MUAMUZI MUDA

 



Adeladius Makwega-MWANZA

Msomaji wangu kwa heshima na taadhima, itazame hiyo picha vizuri, kwa hakika mheshimwa Spika wa Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anaonekana akiwa na ndugu mmoja ambaye amevalia suti ya rangi ya samawati.

Kwa utafiti wa Mwanakwetu umebaini kuwa picha hiyo ilipigwa nchini Tanzania na ilipatikana katika maktaba ya Mwanakwetu lakini haifahamiki picha hiyo ilifikaje katika maktaba hiyo.

Ukiwatazama hao ndugu vizuri, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anaonekana kucheka na huyu jamaa mwenye suti ya rangi ya samawati akicheka pia.

Baada ya Mwanakwetu kufuatilia sana ilibainika kuwa picha hiyo ilipigwa na Mbunge wa Mlalo mhe Rashidi Shangazi ambapo mhe Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwa Naibu Spika alipotembelea Jimbo la Mlalo, mkoani Tanga mwaka 2018.

Mwanakwetu alitamani kumfahamu aliyekuwa kando ya Spika Tulia, alimfahamu vizuri na alipotaka kufahamu maneno yaliyosemwa na ya kumchekesha mhe Dkt Tulia siku hiyo yalikuwa yepi?

Majibu yalkuwa haya , huyu jamaa mwenye Suti ya rangi ya samawati alimwaga mtama huo kwa Mwanakwetu.

“Sasa mheshimiwa Dkt Tulia, itabidi nichukue kigoda ili nilingane urefu na wewe, alafu nikawalingishie kwetu machakani kuwa leo hii nimepiga picha na spika na ninalingana naye urefu.”

Habari za Kuongeza Kigoda pia zilimchekesha Mwanakwetu, ukiitazama picha hiyo vizuri hao ndugu wawili wote wanacheka, wote weusi, wote hao ni Watanzania waliozaliwa  baada ya muungano wa Tanganyika na Zanzibar.Ukiitazama zaidi picha hii utaona kuwa Dkt Tulia na huyu jamaa wote wamefumbata mikono na mkono wa kulia juu na wa shoto ukitangulia.

Ukimtazama tena mhe Spika wetu kapiga gauni maridadi la kitenge, refu hadi chini, siku hizi mheshimwa spika haya mambo ameyaweka kando, yapo likizo kidogo, lakini katika hilo Mwanakwetu asijifanye anajua sana,  watu watasema,

“Wewe Mwanakwetu, huko machakani Kwimba-Mwanza unamuona lini na wapi Spika wetu Dkt Tulia?”

Hivi kweli kujua hilo ni kazi ngumu? Hiyo ni kazi nyepesi tu, itabidi nimpigie simu Mbunge wa Kiteto, Mr Edward Ole Lekaita au Mbunge wa Malinyi Mhe. Antipas Zeno Mngungusi niwaulize.

“Kaka naomba mapigo ya Dkt Tulia mwezi huu yalikuwaje.”

Sasa waheshimiwa hao wakiuliza Mwanakwetu katika hayo mapigo ya Spika unataka nini? Nitawajibu nini mie Mwanakwetu?

Majibu yatakuwepo tu.

“Mimi mwandishi wa habari, nataka kumuandikia makala ya mavazi yake mh wetu, hapo mchezo umekwisha.”

Katika picha hiyo ukitazama vizuri huyu jamaa mwenye suti ya samawati kazidiwa urefu na Dkt Tulia na ndiyo maana jamaa aliomba kigoda ili alingane na mh Dkt Tulia. Jamaa kando ya  Dkt Tulia husuda hiyo ilimjia na aliweza kuisema kwa mhe siku hiyo.

Mwanakwetu alipoitazama picha hiyo tena na tena ilimjia picha ya Mr II -Josephy Mbilinyi ambaye aliwahi kuwa Mbunge wa Mbeya Mjini, ambaye Mwanakwetu anamfahamu kwa karibu tangu anaanza muziki wake akiwa kijana mdogo, aliwahi kuishi Mbagala na akifanya kazi ya ubawabu British Petroleum (BP) Kurasini, hizo ni habari za walikuwapo Dar es Salaam wakati huo tu.

Mwanakwetu alikumbuka kuwa Mr II alikuwa kijana mzuri, kosa ambalo akina Mwanakwetu walifanya kutomuozesha Mr II, kwa hakika angekuwa sasa shemeji yao watu Mbagala , tungekuwa tunagawana naye mirabaha sijui mirahaba ya nyimbo zake, lakini watu wa Mbagala waliweka mitego mingi ya Ndoa za Mkeka lakini akina Mwanakwetu walishindwa kuongeza juhudi katika hilo, sasa hivi lazima tujilaumu.

Kumbuka msomaji wangu kama nilivyokwambia hapo juu hizi ni habari za waliokuwapo Dar es Salaam wakati huo.

Picha hiyo hapo juu ikambeba mzega mzega Mwanakwetu hadi mwaka 2025 Mbeya Mjini, mambo yatakuwaje wakati wa uchaguzi mkuu?

“Mwanakwetu hakuwa na majibu maana hao wote ni nduguze.”

Mwanakwetu siku ya leo anasema nini?

Huyu Sugu je ataweza kuutumia ule Ujanja wa Mjini / Ujanja wa Da es Salaam alivyoweza kupenyepenya na kuibuka kinara wa muziki wake hadi Wazaramo/ Wandengereko akina Mwanakwetu walivyomkosakosa na ndoa za mkeka za dada zao? Je Utamsaidia kushinda ubunge?



Au mambo kwa Dkt Tulia yatakuwa kama hii picha inayoonekana kuwa unapotaka kumfikia Dkt Tulia kwanza una kazi ya kukitafuta kigonda cha kulingana naye, ukishamaliza kazi hivyo ndiyo uanze harakati za kumvuka, nayo ni kazi nzito! Kama huyu baba mwenye suti ya samawati alivyoshindwa akabakia na kicheko?.

Mwaka 2025 si mbali; mwaka, miezi, juma, siku ,saa , dakika na sekundu zinasonga kidogo kidogo, tungoje muda uamue.

“Mwanakwetu anatambua MR II ni nduguye na Dkt Tulia ni dada yake. Sisi sote ni Watanzania, lazima tuijenge nchi yetu viwavyo na iwe.”

Mwanakwetu Upo?

“2025 si mbali Je ni Ndoa za Mkeka au Sogeza Kigoda, Mwanakwetu anasema Muamuzi ni Muda.”

Nakutakia siku Njema.

makwadeladius@gmail.com

0717649257



0/Post a Comment/Comments