MAAMUZI MENGINE YANAHITAJI HEKIMA.

 



Adeladius Makwega-MWANZA

Juni 28, 2024 Mwanakwetu alipata mualiko wa mahafali ya Vijana wa Kikristo wa Vyuo vya Kati na Vyuo Vikuu Tanzania UKWAVITA wanaomaliza masomo yao katika kozi kadhaa za michezo Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya(MCSD).

Katika mahafali hayo yalifanyika mengi na kuzungumzwa mengi, kubwa ni mahubiri ya Mchungaji Simon Edward wa Kanisa Anglikana Tanzania ambao yalitumia dakika 10 huku yakibeba ujumbe mzima kwa kila Mtanzania hususani wale wenye nafasi za umma.

Kwa heshima ya Kanisa la Anglikana Tanzania na kwa heshima ya CCT Mwanakwetu anaamua kuyaweka mahubiri haya katika makala haya ili yaweze kuifikia kila nafsi yenye uhai katika ardhi ya Tanzania na popote ulimwenguni kadili Mungu atakavyowezesha, shabaha yake mahubiri hayo yaweze kuvuka kuta la Kanisa la AICT Malya Mwanza ambapo shughuli hiyo ilifanyika.

Mwanakwetu anatambua CCT inayo idara yake ya habari awali ikiogozwa na rafiki wa Mwanakwetu Mchungaji, Mwalimu John Magafu lakini sasa inaongozwa na Mchungaji John Kamoyo, makala haya yajaribu kuonesha namna mahubiri haya kutoka kwa Mchungaji Simon yanavyoendana na wakati wetu wa sasa.

Katika mahubiri haya yalisemwa haya;

“Leo nazungumzia somo la haki, najua ninazungumza na viongozi mbalimbali wa Kanisa na Serikali, katika biblia(Vitabu 66) neon haki limeandikwa mara 815, neno haki kuandikwa mara zote hizo toka 1-815 ina maana kubwa kwa mwanadamu. Agano Jipya pekee neno haki limeandikwa mara 214 na Kwa Agano la Kale limeandikwa mara 601.

Biblia inasema haki huinua taifa na wewe kama kiongzi tenda haki, mtenda haki sawa na msema kweli huwa hapendwi na watu wengi.Watu wengi tuna tabia ya kuwavunja moyo watenda haki lakini wewe kama mtenda haki usivunjike moyo.

Mwanzo 6,9 ‘Hivi ndivyo vizazi vya Nuhu , Nuhu alikuwa mtu wa haki, mkalimifu katika vizazi vyake, Nuhu alikweeda pamoja na Mungu.’ Biblia inasema kuwa walikuwepo watu waovu lakini Nuhu alisimama katika haki. Siku zote wewe kama kiongozi mambo yatakuja katika ofisi yako, pata muda wa kufikiria na kutafakari kabla ya kutenda.Naomba niwasimulie kisa hiki;

Siku moja watu walikwenda katika mahojiano ya kazi, katika mahojiano haya watu watatu wakafungana kwa alama, waamuzi wakawa njia panda, maana nafasi ni moja tu.

Wakawaita ndugu hao na kuwahoji tena wakachunjwa ndugu mmoja wakabaki wawili.

Kamati ya mahojiano ikawa njia panda tena maana bajeti  ni ya mtumishi mmoja je wanafanyaje?

Mmoja wa wahusika akatoa wazo likakubalika kwa kuwachukua ndugu hao hadi Mkahawani wakahudumiwa kila mmoja kikombe cha chai anywe, walipopewa chai hiyo mmoja alichukua kijiko cha sukari na nakuongeza sukari vijiko kadhaa, mwingine alichukua kijicho na kuonja chai yake alafu akaongeza sukari , mchana walipewa chakula mmoja alizogeza bakuri la mboga a kuongeza chumvi alafu kuanza kula na huyu mwingine alionja mboga yake na kubaini ina chumvi kidogo  alafu akaongeza chumvi.

Yule  aliyeongeza sukari kabla yakuonja ndiyo yuleyule aliyeongeza chumvi katika mboga kabla ya kula. Huyu aliyeonja chai na mboga kabla ya kunywa na kula alipewa kazi maana alionekana akiwa kazini atafanya maamuzi baada ya kuyachunguza’

Mnaohitimu na wengine wote mnakwenda huku mkaamue kwa haki. Wengine hapa ni waamuzi wa mchezo wa soka hata kama wewe ni Simba au Yanga unachezesha mchezo jukumu lako ni kuchezesha kwa haki.”

Katika mahafali hayo mdau mmoja kando ya mwandishi wa makala haya akasema , kama ukiwa muamuzi alafu hautendi haki kila siku utapigwa na mashabiki.

“Kwa hali ya sasa mashabiki wataweza kukufuata hadi nyumbani kwako na kuinyima raha hata familia yako.”

Mahubiri ya mchungaji Simon Edward yaliendelea madhabahuni.

“Mathayo 5 , 10

‘Heri wenye kuhuziwa kwa ajili ya haki maana ufalme wa mbinguni ni wao.’

Ukitenda haki watu wengi watakwenda kinyume na wewe lakini siku zote hekima ya Mungu Ikuongoze.”

Mchungaji Simon Edward alitoa mfano mwingine,

“Kuna wakati nilikuwa mchungaji mahali fulani nilipata changamoto, mke wa mzee mmoja wa kanisa alikuwa akitembea na mwenyekiti wa kwaya.Nikabaini yale mahusiano je maamuzi gani yanafanyika?Jambo hili nikaliweka katika maombi, kulitangaza kanisa ni hatari linaweza kuhatarisha ndoa ya mzee wa kanisa na mkewe.Baadaye nikaamua kumsimamisha kwa siri mwenyekiti wa kwaya huku akitambua kosa lake. Jambo hilo likaleta malalamiko kwa wazee wa kanisa, inakuwaje mchugaji anajiamulia mambo bila kutushirikisha?Mlalamikaji mkubwa aliyekuwa Kiranja ni Mzee wa Kanisa Mweye Mke Mzinzi.

Hali ya Kanisa ilikuwa ya moto, Mchungaji nafanyaje?

Siku moja Baba Askofu alitembelea Kanisa letu yakazungumzwa mengi na langu la kumsimamisha mwenyekiti wa kwaya likatajwa na yule Mzee wa Kanisa Mwenye Mke Mzinzi,

‘Mchungaji Anafanya Maamuzi Bila ya Kutushirikisha.’

Baba Askofu akanipa nafasi kujbu nikasema Jamani eeh Kuna Maamuzi Mengine Yanahitaji Hekima na Ukishirikisha unasambaratisha Kanisa. Baba Askofu akasema mchungaji sema Nikiwa hapo nikaumwaga mtama hadharani kuwa mwenyekiti wa kwaya anatembea na mke wa mzee wa kanisa, hivyo nilitumia hekima kutowashirikisha wazee wa kanisa, wazee wanauliza mke wa nani? Akaambiwa aliyeuliza hilo kuwa mkeo. Mwenye mke alizimia mbele ya baba Askofu, Jamaa alipewa huduma na baadaye alizinduka.

Maamuzi mengine yanahitaji hekima.

Ndiyo maana Injili ya Mathayo inasema Heri wenye kuuziwa kwa ajili ya haki maana ufalme wa mbinguni ni wao.

Mathayo 27, 24 ‘Basi Pilato aliona yakuwa hawafanyi lolote bali ghasia, alichukua mikono yake na kunawa, akisema yeye hataki mtu huyu ahukumiwe, bali muhukumuni nyinyi wenyewe.’

Hapa tunaona Pilato anawaogopa wanadamu, usiwaogope wanadamu.

Mithali inasema kumuogopa mwanadamu kunalea mtego. Wewe kama kiongoz fanya muamuzi wa haki usiangalie wanadamu wanasema nini?

Mithali 10, 27 ‘Kumcha Bwana kunaongeza siku za mtu bali miaka yao wasio haki haki itapunguzwa.’ Pia Mithali 11,8 ‘Mwenye haki uokolewa katika dhiki, mwovu ataingia badala yake.’

Mchungaji Simon Edward alimalizia na haya,

“Muendako mkatende haki

Luka 14 ,14 ‘Na utakuwa heri maana hakuna cha kukulipa maana utalipwa mbele ya ufufuo wa Mungu.’

Nendeni mkatende haki bila ya kujali mliowakuta wanafanya nini.”


 

Mwanakwetu anasema nini siku ya leo?

Mchungaji Simon Edward alimaliza mahubiri yake na baadaye kugawa vyeti kwa wahitimu hao.Hapa kila mmoja wetu analo la kujifunza nah ii ndio shabaha ya Mwanakwetu kuyaandika makala haya.


 

Mwanakwetu Upo

Kumbuka

“Mchungaji Afanya Maamuzi Bila ya Kutushirikisha.- ”

Nakutakia siku Njema

makwadeladius@gmail.com

0717649257











 

0/Post a Comment/Comments