hao binamu katika makala mmoja baada ya mwingine , makala zitakuwa nyingi.

Mmoja wa binamu zake anayezaliwa na shangazi zake, anaitwa Piensia Nyema, mara kadhaa amekuwa akitajwa katika makala za Mwanakwetu, kwa tabia tangu utoto Piensia alikuwa binti mkimya mno, si muongeaji sana, mwenye machache maneno na hata kama anaongea basi kwa yule anayempenda.

Hiyo ni haiba ya binamu huyo wa Mwanakwetu, katika ya miaka kati ya 30 na 40 iliyopita,hiyo ni miaka mingi, msomaji wangu ni siku nyingi,haya ni kwa mujibu wa shajara ya Mwanakwetu yanakufikia hapo ulipo.

Wakiwa wadogo ndugu hao, huyu Piensia alikuwa ni mpikaji mzuri wa chakula hasa wali, kwa kuwa yalikuwa mazingira ya Pwani uungaji wa vyakula ulikuwa ni wa nazi tu, nyakati hizo ulaji wa vyakula kwa mapishi yaliyoungwa na mafuta ulikuwa mdogo sana kwa makabwela labda kwa mabepari waliweza kununua makopo ya mafuta, mwendo ulikuwa nazi, machicha ya nazi na jalalani vifuu vya nazi kibao.

“Wali wa Piensia Nyema ukipikwa ulikuwa hauwi ubwabwa, unakuwa wali mzuri , huku punje za wali huo zikihesabika vizuri , moja baada ya nyingine.”

Sifa hiyo ya mapishi hayo Mwanakwetu anakumbuka sana, maana yeye ni Mpogoro, Mpogoro wali, sifa hii ilikuwa ya binamu pekee hapo nyumbani , yalipokuwa makazi ya Fidelis Makwega, babu wa Mwanakwetu.

Wengine hawakujaliwa hata kuisogelea sifa hiyo , yaani upikaji huo mzuri wa wali, kwao hawa wengine ulikuwa ni mapishi mabaya na safari ya mapishi mazuri na mabaya ilikuwa sawa na mbingu na ardhi.

Piensia alipopata dharura maneno yalikuwa mengi,

 

“Ubwabwa leo, utadhani wagonjwa wa Mwaisela.”

Msomaji wangu Mwaisela ni jina la wodi mojawapo maarufu katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili jijini Dar es Salaam wakati huo hakuna Mloganzila.



Piensia Nyema ambaye sasa ni mama wa watoto kadhaa, akikaribia kujukuu, akiwa ni Afisa Utumishi Mwandamizi katiika Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, yeye alikuwa na sifa nyingine, wakati anapika alikuwa kimya jikoni na sauti yake ilisikika tu chakula tayari mezani katika sinia,

“Jamani njooni mle.”

Palipakuliwa masinia mawili, moja la wanaume na moja wanawake, sinia la wanaume lilikuwa na watu wachache hivyo baadhi ya wasichana waliongeza nguvu ya kutupa mawe pangoni katika sinia la wanaume, ili kuwianisha chakula cha sinia la wanawake na la wanaume. Hapa Piensia aliweza kupima kipimo cha haki cha chakula hicho na kila mara yalisikika maneno haya,

“Jamaniee, hilo sinia lenye wanaumeongezeni chakula, wao wanakula sana.”

Hapo sinia la wanaume mezani, sinia la wanawake katika mkeka na waungwana walianza kula wali unaohesabika punje uliopikwa na Piensia Nyema, binti wa Kingoni na Kipogoro.

Maswali yalikuwa mengi, inakuwaje mapishi ya Piensia Nyema ya Wali mazuri kuliko ya wengine?

Kumbuka kwa Baba ni Mngoni Kwa Mama ni Mpogoro wa Mbagala. Wadau nyumbani wakisema,

“Piensia ni hodari wa kupika, hizo ni juhudi zake binafsi na huyu ataolewa mapema.”

Hizo zilikuwa dua za kina Mwanakwetu kwa binamu yao, mambo yakawa hivyo hivyo na alipomaliza chuo kikuu Mzumbe aliolewa.

Ndiyo kusema dada wengine wa Mwanakwetu wakiwa jikoni hapo tulisikia maneno mengi ,

“Haya leta chujio la nazi, leta chumvi, choteni maji, unga umekwisha ”

Jikoni ukishaona Piensia hayupo, kumbuka hapo hautotoka nyumbani hadi mapishi yakamilike,

“Miito hiyo itajirudi mithili ya santuri iliyogoma kucheza usiku wa manane katika ukumbi wa muziki.”

Hawa binamu wote wa Mwanakwetu walikuwa na faida, siyo Piensia peke yake, hawa waitaji wa kila mara walisaidia vijana wa kiume kuweza kujifunza kiasi namna ya kupika , japokuwa walimu wenyewe walikuwa si wapikaji wazuri, lakini walimtoa mtu kutoka hatua moja kwenda nyingine.

“Jamani mjifunze funze hata kuchemsha chemsha, maana mkianza maisha yenu, mtafakamia mapishi ya watu, mtalishwa na visivyolika. Hata wasichana nyinyi mjifunze funze shughuli za akina baba kuna leo na kesho, unatakiwa kuokoa jahazi.”

Hawa mabigwa wa kuita walipata nguvu zaidi baada ya kusikia Bi Getrude Mongella kaingia katika Mkutano wa Bejing’ mwaka 1995 sasa ikiwa ni miaka 28 iliyopita tangu mkutano huo kufanyika nchini China.

Jamani mjifunze funze hata kuchemsha chemsha, maana mkianza maisha yenu, mtafakamia mapishi ya watu, mtalishwa na visivyolika. Hata nyinyi mabinti mjifunze shughuli za kina baba kuna leo na kesho unatakiwa kuokoa jahazi.



Haya Mwanakwetu anayakumbuka tu maisha ya nyumbani kwao Mbagala miaka karibu 40 iliyopita yeye na ndugu zake.

Mwanakwetu siku ya leo anasema nini?

Mwanakwetu siku ya leo amekumbuka kisa hicho cha dada zake nyumbani kwao, akiamini kwamba siyo kwamba Mkutano Beijng’ ulikuja na kitu kipya la hasha bali ulikuja kuipa nguvu mijadala ambayo ilikuwa inajadiliwa na jamii, nyumbani, shuleni na katika maeneo mengine.

Huu Mkutano wa Beijing ‘ uliwapa nguvu dada za Mwanakwetu waliokuwa wanapika wali vibaya lakini walitoa nafasi ya vijana wa kiume kujifunza kupika angalau kuchemsha chemsha ili wasilishwe limbwata/ litambulila baadaye wakiwa watu wazima.

Ndiyo kusema Mkutano wa Beijing’ pia ulisaidia vijana wa kiume wa wakati huo kuwafahamu wanawake ni watu wa namna gani? Ulimwengu wao una nini? Hata kuwalinda vijana hao kutoingia katika matatizo wanapokuwa watu wazima ambayo mengine yanaweza hata kusababishwa na wanawake , kama ilivyo baadhi ya wanaume wanavyoweza kusababisha shida kwa wanawake.

Popote ulipo Piensia Nyema, salaam tele kutoka kwa nduguyo Mwanakwetu anakusalimia sana leo hii umesababisha amkumbuke bi Getrude Mongella na Mkutano wa Beijing’,

“Piensia Nyema dada yangu, nakujulisha kuwa Noeli ya mwaka huu hodi nyumbani kwako .”

Kwako Bi Getrude Mongella ,kwanza shikamoo ! popote ulipo, tunashukuru kwa kutuwakilisha vema huko Beijing’ China wakati huo, Mwanakwetu anauliza swali, ameona picha moja uliyopiga na Mummar Gaddaf inamtia mashaka na wivu kwa urafiki wako na kiongozi huyu wa Libya ambaye ni marehemu , angeweza kumuuliza Gaddaf lakini hayupo katika upeo ya macho yetu, tunakuuliza wewe bibi yetu mpendwa, tupe siri  na hekima ya ujirani wako na kiongozi huyu, hadi kakuegemea? Bibi Gerude Mongella ,Je Jamhuri ilitoa kibali?

Mwanakwetu Upo?

Mama Mpogoro Mbagala 

Nakutakia siku njema.

makwadeladius@gmail.com

0717649257



0/Post a Comment/Comments