MSIRUHUSU NAFASI YA SHETANI MIOYONI MWENU-PADRI MASANJA

 



Adeladius Makwega-MWANZA

Wakristo wameambiwa kuwa wasiruhusu nafasi ya shetani katika mioyo yao, maana wanaweza kuonekana wanasali lakini hilo litakuwa sawa na bure.

Hayo yamesemwa na Padri Samson Masanja, Paroko wa Parokia ya Malya, katika Kanisa la Bikira Maria Malkia wa Wamisionari , Parokiani hapo, Jimbo Kuu Katoliki la Mwanza katika misa ya kwanza ya Dominika ya Nne ya Mwaka B wa Liturjia ya Kanisa Januari 28, 2024.

“Tunaporuhusu nafasi ya shetani katika maisha ya mioyo yetu , tunaweza kuonekana watu tunaosali, watu tuonasema maneno ya Mungu, watu tunaotangaza neema za Mungu lakini kama ndani yetu hatuna upendo wa Yesu, kama ndani yetu hatuna upendo kwa wenzetu, haya maneno yetu yatakuwa sawa na debe tupo .”

Akiendelea kuhubiri katika misa hiyo Padri Masanja alisema kuwa Kristo leo hii anatuamuru sote tutoke katika hali hiyo maana na namna hiyo neno lake linaleta uponyaji katika maisha yetu na linatela uponyaji katika nafsi zetu.



Padri Masanja aliongeza kuwa anachotaka kusisitiza Mtume Paulo katika somo la Pili la dominika hii,

“Hao walioa na hao ambao hawajaoa, sote tunapaswa kuwa na nguvu zaidi ya kumtumikia Mwenyezi Mungu bila ya kuchukuliwa na mambo ya ulimwengu huu.”

Misa hiyo ilikuwa na nia na maombi kadhaa,

“Eee Mungu Baba utuimarishe katika imani yetu, ili tuweze kupambana na pepo wa wabaya hapa duniani, Eee Bwana-Twakuomba Utusikie.”

Misa hii ilifanyika katika hali ya utulivu mkubwa, baridi kidogo, mawio ya jua yakichelewa kidogo , nayo mvua ikinyesha kwa kuruka ruka siku, mashambani sasa wakulima wakijituma mno katika majaruba yao ya mpunga na wakulima wengine wakipanda mimea jamii ya kundekunde kwa mara ya pili.











0/Post a Comment/Comments